HOTUBA YA WAZIRI KIVULI NA MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI WIZARA YA FEDHA NA UCHUMI NDUGU KABWE ZUBERI ZITTO KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013

Mbunge wa Kigoma kaskazini(CHADEMA)na Waziri Kivuli-Wizara ya Fedha,Zitto Zuberi Kabwe   1.0 UTANGULIZI Mheshimiwa Spika, ... thumbnail 1 summary
Mbunge wa Kigoma kaskazini(CHADEMA)na Waziri Kivuli-Wizara ya Fedha,Zitto Zuberi Kabwe
 


1.0 UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Bunge kanuni ya 99(7), toleo la mwaka 2007 na kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni,napenda kuwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Mafungu ya Wizara ya Fedha – Fungu 50 Wizara ya Fedha, Fungu 21 Hazina, Fungu 22 Deni la Taifa na Fungu 23 Ofisi ya Mhasibu Mkuu wa Serikali. Vile vile Fungu 10 Tume ya Pamoja ya Fedha na Fungu 13 Kitengo cha Udhibiti wa Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi.

Mheshimiwa Spika, mafungu yote yaliyo chini ya Wizara ya Fedha yanaomba kuidhinishiwa na Bunge lako tukufu jumla ya shilingi Bilioni 4,208 (trilioni 4.2) ili yaweze kutekeleza majukumu yake. Mafungu haya maombi yake ya Fedha ni sawa na asilimia 28 ya Bajeti nzima ya Serikali ya mwaka wa Fedha 2012/13.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha ndiyo msimamizi mkuu wa Uchumi wa nchi ikitekeleza majukumu mbalimbali ikiwemo, kusimamia ukusanyaji wa mapato ya ndani na ya nje, kusimamia matumizi ya Serikali, kusimamia utendaji wa Taasisi na Mashirika ya Umma, kusimamia manunuzi ya Serikali na Taasisi na Mashirika ya Umma, kusimamia Deni la Taifa na dhamana za Serikali, kutafuta suluhisho na kusimamia mfumo wa kodi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na kupambana na Fedha haramu.

 Sambamba na hayo ni kusimamia na kutekeleza mpango wa kupunguza umasikini nchini kupitia utekelezaji wa MKUKUTA II.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha na mafungu yote yaliyo chini yake ndio moyo wa Serikali na hivyo ni lazima kuitazama Wizara hii kwa jicho kali na kutilia mashaka kila jambo ambalo inalifanya ili kuhakikisha kuwa moyo huu hausimami maana madhara yake ni kwa taifa zima na watu wake. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kupitia Waziri Kivuli wa Fedha inatekeleza wajibu huu kwa Uzalendo, Uadilifu na kwa misingi ya Uwajibikaji. Tumetekeleza wajibu huu na tunaendelea kuutekeleza bila kujali maneno na kuweka maslahi ya Taifa letu mbele ya kila kitu kingine. Maslahi ya Taifa ni zaidi ya vyama vya siasa, mahala tunapotoka au dini tunazoamini. Maslahi ya Taifa ni kwa ajili ya Watazania na hasa Watanzania milioni 30 (The Bottom 30M) ambao bado wanaishi katika ufukara mkubwa sana wakikosa huduma muhimu za jamii na wanaoishi vijijini ambapo hakuna umeme, barabara hazipitiki na wanahangaika kutwa kutafuta maji safi na salama. Maslahi ya Taifa sio faida ya wachache wenye kuishi mijini au wanasiasa wanaotafuta ushawishi kwa umma bila kujali matakwa ya Umma. Watanzania wanyonge wa vijijini wanajua maslahi yao ni nini. Wanajua kina nani wanapigania maslahi ya Wanyonge.


2.0 MAPATO YA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya mwenendo wa Uchumi ya mwezi Julai (Monthly Economic Review, July 2012) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania, katika kipindi cha mwezi Juni Serikali iliweza kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 998.0. Hata hivyo matumizi halisi yalikuwa kiasi cha shilingi bilioni 1,911.8 hali iliyopelekea kuwepo kwa nakisi baada ya kuondoa msaada wa masharti wa masharti wa shilingi bilioni 400.2; nakisi hiyo ililipwa kwa vyanzo vya ndani na nje.

Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo ilionyesha kuwa mapato yote ukiondoa fedha zilizokusanywa na Serikali za mitaa kwa mwezi Juni, yalikuwa kiasi cha shilingi bilioni 887.5 ambacho ni zaidi ya asilimia 38.1 ya malengo yaliyokuwa yamewekwa kukusanywa mwezi huo. Aidha, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikusanya kiasi cha shilingi bilioni 753.3, kiasi ambacho ni zaidi ya asilimia 22.3 ya malengo ya makusanyo kilichokuwa kimewekwa na mamlaka hiyo. Makusanyo haya ni makubwa zaidi kukusanywa na TRA kwa mwezi mmoja tangu Mamlaka hiyo ianzishwe.

Mheshimiwa Spika, katika makusanyo hayo ya mwezi Juni Mamlaka ya Mapato Tanzania ilikuwa imejiwekea lengo la kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 242.4 kama kodi ya Mapato, lakini ilikusanya kiasi cha shilingi bilioni 366.0 kiasi ambacho ni zaidi kwa asilimia 60.8 ya malengo yaliyokuwa yamewekwa.


2.0 MAPATO YA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya mwenendo wa Uchumi ya mwezi Julai (Monthly Economic Review, July 2012) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania, katika kipindi cha mwezi Juni Serikali iliweza kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 998.0. Hata hivyo matumizi halisi yalikuwa kiasi cha shilingi bilioni 1,911.8 hali iliyopelekea kuwepo kwa nakisi baada ya kuondoa msaada wa masharti wa masharti wa shilingi bilioni 400.2; nakisi hiyo ililipwa kwa vyanzo vya ndani na nje.

Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo ilionyesha kuwa mapato yote ukiondoa fedha zilizokusanywa na Serikali za mitaa kwa mwezi Juni, yalikuwa kiasi cha shilingi bilioni 887.5 ambacho ni zaidi ya asilimia 38.1 ya malengo yaliyokuwa yamewekwa kukusanywa mwezi huo. Aidha, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikusanya kiasi cha shilingi bilioni 753.3, kiasi ambacho ni zaidi ya asilimia 22.3 ya malengo ya makusanyo kilichokuwa kimewekwa na mamlaka hiyo. Makusanyo haya ni makubwa zaidi kukusanywa na TRA kwa mwezi mmoja tangu Mamlaka hiyo ianzishwe.

Mheshimiwa Spika, katika makusanyo hayo ya mwezi Juni Mamlaka ya Mapato Tanzania ilikuwa imejiwekea lengo la kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 242.4 kama kodi ya Mapato, lakini ilikusanya kiasi cha shilingi bilioni 366.0 kiasi ambacho ni zaidi kwa asilimia 60.8 ya malengo yaliyokuwa yamewekwa kutokana na kuongezeka kwa bei ya mauzo ya dhahabu. Hata hivyo Manunuzi yetu kutoka nje yamefikia dola za Kimarekani 12,959 milioni.

Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo inaonyesha kuwa mauzo ya dhahabu Nje kwa mwaka 2011 yalikuwa kiasi cha dola 2,330.7 milioni sawa na aslimia 56.7% ya mauzo yote nje, wakati mauzo ya nje kutokana na bidhaa zilizozalishwa viwandani yalikuwa na jumla ya dola 922.0 milioni sawa na asilimia 22.4% ya mauzo yote ya nje. Aidha mauzo ya mazao mbalimbali kama Pamba, Katani, Korosho, Chai, Kahawa na mengineyo yalikuwa na thamani ya dola 761.1 milioni kwa kipindi hicho cha mwaka 2012.

Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo imeendelea kuonyesha kuwa tuliagiza bidhaa kutoka nje zenye thamani ya dola za Kimarekani milioni 12,958.7. Katika manunuzi hayo tuliyofanya mafuta peke yake yalikuwa na thamani ya dola za Kimarekani milioni 3,586.1 ambalo ni ongezeko la asilimia 60.08% ukilinganisha na kipindi kama hicho kwa mwaka 2011.

Mheshimiwa Spika, takwimu hizi zinaonyesha kwamba fedha zote za kigeni zilizotokana na mauzo ya dhahabu, bidhaa za viwandani na Korosho zilitumika kuagiza mafuta pekee yake! Hali hii ni mbaya sana kwa uchumi wa Taifa letu na juhudi zote za kuongeza mauzo nje zinaliwa na uagizaji wa Mafuta ambao umepanda sana katika siku za hivi karibuni.

