Kuwa mtoto wa mkulima na mfugaji kuna raha yake, lakini katika
Uwanda wa Wazi kwenye Hifadhi ya Taifa ya Arusha, hata wewe unaweza
kupiga picha na nyati kama nilivyofanya mimi. Inapendeza sana na matukio
kama haya hutokea mara chache sana katika maisha.
Na
Daniel Mbega, Arusha
Hifadhi ya Taifa ya Arusha inahusisha Mlima Meru, mlima maarufu wa
volcano wenye urefu wa meta 4566 (futi 14,977 au kilometa 4.6) kutoka usawa wa
bahari, na ipo katika Mkoa wa Arusha, kaskazini mashariki mwa Tanzania.
Hifadhi
hii ni ndogo iliyoanzishwa rasmi mwaka 1960, ikiwa na eneo la kilometa za mraba
137 tu, inavutia ikiwa na aina tofauti ya uoto katika maeneo matatu. Magharibi,
Kasoko ya Meru (Meru Crater) kuna Mto Jekukumia; kilele cha Mlima Meru
kinapatikana hapa. Kasoko ya Ngurdoto (Ngurdoto Crater) upande wa kusini-mashariki ni eneo la
nyasi nyingi. Maziwa madogo yenye vina vifupi ya Momella yaliyojaa magadi
kaskazini mashariki mwa hifadhi hii yanatofautiana kwa rangi na ni maarufu kwa
aina nyingi za ndege wanaopatikana huko.
Lango kuu la kuingilia Hifadhi ya Taifa ya Arusha.
Mlima
Meru ndio mlima wa pili kwa urefu Tanzania baada ya Mlima Kilimanjaro, ambao
uko takriban kilometa 70 tu mashariki na unaonekana vizuri ukiwa kwenye hifadhi
hii ya Arusha. Hifadhi ya Taifa ya Arusha inapatikana katika muhimili wa
kilometa 300 wa hifadhi za taifa maarufu barani Afrika, kuanzia Serengeti na Kasoko ya Ngorongoro (Ngorongoro Crater) upande wa maharibi na Hifadhi ya Taifa ya
Kilimanjaro upande wa mashariki.
Usitishwe na viwango hivi, ni gharama nafuu sana kwa Mtanzania kutembelea hifadhi zetu. Utamu wa ngoma ingia ucheze ati.
Hifadhi
hii ipo kilometa chache tu kaskazini mashariki mwa Jiji la Arusha, ingawa lango
kuu la kuingilia lipo umbali wa kilometa 25 mashariki mwa jiji. Pia iko umbali
wa kilometa 58 tu kutoka Moshi mjini na kilometa 35 kutoka Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
WAMERU WAKATIZA KWA MIGUU
Ukiwa katika Hifadhi ya
Taifa ya Arusha siyo tu utafurahia kuangalia mandhari nzuri ya asili
iliyosheheni hayawani na ndege wa kila namna, bali utajifunza na historia ya wakazi
wa maeneo hayo, hasa Wameru na Waarusha. Wameru ambao wanakaa katika miteremko
ya Mlima Meru walihamia hapo zaidi ya miaka 300 iliyopita na kwa sasa
wanadhaniwa kuwa idadi yao ni milioni 2.
Wameru hawa
wanahusiana jina tu na wale wa Kenya, lakini historia yao ni tofauti. Hawa wa
Tanzania wanasemekana kuwasili kwenye miteremko ya mlima huo mkubwa wakitokea
kwenye Milima ya Usambara katika Mkoa wa Tanga miaka 300 iliyopita, waliwasili
pamoja na Wachaga-Wamachame wa kwanza. Walipowasili katika miteremko ya mlima
kusini-mashariki waliwakuta jamii ya wawindaji waliofahamika kama Wakoningo,
ambao walizamia kwenye jamii ya Wameru. Waarusha wao asili yao ni Wapare na
walifikia Arusha Chini, lakini wakaathiriwa na tamaduni za Kimasai na
kushawishiwa kuishi upande wa magharibi uliko mji wa Arusha.
Wamasai nao walikuwa
kwenye mteremko wa mlima wakifuga kama ilivyokuwa kwa Waarusha. Katika miaka ya
1830 Wameru walipoteza ng’ombe wao wengi kutokana na vita dhidi ya Wamasai
waliotaka kuhodhi mifugo yote pamoja na maeneo ya malisho. Wameru wakakimbilia
upande wa pili wa mlima kutafuta hifadhi.
