VIJANA WAASWA KUPANDA MITI KUPUNGUZA HALI JOTO NCHINI

 Watanzania wameaswa kuwa na utaratibu wa   kupanda miti katika mazingira yao kujiepusha na madhara ya mabadiliko ya tabianchi yanayoikumb... thumbnail 1 summary
 Watanzania wameaswa kuwa na utaratibu wa  kupanda miti katika mazingira yao kujiepusha na madhara ya mabadiliko ya tabianchi yanayoikumba dunia kwa sasa.

Wito huo umetolewa na afisa mazingira wa wilaya ya Bagamoyo Shedrack Maximilian wakati wa zoezi la upandaji miti katika shule ya sekondari Bagamoyo mkoani  Pwani , kulikofanywa na asasi zisizo za kiserikali na wanafunzi kutoka shule mbalimbali za jijini Dar es salaam na wenyeji shule ya sekondari Bagamoyo jumamosi wiki hii.


Afisa huyo aliyekuwa akimwakilisha mkuu wa wilaya ya Bagamoyo  amesema watanzania wanakila sababu ya kupanda miti na kuhifadhi mazingira ili kuendelea kuibakisha nchi katika kijani kibichi.  Amesema sababu za kiuchumi , umaskini na kibiashara zisiwe chanzo cha uharibifu wa mazingira na kukata miti hovyo.

“kama sisi hapa Bagamoyo tupo karibu na jiji la Dar es salaam lenye mahitaji ya matumizi ya kuni na mkaa.  tusipopanda miti  kutabaki  jangwa, hatutaki kuruhusu hili kutokea maana  hatujui dunia inaisha lini . kuna vizazi vinazaliwa  hamna mahali pengine watapata miti na kuwa na mazingira bora”amesema Shadrack

Naye mwakilishi wa shirika la Norwegian  church Agoustina Mosha  amesema shirika lao ni mfadhili wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya vijana, wajasiliamali na miradi ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

“shirika letu limeanza toka mwaka 2011 hapa nchini, tunafanya shughuli zetu na asasi za kiraia na kidini kama Bakwata, Tec ,Katholiki , Buddha na Hindu. Tumefikia wilaya zaidi ya 60 nchi nzima, tunapenda kufanya kazi na vijana kwa sababu ndio wapo wengi nchini kwa mujibu ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, ukiwakusanya vijana na kuwapa mafunzo ni rahisi kuchukua hatua kutokana na kuwa kundi kubwa”amesema mama Mosha.



Akitoa shukrani kwa ugeni huo mkuu wa shule ya Bagamoyo  Halfani Milongo amesema wamepokea zawadi ya miti kwa mikono miwili na watajitahidi  kuilinda na kuitunza ili isiweze kukauka na kufa.

“tuna vijana  wapenda mazingira na wapo tayari kuitunza kwa nguvu zao zote, sote tunajua umuhimu wa miti katika kupunguza hali joto , tutashirikiana na vijana wetu na tuna ahidi  baada ya miaka kadhaa karibuni  kuja kujionea miti mliyotuletea hapa shuleni ikiwa imestawi vyema” anamaliza Mwalimu huyo.

Naye kiongozi wa Tanzania Youth Network  Agnes Mgongo ambao walikuwa washiriki katika  uzinduzi huo wa upandaji miti, amesema  wameshiriki zoezi hilo kwa kutambua faida ya miti kwa ustawi wa jamii na utunzaji mazingira.  Pia ni jukwaa ambalo kama vijana wamepata kukutana na vijana wengine kutoka sehemu  mbalimbali  na kubadilishana mawazo na uzoefu juu ya maswala ya vijana.


“vijana wengi  wa kitanzania tupo  hatutumii fursa  zinazopatikana  ndani na nje ya nchi , tofauti na vijana wenzetu wa Afrika Mashariki.  Ni wakati wetu sasa kubadilika na kwenda na wakati kwa kuchangamkia fursa zinazojitokeza mahali popote dunia, tumepewa akili na maarifa  tusisubiri serikali itufanyie kilakitu  vijana tunaweza” anamaliza kusema Agnes Mgongo.

Uzinduzi huo ulikuwa sehemu ya kutoa elimu ya upandaji miti kwa shule ya sekondari ya Bagamoyo na vijana  kwa ujumla kulikofanywa na vijana kutoka asasi mbalimbali za mazingira kutoka jijini Dar es salaam pamoja na chuo cha mazingira cha Institute of Environment Climate and Development Sustainability  kilichopo Bunju  jijini Dar es salaam.