6

Kambi Rasmi ya Upinzani inatambua kuwa kuanzia mwaka jana Serikali imekuwa ikitekeleza mpango wa Umeme wa dharura ambao umepelekea matumizi makubwa ya Mafuta. Hata hivyo ieleweke kuwa Mpango mzima wa Manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mitambo ya Umeme inaligharimu Taifa Fedha nyingi sana. Takwimu zinaonyesha kuwa Serikali inapaswa kutumia zaidi ya shilingi 42 bilioni kila Mwezi kuendesha mitambo ya dharura ya Umeme. Manunuzi yenyewe ya Mafuta yamejaa mazonge ya ufisadi uliokithiri. 


Licha ya kutaka Spika aunde timu ya kuchunguza ufisadi katika manunuzi ya Mafuta na licha ya Kamati ya Bunge kutaka Uchunguzi wa kibunge kufanyika katika manunuzi haya bado hakuna hatua inayochukuliwa. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Mamlaka ya Manunuzi ya Umma PPRA kufanya uchunguzi wa kina kuhusu manunuzi ya mafuta kuzalisha Umeme ambayo yanachoma bilioni 42 za Serikali kila Mwezi. PPRA hapaswi kufumbia macho manunuzi yanayotafuna shilingi 1.4 bilioni kila siku na yanayoongeza manunuzi ya nchi kutoka nje (imports) na hivyo kupoteza fedha za kigeni hovyo.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha ambayo ndio wizara mama ya PPRA kupitia Fungu 50, na ndio Wizara yenye kusimamia uchumi wa nchi kwa ujumla ituletee Bungeni Taarifa ya Uchunguzi utakaofanywa na PPRA kuhusu manunuzi shilingi 1.4 bilioni kila siku ya mafuta kuendesha mitambo ya kuzalisha Umeme.

2.3 Deni la Taifa.
Mheshimiwa Spika, Fungu 22 linaombewa jumla ya shilingi bilioni 2,735 ili kuweza kulipa madeni ikiwemo deni la nje la shilingi bilioni 373 na trilioni 1.5 kama deni la ndani. Kwa mujibu wa taarifa ya mwenendo wa uchumi ya mwezi Julai 2012, deni la nje la Taifa (external debt) mpaka mwisho wa mwezi Juni 2012 lilikuwa limefikia kiasi cha dola za Kimarekani milioni 10,354.6 kiasi ambacho ni ongezeko la zaidi ya dola milioni 385.9 kwa kipindi kama hicho mwaka 2011. Aidha katika kipindi hicho deni la ndani lilikuwa kiasi cha shilingi bilioni 4,174.2. Kambi ya Upinzani Bungeni ina taarifa kwamba takwimu hizi za Deni la Taifa hazihusishi dhamana ambazo Serikali imezitoa kwa Mashirika ya Umma na Kampuni binafsi. 

Dhamana lazima katika siku za usoni ziwe ni sehemu ya deni la Taifa maana tumeshuhudia sasa ambapo Kampuni nyingi binafsi zimeshindwa kulipa mikopo iliyodhaminiwa na Serikali. Mfano ni malipo ya deni lenye thamani ya shilingi bilioni 60 la kukodisha ndege ya Airbus kwa Shirika la ATCL kutoka kampuni ya Wallis Traders ya Lebanon na Deni lililochukuliwa na Kampuni ya Kiwira Coal and Power limited ambayo mbia wake alishindwa kuendesha mradi wa Makaa ya Mawe Kiwira licha ya kudhaminiwa na Serikali Mkopo kutoka kwenye taasisi za Fedha hapa nchini ambapo sasa Serikali imepanga kulipa shilingi bilioni 40 katika Bajeti ya mwaka huu.


Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani haina tatizo na uhimilivu wa Deni la Taifa (Debt sustainability) kwani tunajua kuwa mataifa makubwa yanakopa sana na yana uwiano mkubwa wa Deni kwa GDP kuliko sisi. Tatizo letu ni namna ambavyo fedha za mikopo zinatumika. Matumizi ya mikopo tunayochukua sio endelevu maana sehemu ya mikopo hiyo hutumika kwa matumizi ya kawaida badala ya matumizi ya uzalishaji au kuongeza uwezo wetu wa kuzalisha.