Kwa kutambua kwamba
mlima na misitu ndiyo iliyowaokoa, Wameru tangu enzi hizo wamekuwa wahifadhi
wazuri na hawakuweza kuharibu mazingira huku wakiendelea na kilimo cha mazao
mbalimbali, ikiwemo kahawa. Ni watunzaji wazuri wa ardhi kutokana na historia
ya eneo hilo ambalo limekuwa na migogoro ya ardhi tangu enzi za utawala wa
Mjerumani.
Hata kabla haijatangaza eneo hilo kuwa hifadhi mwaka 1960, Wameru wamekuwa wakikatiza kwa miguu msituni kutoka Arumeru kwenda upande wa kaskazini hadi Ngarenanyuki na vijiji vingine vya huko. Barabara kuu inayokatiza kutoka kwenye Lango la Ngongongare (kwa Kimasai ni Engong Engare – Eneo la Majimaji) upande wa kusini kuelekea kaskazini kupitia geti la Momella, inaelezwa kwamba inakwenda mpaka Kenya.
Kwa hali
hiyo, siyo ajabu ukifika kwenye mageti hayo au hata ukiwa hifadhini ukakutana
na bodaboda au watu wanaotembea kwa miguu, kwani ndiyo njia kuu wanayoitumia
wananchi wa huko, hasa wa upande wa kaskazini mwa hifadhi ambao mahitaji yao
wanayapata Arumeru na Arusha.
MAKAZI YA WAZUNGU
Ni
ukweli usiopingika kuwa Meru imejazana na kubanana na Wazungu toka maeneo
mbalimbali dunia. Ni kama historia mpya inayojirudia toka enzi za mababu zetu
kuwa Meru ni sehemu mojawapo salama zaidi ya kuishi nchini Tanzania kutokana na
hali yake ya hewa, mazingira mazuri pamoja na historia ya muda mrefu yenye
mvuto.
• Kila siku nyuzi joto za eneo la Meru zinaanzia 21 – 27 c ambazo ni nyuzi joto nzuri zaidi kwa kuuwezesha mwili wa mwanadamu kufanya kazi bila tatizo. Hali hii iliifanya Meru kuwa sehemu muhimu ya makutano ya mambo mengi ya kiserikali hasa mikutano, semina na mafunzo mbalimbali.
• Ni sehemu yenye vivutio vya asili kama vile mila na desturi zinazokaribisha wageni bila ubaguzi.
• Ni sehemu iliyo salama zaidi kiafya bila kuwepo na magonjwa yaliyozoeleka kama yalivyo maeneo mengine yalivyo na malaria, homa za matumbo (typhoid) na mengine mengi.
• Ni sehemu kuu na muhimu ya vyanzo vya maji vinavyounda Mto Pangani kupitia Bonde la Mto Kikuletwa yaliko makutano ya mito na mifereji yote ya Meru.
• Ni Meru tu inayomiliki mlima wa pili kwa urefu Afrika ambapo hifadhi ya aina yake ina aina ya Kima wasiopatikana mahali pengine hapa nchini. Hifadhi hii kwa historia ilikuwa shamba la mifugo ya wakoloni na sehemu yake ilikuwa shamba la mapapai.
• Zaidi ya yote ni Meru iliyo na ardhi na maeneo tofauti unakoweza kulima zaidi ya aina kumi tofauti za mazao na kustawi bila tatizo.
Wenyewe wanasema, “Meru ni Nchi ya Ahadi kwa Wameru”.
• Kila siku nyuzi joto za eneo la Meru zinaanzia 21 – 27 c ambazo ni nyuzi joto nzuri zaidi kwa kuuwezesha mwili wa mwanadamu kufanya kazi bila tatizo. Hali hii iliifanya Meru kuwa sehemu muhimu ya makutano ya mambo mengi ya kiserikali hasa mikutano, semina na mafunzo mbalimbali.
• Ni sehemu yenye vivutio vya asili kama vile mila na desturi zinazokaribisha wageni bila ubaguzi.
