Mheshimiwa
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib
Bilal jana Desemba 10, 2014, amewahutubia wawakilishi wa Afrika katika
Mkutano wa Mazingira Duniani (Cop20) unaofanyika jijini Lima, nchini
Peru.
Mheshimiwa
Makamu wa Rais anahudhuria mkutano huu akimuwakilisha Rais Jakaya
Kikwete ambaye ni Kiongozi wa Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka Afrika
kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi. Mkutano huo wa jana ulikuwa na dhima ya
Afrika baada ya mwaka 2015: Makubaliano Mapya kuhusu Mabadiliko ya
Tabia Nchi.
Awali
Mheshimiwa Dkt. Bilal aliwaambia wawakilishi wa Afrika katika mkutano
uliojumuisha Mawaziri wa Afrika wanaoshughulikia masuala ya Mazingira
katika nchi zao kuwa, Afrika licha ya unyonge wake bado inalo jukumu la
kusimama kidete katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi na ili
kufanikiwa katika jambo hilo ni muhimu kwa Bara hili kuwa na sauti ya
pamoja.
Mheshimiwa
Makamu wa Rais aliendelea kusema kuwa, Bara la Afrika lina kila sababu
ya kuwa na mipango yake ambayo itatumika kushirikisha nchi za nje ya
Afrika ili kwa pamoja Dunia iweze kuwa na kauli inayofanana yenye
kulenga kukabiliana na majanga yanayotokana na mabadiliko ya Tabia Nchi
licha ya kuwepo tofauti za kimaendeleo kati ya Afrika na nchi za mabara
mengine.
Awali
akizungumza kabla ya Mheshimiwa Makamu wa Rais, Waziri wa Mazingira wa
Sudan ambaye ni Mwenyekiti wa kundi hili la Afrika Dkt. Hassan
Albdelgadir Hillal alisema, kundi la Afrika linapongeza uongozi wa
Tanzania kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete kwa namna unavyosimamia agenda
hizi za mabadiliko ya Tabia Nchi na kusimamia upatikanaji wa sauti moja
kutoka kwa nchi za Afrika.
Dkt.
Abdelgadir aliendelea kusema kuwa, Afrika inatakiwa kutumia mkutano huu
wa Lima kwa umakini ili kuhakikisha mipango inayofikiwa inapata
kutambulika na kuonekana mwakani wakati mkutano kama huu utakapofanyika
jijini Paris.
Kwa
upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira Dkt.
Binilith Mahenge ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mawaziri wa Mazingira kwa
nchi za Afrika yeye alibainisha kuwa, viongozi wa nchi za Afrika
wamekuwa mstari wa mbele kabisa kuhakikisha kuwa Afrika inasikika na
kwamba anatarajia ushirikiano katika ngazi ya Mawaziri kuendelea hata
pale atakapokuwa anakabidhi nafasi hiyo kwa Waziri wa Mazingira wa
Misri.
Katika
mkutano mwingine ambao pia ulikuwa mwendelezo wa Siku ya Afrika katika
COP20, Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Bilal alisisitiza kuwa Afrika
inatakiwa kuhakikisha vijana na akina mama wanakuwa mstari wa mbele
katika kukabiliana na hali hii ya mabadiliko ya tabia nchi.
“Makundi haya ni muhimu sana kwa kuwa ndiyo yanayohusika moja kwa moja
na shughuli za kila siku. Hatutaweza kufanikiwa kama tutayaacha makundi
haya nyuma,” alisema Mheshimiwa Makamu wa Rais katika Mkutano huo ambao
pia ulihutubiwa na Dkt. Fatima Denton, Mkurugenzi wa Harakati Maalum
kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Kamishenbi ya Uchumi kwqa Afrika
(UNECA).
Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal,
akisalimiana na Mwenyekiti wa Kamati ya Wataalam ya Afrika katika
masuala ya Majadiliano ya Mabadiliko ya Tabianchi kutoka nchini Sudan,
Nagmeldin El-Hassan, wakati alipokuwa akiwasili katika ukumbi wa
mikutano kwa ajili ya kuzungumza na wawakilishi wa Afrika katika mkutano
wa Mazingira Duniani (Cop20) unaoendelea jijini Lima, nchini Peru.
Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal,
akizungumza na Wawakilishi wa Afrika katika mkutano wa Mazingira wa
Dunia (Cop20) (hawapo pichani) alipokuwa akiwahutubia leo Desemba 11,
2014. Katikati ni Waziri wa Mazingira wa Sudan, (kushoto) ni Mwenyekiti
wa Kamati ya Wataalam ya Afrika katika masuala ya Majadiliano ya
Mabadiliko ya Tabianchi kutoka nchini Sudan, Nagmeldin El-Hassan.
Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal,
akiagana na baadhi ya wawakilishi wa Afrika katika mkutano wa Mazingira
wa Dunia (Cop20) baada ya kuwahutubia leo Desemba 11, 2014, katika
Mkutano wa Mazingira Duniani na majadiliano kuhusu Mabadiliko ya
Tabianchi, unaoendelea jijini Lima, nchini Peru.
Ujumbe
wa Tanzania katika mkutano wa Mazingira Duniani, wakimsikiliza Makamu
wa Rais Dkt. Mohammed Gharib Bilal, wakati akiwahutubia leo, Desemba 11,
2014, mkutano wa Mazingira Duniani (Cop20) unaoendelea jijini Lima,
nchini Peru.
Sehemu
ya Wawakilishi wa nchi za Afrika katika mkutano wa Mazingira Duniani,
wakimsikiliza Makamu wa Rais Dkt. Mohammed Gharib Bilal, wakati
akiwahutubia leo, Desemba 11, 2014, mkutano wa Mazingira Duniani (Cop20)
unaoendelea jijini Lima, nchini Peru.