BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira
(NEMC), limeanza kung’ata kwa kutumia kanuni ili kudhibiti uchafuzi wa
mazingira kwa kelele na mitetemo.
Kwa sasa mtu akitaka kufanya sherehe mtaani, kupiga muziki
kwa kelele, kuendesha ngoma za kukesha za nusu uchi (vigodoro) au ‘bai
koko’ au kufanya ibada kwa kelele mitaani, atapaswa kulipa Sh milioni
10.
Pia, baa na kumbi za starehe za usiku zitakazopiga kelele, zitapaswa kulipa kiasi hicho.
Aidha, NEMC imesema pia kuwa wale watakaohusika na kelele
za migodini za kutumia baruti, kupasua miamba zilizo zaidi ya matakwa ya
sheria ya mazingira ya kelele na mitetemo, watapaswa kulipa Sh milioni
tano ili kupata kibali.
NEMC imetaka watu kuheshimu kanuni za viwango vya kelele na
mitetemo katika maeneo mbalimbali nchini. Imeonya kuwa watakaokiuka,
hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Kanuni hizo zimeanza kutumika mwaka
jana (2015).
Mkurugenzi Mtendaji wa NEMC, Bonaventure Baya alisema hayo
Dar es Salaam jana. Alisisitiza kuwa uchafuzi wa mazingira,
unaosababishwa na kelele na mitetemo, umekuwa ukifanyika bila kujali
sheria za nchi na sasa watashughulikia suala hilo ipasavyo.
Alisema hivi sasa kanuni za kudhibiti suala hilo,
zimekamilika na zimeanza kutumika kikamilifu. Mtu yeyote atakayekwenda
kinyume cha kanuni na sheria, atachukuliwa hatua kali. Baya alitoa
ufafanuzi kuwa yapo maeneo yenye kelele zaidi ya viwango vinavyoruhusiwa
kisheria, ikiwamo maeneo ya migodini.
Alieleza kwamba kanuni zimeweka vigezo na tozo maalumu la
kuanzia Sh milioni tano hadi Sh milioni 10, kulingana na eneo na aina ya
kelele na mtetemo. Alisema mambo mengine ambayo kanuni zimeweka ni
faini kwa kila kanuni itakayovunjwa na kusisitiza kuwa hatua hizo
zitachukuliwa ipasavyo.
Kulingana na hatua hiyo ya NEMC, sasa mtu mwenye kutaka
kufanya sherehe mtaani, itakayohuisha kelele zitakazosumbua jamii pamoja
na majirani zake, ikiwamo muziki maarufu wa ‘kigodoro’, ibada za
makanisani zinazozidi matakwa ya kisheria ya uanzishwaji wa makanisa
hayo katika jamii, atapaswa kulipa Sh milioni 10 ndipo aruhusiwe
kuendelea na shughuli yake.
Kwa mujibu wa NEMC, ruhusa hiyo inayo lipiwa, pia ina muda
na viwango vyake, ambapo kila muda husika unapoisha, kelele zinapaswa
kupunguzwa ama kuzimwa. Hii inahusisha pia baa na kumbi za starehe za
usiku.
Baya aliitaka jamii kuepuka uchafuzi huo wa mazingira wa
kelele na mitetemo, ambao watu wengi wamekuwa wakidhani si tatizo.
Alitaka watu kuheshimu matakwa ya sheria na kanuni kwa nyakati za mchana
na usiku.
“Tumekuwa tukipokea malalamiko kutoka kwa watu wengi,
wakilalamikia usumbufu wa kelele na mitetemo kutoka kwa watu
wanaoendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii katika jamii,”
alifafanua Baya.
Alitoa angalizo kwa wanaotumia vyombo vya muziki na sauti
katika maeneo ya makazi, ambavyo vimeleta madhara kwa afya za watu.
Alisema matumizi ya vipaza sauti na vyombo vya sauti kubwa, wanapaswa
kuwa na kibali maalumu.
Alieleza kuwa kanuni za kelele na mitetemo, zimeweka vigezo
na viwango vya sauti kwa ajili ya kudhibiti uchafuzi wa mazingira
katika maeneo ya hospitali, makazi, migodini, kumbi za kijamii, kumbi za
usiku za starehe, matangazo, baa na maeneo mengine.
Baya alisema baraza limepata changamoto kadhaa, ikiwamo
uelewa mdogo wa jamii kuhusu kiwango cha sauti kinachotakiwa na
kisichoruhusiwa na baadhi ya watu kwa makusudi huvunja sheria.
Kuhusu faini, alisema sheria ya mazingira imeweka wazi
faini kwa wanaokiuka na kuchafua mazingira kwa kelele na mitetemo. Faini
hiyo haiingiliani na tozo la Sh milioni tano hadi Sh milioni 10
lililoelezwa, ambapo mtu anapaswa kulipa si chini ya Sh milioni 50 na si
zaidi ya Sh milioni 50 ama kifungo jela.
Kaimu Mkurugenzi wa Usimamizi wa Sheria za Mazingira wa
NEMC, Ruth Lugwisha alisema tatizo la kelele na mitetemo, limekuwapo kwa
muda mrefu. Alisema tangu kupitishwa kwa kanuni, tayari watu kadhaa
wamewajibishwa.
Alisema miongoni mwa waliowajibishwa ni makanisa, kumbi za
starehe na baa. Hata hivyo, hakuwa tayari kuwataja wahusika wala maeneo.
Alisema uwajibishwaji huo ulihusisha faini, kufungiwa na onyo