• Ni sehemu iliyo salama zaidi kiafya bila kuwepo na magonjwa yaliyozoeleka kama yalivyo maeneo mengine yalivyo na malaria, homa za matumbo (typhoid) na mengine mengi.
• Ni sehemu kuu na muhimu ya vyanzo vya maji vinavyounda Mto Pangani kupitia Bonde la Mto Kikuletwa yaliko makutano ya mito na mifereji yote ya Meru.
• Ni Meru tu inayomiliki mlima wa pili kwa urefu Afrika ambapo hifadhi ya aina yake ina aina ya Kima wasiopatikana mahali pengine hapa nchini. Hifadhi hii kwa historia ilikuwa shamba la mifugo ya wakoloni na sehemu yake ilikuwa shamba la mapapai.
• Zaidi ya yote ni Meru iliyo na ardhi na maeneo tofauti unakoweza kulima zaidi ya aina kumi tofauti za mazao na kustawi bila tatizo.
Wenyewe wanasema, “Meru ni Nchi ya Ahadi kwa Wameru”.
1. SERENGETI NDOGO
Hapa ndiyo 'Serengeti Ndogo' ambako utakuta wanyama wengi.
Mtalii yeyote
anaweza kushtuka wakati atakapoambiwa na Mhifadhi kwamba sasa anapelekwa katika
Serengeti ndogo ndani ya Hifadhi ya Arusha. Eneo hilo siyo kubwa sana, lakini
ni mbuga ya wazi inayofanana na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Hapa
wanyama mbalimbali wa mbuga za wazi wanaonekana kwa urahisi na kwa makundi,
wakiwemo ngiri (warthog), pundamilia
(zebra), kuro (waterbucks), twiga (giraffe)
na mbogo (buffalo). Nilimchekesha mhifadhi wakati nilipoona kundi
na pundamilia wakiwa wamemzunguka mwenzao aliyelala chini ambaye nilidhani
amekufa. “Ndugu, naona hawa wana msiba, mwenzao mmoja anaonekana kama amekufa!”
Nikamwambia kwa mshtuko wakati nikipiga picha. Mhifadhi huyo akaniambia kwamba
kwamba huyo hajafa, bali anajigalagaza. Kweli, dakika mbili baadaye nikamuona
anagalagala.
“Kwa
kawaida pundamilia huwa hawakusanyiki kwa msiba hata mwenzao anapokufa. Wanyama
pekee ambao wanaweza kukusanyika kwa msiba ni tembo na nyani. Hata hivyo, nyani
ndio wanaoongoza kwa kuomboleza msiba ambapo mwenzao akifa watambeba na
kutembea naye kila waendako mpaka atakapooza na kunuka ndipo watamwacha. Lakini
wanaomboleza kweli kama binadamu!” mhifadhi huyo akanieleza. Naam, tembea uone.
2.
‘OL DOINYO OROK’ NDIO MLIMA MERU
Oldoinyo Orok au Mlima Mweusi, ndio Mlima Meru
Jina la mlima huo
limetokana na watu wa kabila la Wameru wanaoishi maeneo hayo yapata miaka 300
sasa. Kwa mujibu wa wanahistoria, eneo hili lilikuwa linakaliwa na Wamasai,
ambao nao walikuwa wahamiaji. Wamasai wenyewe waliuita mlima huo Ol Doinyo Orok (yaani Mlima Mweusi)
kama ilivyo kwa ile Milima ya Namanga ambayo mpaka sasa inaendelea kujulikana
kwa jina hilo la Ol Doinyo Orok kule upande wa Kenya yenye urefu wa meta 2,548
(8,360 ft).
Mlima huo wa asili ya
volcano ulioko takriban kilometa 70 magharibi mwa Mlima Kilimanjaro ni wa pili
kwa urefu Tanzania ukiwa na urefu wa meta 4,565 (futi 14,977) kutoka usawa wa
bahari na ni mlima wa tisa au wa kumi kwa urefu barani Afrika kati ya vilele 75
huku ukiwa wa 72 duniani. Mjerumani Fritz Jäger ndiye anayetajwa kuwa binadamu
wa kwanza kufika kileleni mwaka 1904.
