WATAALAM WA KILIMO KUTOKA ANSAF WATEMBELEA KIJIJI CHA MAISHA PLUS NA KUTOA MAFUNZO YA KILIMO.

    Kulikuwa na mdahalo kijijini ulioendeshwa na wataalamu wa kilimo kutoka ANSAF (Agricultural No State Actors Forum) ambalo limejikita ... thumbnail 1 summary
 
 Kulikuwa na mdahalo kijijini ulioendeshwa na wataalamu wa kilimo kutoka ANSAF (Agricultural No State Actors Forum) ambalo limejikita katika kushawishi serikali na wadau wa kilimo, kusaidia wakulima wadogo wadogo, kuimarisha fursa zilizopo na kuongeza myororo wa thamani katika kilimo. Mdahalo huu uliongozwa na Mkurugenzi wa ANSAF Audax Rukonge na wanajopo wengine Elias Rwekeza Mkurugenzi Mtendaji wa OppAccess Co. Ltd iliyopo Morogoro, Mwenyekiti mwanzilishi wa Tanzania Graduate Farmers Association Stephano P. Kigazi, Ernest Likokoo kutoka TGFA, Brendalinny John na Epiphania Mngazija kutoka ANSAF. Katika mdahalo huu upatikanaji wa taarifa sahihi katika kilimo umetiliwa mkazo ili kumuweka mkulima katika hali ya kuweza kufanya maamuzi sahihi yanayohusu kilimo na kuweza kumpatia tija zaidi.


Vile vile wanakijiji cha Maisha Plus walipata fursa ya kuweza kupata maelezo ya hatua zinazotakiwa kufuatwa katika ujenzi wa jiko la gesi kuanzia ujenzi wenyewe, mitambo na matumizi yake, gesi yenyewe inavyozalishwa na hatimaye tope chujio. Tope chujio ni hatua ya mwisho ya uzalishaji gesi ambayo ni mbolea nzuri na yenye ubora kwa mimea tunayozalisha. Darasa hili lilitolewa na Richard Daniel ambaye alikuwa bega kwa bega na wanakijiji cha Maisha Plus katika hatua zote za ujenzi akisaidiana na mwanadada Theopista Mapunda katika hatua ya awali.
 Jiko hili tayari lilizinduliwa rasmi na mama Tunu Pinda na kuanza kutumika na wanakijiji. Kila kaya ya kijiji cha Maisha Plus hupata fursa ya kupika katika jiko hilo la gesi na kupunguza adha ya kutafuta kuni wakati huo huo kutunza mazingira kwa kuepuka kukata miti ovyo. 

Ile azma ya kundi lililoshinda kutumikiwa na makundi yaliyoshindwa imetimia baada ya kundi hilo kuibuka kidedea katika kutambua vitu mbalimbali huku wakiwa wamefunikwa macho kwa kitambaa cheusi. 

Kila mwanakikundi alipewa mjakazi wa kumtumikia na kufanya yale yote aliyoagizwa na mfalme au malkia kwa kuwa kundi hilo walipewa cheo cha malkia kwa wanawake na mfalme kwa wanaume. Wafalme wengine waliamuru wajakazi wao wawabebe mahali popote waendapo hapo kijijini kama ilivyokuwa kwa mfalme Said Rashid kutoka Uganda alimtaka Asumta Mwingira wa Tanzania atembee naye popote pale aendapo. Kwa malkia Flora John wa Tanzania alimtaka Caron Abisai kutoka Kenya amwimbie na kumpigia gitaa ili apate kuburudika. Wanakijiji walikuwa na pilika pilika za hapa na pale kuwatumikia wafalme na malkia kijijini hapo.