Serikali yatoa miche 27000 ya matunda mkoani Simiyu

Kufuatia utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa kupanda miti kutunza Mazingira na Kuhifadhi Vyanzo vya Maji, Serikali kupitia Ofisi ya M... thumbnail 1 summary
Kufuatia utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa kupanda miti kutunza Mazingira na Kuhifadhi Vyanzo vya Maji, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Raisi Muungano na Mazingira, imetekeleza ahadi yake ya kugawa miche ya miti ya matunda Mkoani Simiyu katika Majimbo ya ya Uchaguzi ya Busega, Bariadi, Itilima, Kisesa, Meatu, Maswa Mashariki na Maswa Magharibi.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Raisi Mhe. Luhaga Mpina, amechangia miti ya matunda ya maembe na machungwa ipatayo Elfu Kumi (10,000) huku, Halmashauri na Wabunge wa Mkoa huo ,wamechangia idadi ya miche inayozidi Elfu Kumi na Tatu (13,000).

Kwa kuanzia idadi ya miche ya miti ya matunda ipatayo Elfu Kumi na Tatu Mia Sita Sitini na Sita,(13,666) imeshapelekwa Mkoani simiyu ikiwa ni miti ya maembe Elfu Kumi na Tatu na Mia Tano Sitini na Sita (13,566) na Michungwa Mia Moja (100).

Awali, Mhe. Mpina akitoa ahadi hiyo alisema, Mkoa wa Simiyu hauna miti ya matunda ya kutosha hivyo Mkakati wa upandaji miti ya matunda utasaidia chakula kwa familia, fedha kwa kuuza matunda na malighafi kwa viwanda nchini na kusema kuwa miti ni Mali na miti ni uchumi.Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais inamshukuru Mhe. Daudi Njalu Silanga (Mb). wa Itilima, kwa kujitolea usafiri wa kusafirisha miche hiyo kutoka Chuo cha Kilimo cha Sokoine kilichopo Mkoani Morogoro.

Idadi ya miche elfu ishirini na saba (27,000) inatarajiwa kugawanywa katika majimbo hayo, ikiwa ni pamoja na michango ya wabunge wa majimbo hayo.Kupitia Mkakati huo wa Kitaifa wa kupanda miti na kuhifadhi vyanzo vya Maji, Serikali pia imewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika kutunza mazingira na hususan wananchi wa Simiyu kuitunza miti hiyo ya muda mfupi, ili kuiepusha nchi na hali ya jangwa na ukame.

IMETOLEWA NA KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
OFISI YA MAKAMU WA RAIS.