Kwa
mujibu wa wanajiografia Siebert L, Simkin T (2002-), maeneo mengine ya volcano
nchini Tanzania ni Mlima Kilimanjaro, Ol Doinyo Lengai ambao ni mlima pekee
Afrika wenye volcano hai, Burko, Embulbul, Elan Nairobi, Esimingor, Gelai,
Igwisi Hills, Izumbwe-Mpoli, Ketumbaine, Kieyo, Lemagrut, Loolmalasin,
Ngorongoro, Ngozi, Oldeani, Ololmoti, Olossirwa, Mlima Rungwe na Bonde la
Usangu.
Inaelezwa kwamba,
Mlima Meru ndio ulikuwa mrefu zaidi kuliko Kilimanjaro, lakini ulipungua urefu
kutokana na mlipuko wa volcano uliotokea takriban miaka 8,000 iliyopita
ukaubomoa kama ilivyotokea kwa Mlima wa St. Helens huko Washington, Marekani
mwaka 1980. Mlipuko huo uliufanya Mlima Meru uwe na umbo la nusu-duara, hivyo kufanya uwe sehemu ya
maajabu kwa yeyote anayetembelea Hifadhi ya Arusha na kuupanda.
Mlipuko wa mwisho wa
volcano ulitokea katika Mlima Meru mwaka 1910. Ukifika utastaajabu kuona
vichuguu na kasoko ndogo ndogo zinazothibitisha kwamba kulikuwa na milipuko ya
mara kwa mara ya volcano, ambayo ilisababisha sehemu kubwa ya udongo utiririke
hadi katika maeneo ya West Kilimanjaro na Arusha Chini.
Mlima Meru ndio kiini
cha Hifadhi ya Taifa ya Arusha, miteremko yake imetandwa na misitu minene ya
savanna iliyohifadhi aina mbalimbali ya wanyama, zikiwemo aina 400 za ndege.
Unaweza
kuupanda Mlima Meru kwa siku nne kwa kutumia mojawapo ya njia mbili zilizopo kutokea
Lango la Momella (meta 1,500 kutoka usawa wa bahari). Unaweza kutumia njia ya
Kaskazini ama Kusini na kufika kwenye mabanda ya Miriakamba kabla ya kuendelea
na safari katika vituo vya Saddle hadi kileleni.
3. KASOKO YA NGURDOTO
Ngurdoto
ni matokeo ya Wazungu kushindwa kutamka neno la Kimasai la Engur toto, yaani bonde
katika mlima au kasoko (crater). Eneo
hili la kasoko lipo katika Mlima Ngurdoto ambapo lina ukubwa wa kilometa za
mraba 8 na mzingo wa kilometa 10.67 huku kina chake kikiwa cha meta 333.
Ukiwa
katika eneo lenye mwinuko wa juu kabisa kwenye ukingo wa kasoko panapoitwa
Leitong unakuwa kwenye kilele cha meta 1,824 kutoka usawa wa bahari. Tofauti na
Kasoko ya Ngorongoro (Ngorongoro Crater),
kwenye Kasoko ya Ngurdoto huwezi kushuka chini kutazama wanyama na mandhari,
ingawa wapo wengi kama nyati wanaoonekana kwa makundi. Zamani walikuwepo faru
wengi, lakini majambazi wakawapopoa na kuchukua vipusa.
Katika
eneo hilo la Leitong unaweza kuiona hata barafu ya Mlima Kilimanjaro, maziwa ya
Momella pamoja na kuona shughuli nyingi za kijamii, hasa kilimo, katika vijiji
mbalimbali. Unyevu na ukungu mwingi kwenye eneo hili umesaidia kustawi kwa
mimea aina mbalimbali kama feni, kuvumwani, okidi na kuvu (kuvumwani yenye
vinyweleo).
Ni mahali
pazuri kutembelea na panawavutia watalii wengi.
4. MSITU WA ASILI WA NGURDOTO
Mnyama jamii ya Mbega ndiyo alama ya Hifadhi hii na wanapatikana kwa wingi
Kama
unataka hewa nzuri, ya asili na iliyotulia, basi tembelea Hifadhi ya Taifa ya
Arusha, na ufike kwenye msitu huu wa asili wa Ngurdoto. Mandhari tulivu ya eneo
hili yenye upepo mwanana usio na uchafuzi wowote wa mazingira utakusahaulisha
msongo wa mawazo na mambo mengi ya kidunia. Kuna miti mingi aina kwa aina,
ambayo imebandikwa vibao vyenye majina.
