Jicho la ForumCC: Ukweli kuhusu mafuriko yaliyotokea Buguruni kwa Mnyamani

  ForumCC ni Jukwaa la asasi zisizo za kiraia Tanzania zinazojuhusisha na Mabadiliko ya Tabianchi. ForumCC inafanya shughuli zake kua... thumbnail 1 summary


 
ForumCC ni Jukwaa la asasi zisizo za kiraia Tanzania zinazojuhusisha na Mabadiliko ya Tabianchi. ForumCC inafanya shughuli zake kuanzia ngazi ya chini kwa wananchi hadi kitaifa. Kwa lugha rahisi ambayo mwananchi wa kawaida kabisa anaweza kuelewa.

Mabadiliko ya Tabianchi ni mabadiliko ya muda mrefu na ya kudumu ya hali ya hewa, hasa jotoridi na mvua, vile vile mabadiliko haya yanagusa kasi na mwelekeo wa pepo na mambo mengine yanayohusiana na hali ya hewa. Moja ya athari za wazi wazi ni kuongezeka kwa joto, pia kuongezeka sana au kupungua sana kwa mvua. Athari hizi tayari sisi kama sehemu ya dunia tumezishuhudia katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Sasa kwa hili la Buguruni kwa Mnyamani nalo lina sura yake ambayo haikuwekwa wazi na watoa taarifa kwa umma hasa kilichosababisha.

Mnamo tarehe 22 march 2015 saa tisa mchana Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitoa tahadhari ya kuwepo kwa mvua kubwa katika ukanda wa pwani itakayonyesha kwa siku tatu mfulilizo. Unakanda huu unajumuisha mikoa ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara, Pwani, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba. Mamlaka hiyo ilitoa tahadhari ya ongezeko la mvua kwa zaidi ya milimita 50 ndani ya saa 24.

Masaa machache baada ya tahadhari kutolewa mvua ilianza kunyesha katika maeneo  mengi, ikiwemo Dar es Salaam, mvua ambayo ilipelekea maafa makubwa kwa wakazi zaidi ya 5,170 katika eneo la Buguruni kwa Mnyamani. Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Bw Abdallah Mng’ae anasema takribani nyumba 517 zilihadhiriwa na mvua kubwa iliyonyesha na kila nyumba ina wastani wa wakazi 10.

Nini Sababu za Mafuriko Katika eneo la Buguruni Kwa Mnyamani?.
Sababu iliyotolewa kwa vyombo vya habari kama kisababishi cha mafuriko hayo ni kuziba kwa mfereji wa kupitishia maji katika eneo hilo, ambapo chanzo chake ni wizi wa chujio la kuchuja takataka. Inasemekana chujio hilo liliibiwa na kuuzwa kama chuma chakavu, biashara ambayo imesababisha kuhujumiwa kwa miundombinu mbalimbali ya maendeleo katika maeneo mengi hapa nchini.

ForumCC inapinga na kukemea kwa nguvu zote wizi wa namna hiyo ambao unarudisha nyuma maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla. Pia tunatoa wito kwa jamii kulinda miundombinu na kutoa taarifa kwa vyombo vinavyohusika pale wanapobaini watu wanaohujumu miundombinu mbalimbali. Wizi ni kitendo kisichokubalika, na jamii isikae kimya pale inapobaini wezi hawa, ni vizuri taarifa zikatolewa kwa vyombo husika ili hatua za kisheria ziweze kuchukua mkondo wake.
Jicho la Tatu Kuhusu Mafuriko

Kwa kutumia jicho la tatu utagundua kuwa kuibiwa kwa chujio kwenye mfereji unaopitisha maji katika eneo la Buguruni kwa Mnyamani si kisababishi pekee cha mafuriko hayo. Kuna visababishi vingine vyenye uzito sana ambavyo havikuzungumziwa kabisa. Kuna maswali kadha wa kadha ya kujiuliza kuhusu janga hili lililowakumba wakazi wa Buguruni kwa Mnyamani.

·         Je ongezeko la mvua kwa milimita 50 si sababu mojawapo ya mafuriko kutokea?.
·         Je ukubwa wa mfereji wa kupitishia maji katika eneo la tukio unaweza kuhimili ongezeko kubwa la maji?.

·         Je hilo chujio lingeweza kuhimili uchafu mwingi ambao ungetokana na ongezeko la mvua?.
·         Je kuna watu ambao huondoa uchafu kwenye machujio haya wakati mvua ikinyesha ili kudhibiti lisizibe?.

Majibu ya maswali haya moja kwa moja yanaonyesha uwezekano mkubwa sana wa mafuriko kutokea hata kama chujio lililoibiwa lingekuwepo. ForumCC inaona hivyo kwa sababu ni ukweli usiopingika kuwa uwezo wa miundombinu yetu kuhimili mafuriko bado upo chini sana. Na kutokana na uwepo wa mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la mvua kupita kiasi kwa muda mfupi ni moja ya vitu ambavyo vitakuwa vinajirudia hivyo basi tusipojenga miundombinu imara na yenye kuzingatia uwepo wa mabadiliko ya tabianchi tutazidi kuathirika zaidi.

Kulingana na mazingira ya mfereji wa kupitishia maji katika eneo la Buguruni kwa Mnyamani na mpango wa makazi ni dhahiri kuwa hata chujio lingekuwepo mafuriko yangetokea tu.
Ni wakati sasa wa wananchi kuhimiza serikali yao ijenge miundombinu bora ambayo inazingatia uwepo wa majanga tofauti tofauti katika jamii yetu. Wakati huo huo wananchi nao wanawajibu wa kuboresha makazi yao kulingana na mabadiliko ya tabianchi.

Ni wito wetu kwa watoa taarifa za majanga mbalimbali na masuala mengine kueleza kwa kina kuhusu tukio ili jamii ijue ukweli na pale ambapo inaweza kushiriki kuboresha, kuepuka au kuhimili wajue wajibu wao. Vilevile maelezo ya kina na ya jicho la tatu yatakuwa ni elimu tosha kwa jamii na wadau wengine.

Tuboreshe miundombinu na Kuilinda