Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira),
January Makamba ameliagiza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa
Mazingira (NEMC) kutumia Sheria ya Mazingira kupiga marufuku matumizi ya
majiko banifu ya kienyeji na ukataji mkubwa wa miti ya asili kwa ajili
ya biashara ya tumbaku.
January amesema katazo hilo litawahusu wakulima na vyama vya msingi vyote vinavyojihusisha na biashara ya tumbaku.
Ametoa agizo hilo akiwa ziarani wilayani Urambo na kubaini changamoto
kubwa ya uvamizi wa misitu na ukataji wa miti ya asili kwa ajili ya
kuni za kukaushia tumbaku.
Ameiagiza NEMC kutumia Sheria ya Mazingira Namba 20 ya Mwaka 2004
Kifungu Namba 196 (1) (a na b) kupiga marufuku ya matumizi ya majiko
banifu ya kienyeji pia ukataji mkubwa wa miti ya asili kwa ajili ya
biashara ya tumbaku.
Kuhusu hifadhi ya mazingira, amewataka wakazi wa Ufulaga kuacha tabia
ya kukata miti ya asili na kusisitiza kuwa uharibifu wa mazingira
unabadilisha tabia za watu.
“Wana Ufulaga, binadamu wakiharibu mazingira kwa kiasi kikubwa
wanaanza wizi na udokozi na wanyama wataanza kuwinda watu kwa kukosa
malisho,” alieleza.
Akiwa Wilaya ya Kaliua, alikutana na changamoto kubwa ya uharibifu wa
mazingira na uvamizi wa misitu unaofanywa na wananchi. Katika Kijiji
cha Ufugala, alifanya mkutano wa hadhara kijijini hapo na kubaini kuwa
kitongoji hicho hakikufuata taratibu za kisheria katika kuanzishwa kwake
na kimeanzishwa ndani ya Hifadhi.
Akitoa maelezo ya awali, Mkuu wa Wilaya ya Kaliua, Abel Busalama
alisema kitongoji hicho kiko ndani ya Hifadhi ya Msitu wa Kijiji ambapo
jumla ya vijiji 11 viliamua kutenga eneo hilo kwa ajili ya hifadhi.
Alisema wakazi hao wamekwisha amriwa kuondoka katika hifadhi hiyo na utekelezaji wake unaendelea.
Akijibu hoja zilizowasilishwa na wakazi wa eneo, January alisema
wajibu wa serikali ni kuhakikisha kuwa sheria, tararibu na kanuni
zinafuatwa bila kukiukwa.
Source: Habari Leo