Msitu huu
ndio pekee ambapo wanyama aina ya Mbega weupe wanapatikana kwa wingi katika
Tanzania. Umekwishawahi kusikia usemi kwamba 'Mbega aliponzwa na uzuri wake?'. Basi
uzuri wa wanyama hao ni wa pekee. Manyoya yao yanapendeza mno, halafu zile
nyusi zao za asili hakika hata mwanamke ajipambe na atinde nyusi kiasi gani
katu hawezi kuwafikia. Habari ndiyo hiyo!
Ni hifadhi chache sana pamoja na misitu ambamo Mbega wanapatikana. Lakini
ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Arusha ndimo wanamopatikana kwa wingi mno. Ni
wanyama adimu na adhimu.
Mbega weupe-na-weusi ni ngedere wa kale wanaotokea katika jenasi ya Colobus, wakiwa wanapatikana zaidi
barani Afrika. Wana uhusiano wa karibu na mbega wekundu wanaotokea kwenye
jenasi ya Piliocolobus. Mbega ni
jamii ya wanyama wasiokula nyama (herbivorous),
chakula chao kikuu ni majani, matunda, maua na kadhalika. Yaani hawa jamaa ni
ma-vegetarian hasa. Wanaishi katika
makundi ya wanyama 9, kutegemeana na dume mmoja katika kundi la majike wengi na
watoto.
Mbega ni muhimu kwa usambazaji wa mbegu kutokana na tabia yao ya ulaji na
mfumo wa mmeng'enyo. Kuna aina tano ya spishi za kima hawa, huku kukiwa na
spishi ndogo nane ambazo ni: Black
colobus (C. satanas), Gabon black colobus (C. s. anthracinus), Bioko black colobus (C. s. satanas), Angola colobus (C.
angolensis), Sclater’s Angola
colobus (C. a. angolensis), Powell-Cotton’s Angola colobus (C. a. cottoni), Adolf Friedrichs’s Angola colobus au Ruwenzori black-and-white colobus (C. a. ruwenzorii), Cordier’s
Angola colobus (C. a. cordieri),
Prigogine's Angola colobus (C. a. prigoginei), Peters's Angola colobus au Tanzanian black-and-white colobus (C. a. palliatus), King colobus (C. polykomos), Ursine
colobus (C. vellerosus) na Mantled guereza au Abyssinian black-and-white colobus (C. guereza).
Wanatokea katika Himaya ya Animalia,
Faila ya Chordata, Daraja ya Mammalia, Oda ya Primates, Familia ya Cercopithecidae
na Familia ndogo ya Colobinae.
5. MAZIWA YA MOMELLA
Ndege aina ya Flamingo wanavyoonekana katika Ziwa Momella Kubwa.
Haya ni
maajabu mengine ambayo mtalii yeyote hapaswi kuyakosa. Maziwa haya ambayo maji
yake yana magadi (alkaline) kwa miaka
mingi yamekuwa mahali pa ndege kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni kuja
kustarehe. Flamingo na Heroe kwa aina zake, wakiwemo wale wa Ziwa Natron (Ziwa
Magadi), hujazana hapo wakipumzika kabla ya kurejea kwenye makazi yao ya asili.
Inaelezwa
kwamba, ndege hao hutaga mayai huko Ziwa Natron na kuyaangua, ambapo baada ya
muda huelekea kwenye maziwa haya ya Momella kujipumzisha kutokana na mazingira
yake tulivu. Ukifika nyakati za asubuhi na jioni utashangaa kuona, hasa kwenye
Ziwa Momella Kubwa, Flamingo wakiwa wametanda kama maua pembezoni mwa maziwa
hayo na wengine wakiwa katikati na kutengeneza kundi linaloonekana kama kisiwa.
Maajabu ya
maziwa haya ni kwamba, hakuna mito rasmi inayopeleka maji wala kutoa maji,
isipokuwa inaelezwa kuwa yanapokea maji hayo kupitia kwenye mito inayopita
chini ya ardhi. Maziwa hayo hayana kina kirefu, lakini pamoja na maji kuwa na
chumvichumvi, yamekuwa matumizi muhimu kwa wanyama.
