Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ( TFS) kumi bora Kwenye Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi, Ombeni Sefue, amewataka Watumishi wa Umma kuwa wabunifu katika kutoa huduma kwa wananchi ili kuleta ufanisi u... thumbnail 1 summary
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi, Ombeni Sefue, amewataka Watumishi wa Umma kuwa wabunifu katika kutoa huduma kwa wananchi ili kuleta ufanisi uwazi na uadilifu.
Aliyasema hayo katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam. 


Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika kwa wiki moja yakiwa na Kauli Mbiu isemayo ’’ Mkataba wa Msingi wa Kanuni za Utumishi wa Umma Barani Afrika ni Chachu ya Kuimarisha Utawala Bora na Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi’’yamewapa fursa Watumishi wa Umma kubadilishana uzoefu na wananchi wapatao laki tano.


Aidha, Maadhimisho hayo yaliyoambatana na utoaji tuzo kwa washiriki waliofanya vizuri katika vipengele mbalimbali, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) wamekuwa kumi bora kati ya taasisi 88 zilizoshiki kwenye maadhimisho ya wiki ya Utumishi wa Umma katika kipengele cha ubunifu.


Wakala wa huduma wa Misitu Tanzania ( TFS) imetajwa kufanya vizuri katika kipengele cha ubunifu wa kuzuia moto kwa kutumia njia ya kisasa inayowezesha kugundua moto mara tu unapoanza kuwaka mahali popote nchini.


Hivyo ubunifu wa teknolojia hiyo ya kuzuia moto itasaidia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kupunguza tatizo la moto ambalo limekuwa likiteketeza misitu mingi nchini.
‘’Wananchi wana matumaini makubwa sana na ninyi watumishi wa Umma hivyo wahudumieni vizuri hii itasaidia kupunguza malalamiko katika ofisi za umma’’ Balozi Sefue, alisisitiza.


Alisema kila Mtumishi wa Umma lazima ahakikishe anakuwa mbunifu ili kuweza kutimiza malengo yake aliyakusudia na aliwakikishia kuwa Serikali itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi kila mwaka.


Katibu Mkuu Kiongozi aliwaasa Watumishi Umma kuwa waaminifu na wachapa kazi kwani Maadhimisho ya Wki ya Utumishi wa Umma yamemsaidia kila Mtumishi Umma kuijtazama na kujitathmini katika utendaji wake wa kazi wa kila siku.


Aidha Wizara ya Maliasili na Utalii na Taasisi zake zilizoshiriki kwenye Wiki ya Utumishi Umma ikiwemo Bodi ya Utalii Tanzania, Chuo Cha Taifa cha Utalii, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania zimepata fursa ya kuwashirikisha wananchi kwa kutoa maoni yao jinsi ya kuboresha huduma wanazozitoa kwa lengo la kuhakikisha Maliasili zilizopo nchini zinalindwa na kuhifadhiwa kwa gharama yoyote kwa kuwashirikisha wananchi kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.