Serikali
imesimamisha shughuli za uchimbaji wa Makaa ya Mawe ya Kampuni ya Off
Route Technology iliyopo Kyela ikiwemo kukamata vifaa vya uchimbaji na
kuhakikisha kuwa vinakuwa chini ya uangalizi wa Mkoa wa Mbeya hadi
hapo uchunguzi dhidi ya uhalali wa kampuni hiyo kuchimba makaa
utakapokamilika.
Hatua
hiyo inafuatia ziara ya Waziri wa Nishati na Madini, Prof Sospeter
Muhongo kutembelea mgodini hapo na kubaini kuwa, kampuni hiyo inachimba
makaa bila kuwa na leseni halali ya uchimbaji madini.
Aidha,
Prof. Muhongo ameitaka kampuni hiyo kulipa kodi zote za Serikali
ikiwemo inazodaiwa na Halmashuri tangu ianze kufanya shughuli za
kuchimba.
Aidha,
ili kujua undani wa suala hilo, Prof. Muhongo ameitisha kikao kifanyike
kati ya mgodi huo , Wizara ya Nishati na Madini, Wakala wa Ukaguzi wa
Madini Tanzania ( TMAA), Ofisi ya Madini Kanda ya Kusini Magharibi,
Katibu Tawala wa Wilaya ya Kyela, tarehe 18 Januari, 2016 chini ya
uenyekiti wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini.
"Hawa
watu wamechimba makaa, wameuza bila kuwa na Leseni na tunawadai kodi
zetu. Uongozi hakikisheni katika kikao hicho mnakuja na madai yenu,TMAA
pia mje na madai yenu", ameongeza Prof. Muhongo.
Prof.
Muhongo pia amezitaka pande zote kuwasilisha nyaraka muhimu kuhusu
suala hilo, ili iamuliwe kwa kufuata sheria na taratibu stahili,
"hakuna mtu atakayeonewa, kila upande uje na nyaraka zote na sisi
wizarani huko ndani kwetu tutaulizana wenyewe kuhusu jambo hili halafu
tutalitolea taarifa" ,amesema. Prof. Muhongo.
Akifafanua
kuhusu suala hilo , Afisa Mfawidhi wa TMAA ,Mhandisi Jumanne Mohamed
amesema kuwa, awali Wakala huo ilifanya ukaguzi na kubaini kuwa kampuni
hiyo hailipi kodi na kuwa yapo malimbikizo ya madai ambayo yalipaswa
kulipwa na kuongeza kuwa baada ya mawasiliano juu ya suala hilo,
kampuni iliahidi kulipa kwa awamu jambo ambalo halijafanywa hadi sasa.
Kampuni ya Off Route Technology, ipo katika Kijiji cha Ngana Wilaya ya Kyela mkoa wa Mbeya.