Ziwa
Momella ndogo ndilo pekee ambapo wanyama aina ya Viboko hupatikana kutokana na
maji yake kuwa na alkaline kidogo, lakini pia ndilo linalotumiwa kwa utalii wa
makasia.
6. ZIWA LA IONGILI
Hili ndilo
ziwa pekee miongoni mwa maziwa madogo matano yanayopatikana hifadhini ambalo
maji yake hayana chumvi ambapo samaki aina ya perege (tilapia) wanapatikana. Ukiwa kwenye eneo hili utawaona wanyama kama
viboko, mbogo na kuro huku mimea aina ya matete (mace) na mafunjo (papyrus)
ikiwa inaonekana kama visiwa na huhama kulingana na mwelekeo wa upepo.
Hapa
wanapatikana ndege wengi kama red knobbed coot, Africana, fish eagle na
Africana jacana.
7. MAPOROMOKO YA MAJI
Haya ni maporomoko ya Tululusia
Hata Twiga nao wanapozi unapotaka kupiga picha ili watokelezee.
Ndani ya
Hifadhi ya Arusha kuna maporomoko ya maji ya aina mbili – yale ya Tululusia na
Maio, ambapo yanavutia sana kwa uzuri wake. Maporomoko ya Tululusia yana urefu
wa meta 28 ambapo yapo karibu na Lango la Momella, wakati yale ya Maio yapo
pembezoni mwa barabara iendayo mlimani.
Kabla ya
kuyafikia maporomoko ya Tululusia kwa kupitia Njia ya Kaskazini ukiwa
unapandisha Mlima Meru, lazima kwanza utakuwa umepata bahati ya kupita kwenye
uwanda wa wazi ambapo utapata fursa ya kupiga picha kwa karibu na wanyama kama
twiga na mbogo.
Kimsingi,
eneo hili ndilo pekee ambalo unaweza kutembea na kuwakaribia wanyama hao, hasa
mbogo, ukapiga nao picha kana kwamba unawachunga ng’ombe pori. Ni uzoefu
unaokuja mara moja katika maisha na kwa hakika hutaweza kujutia safari yako.
8. TAO LA MTI
Hili ndilo Tao la Mti
Ukiwa na
gari kama unakwenda Mlima Meru lazima upite kandokando ya mlima Tululusia ambao
una mandhari nzuri ya kuvutia. Lakini baada ya kuupita mlima huo utakutana na
kivutio kingine cha ajabu ambacho ni Tao la Mti wa Mkuyu (Fig Tree Arch).
Inaelezwa
kwamba, mti huo uliota baada ya ndege wala matunda kudondosha punje za mkuyu
kwenye mti mwingine wa asili, ambapo baadaye mkuyu ukaota kama tao, ambalo ni
kubwa kiasi kwamba gari lenye ukubwa wa tembo linaweza kupita bila shida.
Hiki ni
kivutio kingine ambacho hakika unapaswa kukitembelea na kujionea maajabu haya
na hasa kwa Mti wa Mkuyu ambao una maajabu yake. Kama ulikuwa hujui, Mkuyu ndiye malkia wa miti yote ulimwenguni
na kuna watu wanaouita mti mtakatifu. Wacha nikuelezee kidogo kuhusu mti huo:
Nakumbuka
enzi za utotoni tulizowea kuambiwa mti wa mbuyu ni wa mashetani na tusithubutu
hata siku moja kukaa karibu pindi mvua inaponyesha kwa sababu radi linaweza
kuupiga na kuugawanya katikati. Hata hivyo, bado tuliendelea kukwea na kuchuma
matunda yake nyakati za kiangazi.
Tuliambiwa
kwamba wachawi hupendelea kuweka maskani yao kwenye miti hiyo ya mibuyu, ambayo
ni miongoni mwa miti mikubwa na inayoweza kukua na kumea katika maeneo yenye
ukame, kama Dodoma na Singida kwa hapa Tanzania.
Lakini
ukiachilia mbali mbuyu, pia wazee wetu walikuwa wakitukataza tusipendelee
kucheza kwenye miti ya mikuyu, ambayo inatajwa kwamba ndiyo ‘malkia wa miti
yote’. Sababu kubwa waliyotuambia ni kwamba miti hiyo ni ya miungu na ndiyo
maana inapendelea kuota sehemu zilizotulia kwenye mapito ya maji huku ikiwa
inaongoza kwa kuwa miti pekee yenye mizizi mingi.
