Ushirikiano wa wanasayansi na wanahabari utakuza uelewa wa mabadiliko ya tabianchi

Dotto Kahindi RoadToParis2015 with tabianchiblog&CFIMedias21 Wanahabari ni miongoni mwa watu wenye nguvu kubwa ya ushawishi amba... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi
RoadToParis2015 with tabianchiblog&CFIMedias21
Wanahabari ni miongoni mwa watu wenye nguvu kubwa ya ushawishi ambao wamekuwa wakitumika kama daraja kati ya vikundi tofauti hasa katika kupasha habari.

Mawasiliano kati ya viongozi, wanasayansi, watafiti na wananchi katika jamii mbalimbali yamekuwa yakiwezeshwa kwa kiasi kikubwa na vyombo vya habari na waandishi wa habari wenyewe.

Waandishi wameonekana kuwa muhimu sana katika maendeleo na ustawi wa mataifa mbalimbali kutokana na kuyachambua mambo magumu, kuyalainisha na kuyafikisha kwa wananchi ili waweze kuyaelewa kwa urahisi.

Hata hivyo waandishi wengi wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo kukosa uelewa na ufahamu wa kutosha wa kuandika habari za sayansi na mazingira, jambo ambalo linafanya habari nyingi za aina hiyo kukosa ladha ya kuwavutia wasomaji.

Kwa kipindi kirefu kumekuwa na utengano baina ya waandishi na wanasayansi, jambo ambalo limepelekea jamii kukosa kupata habari za kina zenye majawabu ya matatizo yanayohusiana na sayansi.

Hii ni kutokana na wanasayansi wengi kutoa ripoti zao katika lugha ngumu yenye kuwatatiza waandishi wa habari ambao ndio wawasilishaji wa mwisho wa taarifa hizo kwa wananchi.

Mkutano wa wanasayansi mjini Paris, Ufaransa, Picha na Christophe Maitre INRA
Wanasayansi wamefikia mahala wamegundua kuwa kazi zao haziwezi kuwa na maana kama hazijalainishwa na kuwa katika hali nzuri ya kumezwa na walaji wa mwisho na ndio maana wameona umuhimu wa kushirikiana na waandishi wa habari ili kazi zao ziwafikie wananchi

“Tungependa kuimarisha ushirikiano wetu wanasayansi na waandishi wa habari, kuanzia katika hatua za mwanzo mpaka mwisho katika shughuli zetu za utafiti, hii itawezesha taarifa zetu za kisayansi kuwafikia wananchi kwa urahisi na katika lugha nyepesi” anasema Madaka Tumbo, mtafiti kutoka kwenye Taasisi ya Kutathimini Rasilimali Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (IRA)

Katika kuhakikisha kuwa waandishi wa habari hasa wa kizazi kipya wanakuwa na uwezo wa kuripoti habari za mazingira, Shirika la Habari la Ufaransa (CFI) kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni  UNESCO wametoa mafunzo kwa waandishi wa habari kutoka Tanzania, Kenya na Madagascar.

Mafunzo hayo yanalenga kujengea uwezo wa waandishi hao kuripoti habari za sayansi na mazingira kwa kushiriki kwenye mikutano ya wanasayansi ili kujifunza kwa vitendo namna ya kuandaa na kuandika habari za namna hiyo

Ikiwa kama nchi mwenyeji wa mkutano wa mazingira, Urasansa kupitia shirika la habari za Ufaransa (CFI), french media cooperation agency) kwa ufadhili wa Wizara ya Mambo ya Nje ya serikali ya Ufaransa wameanzisha mradi wa mafunzo ya uandishi wa habari na mabadiliko ya tabianchi (Media21 Journalism and Climate Change)

Lengo la mradi huo ni kuwajengea uelewa wa mambo mbalimbali wakati wa mkutano wa mazingira, kuwezesha uelewa kwa wananchi juu ya mabadiliko ya tabianchi na kuwawezesha waandishi wa habari juu ya namna ya kuwasilisha kazi zao katika lugha inayoeleweka kwa wasomaji wao.

Akiwa katika chakula cha pamoja na waandishi wa habari kutoka kutoka Tanzania, Kenya na Madagascar Mkurugenzi Mkuu wa CFI, Etienne Fiatte anabainisha kuwa “Hii ni sehemu ya mpango wetu wa kushirikiana na vyombo vya habari Barani Afrika katika kuchangia upashaji habari za mabadiliko ya tabianchi tukielekea kwenye mkutano wa wanachama wa mabadiliko ya tabianchi COP21 desemba mwaka huu, tunamatumaini makubwa kwa waandishi hawa kwamba watajifunza na kutoa matokeo chanya katika mradi huu”

Waandishi wa habari kutoka nchi hizo tatu awali walikutana mjini Nairobi nchini Kenya kupata mafunzo ya namna ya kuandika habari za sayansi na mabadiliko ya tabianchi kwa lugha tamu na ya kuvutia kwa wasomaji kabla ya kushiriki kwenye mkutano wa wanasayansi unaofanyika mjini Paris Ufaransa.

“Mafunzo haya yamenipa uwezo wa kuandika habari za mabadiliko ya tabianchi katika lugha nyepesi, naweza kuzichanganua taarifa ngumu za kisayansi katika makundi madogo madogo yanayoweza kueleweka moja kwa moja kwa wasomaji wa habari zangu” anasema Sophia Mbuguah mwandishi wa habari wa kujitegemea kutoka Kenya na kuongeza kuwa: “Hapo awali niliandika habari zangu kwa ujumla sana na ilikuwa ngumu kwa msomaji kuguswa na habari hiyo, lakini sasa naweza kuhusianisha habari yangu na mambo mtambuka kama uchumi, kilimo, afya na kutoa uchambuzi wa kina unaomfanya msomaji aelewe kwa urahisi”