“Ninyi
hamuoni, hata nyakati za kiangazi mti unaonekana umependeza, tofauti na ule
mbuyu. Ule mbuyu ni mti wa mashetani, lakini huu ni mti wa miungu. Msije
mkathubutu hata siku moja kuukata ama kuuchezea, miungu ikikasirika mtapata
shida,” nakumbuka mzee mmoja alipata kutuambia wakati tukiwa wadogo.
Kweli
hatukuwa tukiikata miti hiyo, lakini daima tulipendelea kucheza chini ya vivuli
vyake na kukwea kuchuma matunda yake mazuri kuyatazama, matamu kuyala, lakini
yakiwa yamejaa wadudu wengi ambao unalazimika kuwaondoa kabla ya kuyala.
Huo ndio
mkuyu, mti ambao ni wa ajabu ambao si wengi wanaoufahamu kutokana na kutoota
kila mahali kama ilivyo miti mingine. Tena basi si mti wa kupandwa, bali
hujiotea wenyewe, hasa katika maeneo ya kitropiki, ingawa baadhi ya jamii yake
inaweza kuota kwenye maeneo ya joto.
Tunaambiwa
kwamba mti mashuhuri wa mkuyu (Ficus
carica) asili yake ni Asia na Mashariki ya Kati lakini umefanikiwa kumea
hata katika maeneo mengine, ukiwa unazaa matunda matamu sana, ambayo kama
unaweza kuhudumiwa kama yalivyo matunda mengine, huwezi kukuta wadudu ndani ya
matunda yake yenye majimaji mengi.
Wataalamu
wa mambo ya kale wanasema kwamba mti huu wa mkuyu unaweza kuwa mmoja kati ya
mimea iliyowahi kutunzwa na binadamu (katika sehemu nyingine mikuyu inatunzwa,
hasa kwa watu wenye maeneo makubwa, kwa sababu miti hii huchukua maeneo makubwa
sana kutokana na mfumo wao wa mizizi kuwa yenye kutambaa). Mkuyu unatajwa ndani
ya Biblia, wakati Adam na Eva wanapotumia majani yake kujistiri baada ya kuona
wako uchi ndani ya Bustani ya Eden.
Ukristo
siyo dini pekee ambayo imeupa mkuyu nafasi kubwa kama unavyotajwa pia katika
Injili. Jamii nyingine ya mkuyu au mtini wa Kiasia, Ficus religiosa, unachukuliwa kama mti mtakatifu na Wahindu,
Wajaini, na Mabuddha. Inasemekana Buddha Mkuu, Siddhartha Gautama, alipata
ufunuo wakati alipokuwa ameketi chini ya mti mtakatifu wa mkuyu, ambao pia
unajulikana kama bo au pipal. Waislamu pia wanaichukulia miti
mingine ya jamii ya mkuyu kama mitakatifu.
Kwa
hakika, kati ya miti yote duniani, mikuyu (Ficus)
ndiyo miti pekee ambayo ukuaji wake umetandwa na utata utata na hata
uchavushaji wake ni wa ajabu. Jaribu kufikiria mti ukiwa umejaa mizizi
inayofanana na nyoka, ikiwa imejiviringisha na kuchomoza kwenye shina ama
matawi ya mti mkubwa na kutanda kila sehemu na hata kuinyonga miti mingine ya
jirani yake.
Miti hii
ambayo iko katika jenasi ya Ficus,
katika familia ya Mulberry (Moraceae), ndiyo yenye jamii kubwa zaidi
ikiwa na aina ya miti 1,000. Miti inayoifuatia kwa kuwa na jamii nyingi ni ile
ya jamii ya mikungugu yenye miiba, maarufu kama Acacia (ambayo ina jamii 800), Mikaratusi ama Eucalyptus (500), na
Cassia (500).
Wazee wetu
walikuwa na akili sana – japo hawakuwa na elimu ya darasani – lakini walijua
namna ya kutunza mazingira. Walitukataza tusiiharibu miti hiyo kwani mara
nyingi huota katika vyanzo vya maji au sehemu iliyopitisha maji kama mto, au
sehemu iliyokuwa na uoto mzuri na ardhi yenye rutuba.
Kama
iliota sehemu za nyikani, basi tuliamini kwamba ikiwa utachimba kisima mahali
hapo maji hayakuwa mbali sana, na ndivyo ilivyokuwa, hasa kwa sisi ambao
tulikuwa tukiishi katika maeneo kame kama yale ya mikoa ya kati.
Faida yake
ni kubwa, kwamba pamoja na kuwa vyanzo vya maji na vivutio vya mawingu ya mvua,
lakini matunda yake ni chakula kizuri sana kwa ndege, wanyama wa porini na hata
binadamu.
Tunaambiwa
kwamba matunda ya mkuyu yana viiniisho kama wanga, hamirojo, sukari, mafuta na
protini kibao, hivyo ni mazuri sana kuliwa. Kwa sisi tuliowahi kuyala wakati wa
utotoni tunaujua utamu wake, lakini linaweza kuwa jambo geni kwa wale ambao
hata mti wenyewe hawaujui.
Tunda la
mkuyu linachukuliwa kama tunda, lakini kwa hakika hilo ndilo kama ua la mkuyu.
Linaweza kutajwa kama ni tunda bandia ama tunda linalojipogolesha, ambapo ua na
mbegu hukua pamoja na kufanya tunda.
Pengine
uwezo huu wa kutoa maua ambayo ni matunda, tofauti na miti mingine, ndiyo
yaliyowafanya hata wazee wetu waone kwamba huu ulikuwa ni mti wa miungu,
tofauti na mbuyu ambao maua yake yanaonekana mpaka matunda yanapokomaa.
Maelezo
mengine watakupatia wahifadhi na watalaamu wa mimea mara utakapofika kwenye
hifadhi hii, mimi nimekupatia uzoefu wangu tu wa uhifadhi wa asili.
9. KASOKO YA MERU
Kila eneo
lina raha yake kulitazama. Ukiwa unapanda Mlima Meru lazima utapita kwenye
uwanda wa wazi ambao unajulikana zaidi kama Mandhari ya Kitoto, ambapo unaweza
kuona mazingira ya Momella, pori la wazi na Mlima Kilimanjaro.
Lakini
ukipita eneo hilo utakuta kuna njia nyembamba ambayo inaishia kwenye Kasoko ya
Meru. Hapo utaona kitu kilichosimama kama ukucha wa ndege wa kuparura ndani ya
kasoko, ambako kwa uhakika ni majivu ya volcano yenye umbo kama pia.
Kasoko ya
Meru ni eneo tambarare na lenye kuvutia ambapo unaweza kuona vizuri mofolojia
yam lima hasa siku zisizo na mawingu.
10. TAMBIKO LA WAMERU
Njia
nyembamba inayoanzia kasoko ya Meru huelekea kwenye mandhari ya Njeku kupitia
mandhari nzuri ya Ash-cone na kasoko, ambapo kuna jukwaa kwenye mwinuko wa juu
unaotazamana na maporomoko ya maji katika korongo la mto wa Ngarenanyuki.
Wakati wa
ukame Wameru hulitumia eneo hilo kutambikia mungu wao chini ya mti ujulikanao
kama African pencial cidar (Juniper)
ambao upo karibu na tambarare ya kasoko. Kadiri miaka inavyozidi kusonga mbele,
matambiko haya yanaelekea kupungua hifadhini, lakini eneo hili bado limekuwa
kivutio kikubwa kwa watalii.
WANYAMA NA NDEGE
Huyu ni Hondohondo wa jamii ya Decken Toko Tockus deckeni
Pamoja na
kuwa na eneo dogo la hifadhi, lakini hifadhi hii ina utajiri mkubwa wa wanyama
kama twiga, pundamilia, mbogo, ngiri, mbega, kima, tembo, chui. Hakuna simba
kwenye hifadhi hiyo.
Utajiri mkubwa ulioko humo ni ndege aina kwa aina, ambapo
miongoni mwao ni Korongo, Njiwa, Kunguru,
Tai, Kipanga, Yangeyange, Kibisi, Shakwe, Dudumizi, Firigogo, Kasuku, Shorobo,
Kekeo, Mdiria, Hondohondo, Zuwakulu, Kigong'ota, Shore, Kuzi au Kwenzi kwa
jamii zake na kadhalika.
0656-331974