Kambi Rasmi ya Upinzani inaendeleza wito wake wa kutaka Fungu 22 la deni la Taifa lifanyiwe ukaguzi maalum (Special Audit) ili tuweze kujua mikopo hii tunayochukua kila wakati inatumika kufanyia nini? Miradi iliyotekelezwa kutokana na Madeni ambayo Waziri wa Fedha aliitangaza wakati wa kufunga mjadala wa Bajeti kuu ya Serikali ifanyiwe ukaguzi kutambua ukweli na kuona thamani ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaendelea kuhoji kama tulivyohoji mwaka 2011/2012 kuhusu matumizi mabaya ya fedha za umma. Katika fungu 21, kasma 229929, Serikali imetenga Shilingi bilioni 26.4 kwa ajili ya kulipa fidia kwa mikataba mbalimbali ambayo Serikali imeingia. Hii inaonyesha kuwa Serikali inatumia fedha nyingi sana kwa ajili ya mikataba iliyoingiwa na Mashirika ya Umma na kuliletea hasara Taifa.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na kutaka majibu kutoka kwa serikali, bado tunataka kuwe na usimamizi thabiti ili kulinda fedha za umma zinazotumika kwenye Mashirika ya Umma, ambapo kumekuwa na usimamizi mbovu sana na unaopelekea Taifa kupoteza fedha nyingi sana kutokana na ubadhirifu katika Mashirika ya Umma. Hii ni kweli kwa Mashirika ambayo Serikali inamiliki sehemu ya hisa.

2.5 MKOPO WA KUNUNUA RADA ILIYOGUBIKWA NA UFISADI

Mheshimiwa Spika, sehemu ya Malipo ya Deni la Taifa ni Mkopo ambao Serikali ilichukua ili kununua Rada kutoka kampuni ya BAE ya Uingereza. Suala hili la rada limejadiliwa sana nchini kwa upande mmoja tu wa ufisadi wa kupandisha bei ya Rada na hatimaye kurejeshwa kwa iliyoitwa chenji ya Rada. Hiyo ilikuwa ni nusu tu ya ukweli kuhusu suala la Rada kwani Serikali ilikopa kiasi cha dola za kimarekani 40 milioni kutoka Benki ya Barclays ya Uingereza kwa ajili ya kununulia Rada. Mkopo huo ulikuwa na Riba ya asilimia 4.9 juu ya kiwango cha riba zinazotolewa na Benki ya Dunia au IMF.

Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kujua kama mkopo huu umeshalipwa wote na jumla tulilipa kiasi gani cha fedha. Ukilinganisha fedha iliyorejeshwa kama chenji ya Rada na Fedha ambayo Tanzania iliilipa Benki ya Barclays (Principal amount na Interest), je chenji ya Rada ilikuwa na thamani yoyote kifedha? Mjadala wa ununuzi wa Rada hauwezi kuisha kwa kufurahia kurejeshewa chenji tu. Mjadala huu bado mbichi kabisa kwani tunataka ukweli na ukweli mtupu uelezwe kwa umma na kuona Taifa lilipata hasara kiasi gani kwa ufisadi huu wa kimataifa na hatua stahiki za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wote walioingiza hasara kwa Taifa letu.

2.4 Kitengo cha Udhibiti wa Fedha Haramu

Mheshimiwa Spika, taifa letu limekuwa na sheria nyingi ambazo ziliwahi kutungwa kwa ajili ya kukabiliana na tatizo la fedha haramu, rushwa na uhalifu uliopangwa hapa nchini mwetu tangu tupate uhuru na hii inathibitishwa na uwepo wa sheria zaidi ya 15 kuwahi kutungwa tangu uhuru (tazama kiambatanisho A). Vile vile Bunge liliimarisha Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu mwaka 2011. Hata hivyo bado nchi yetu imegubikwa na fedha chafu na hasa wizi katika Mabenki hapa nchini. Wakati sheria ya Fedha haramu inayataka Mabenki kutunza kumbukumbu sahihi za wateja, kumekuwa na matukio (yaliyoripotiwa na yasiyoripotiwa) ya Wafanyakazi wa mabenki hapa nchini kushirikiana na baadhi ya wananchi kuiba fedha za wateja na hasa wateja ambao wamefariki dunia na ndugu na jamaa zao kutojua taarifa za kibenki za marehemu hawa. 


Serikali inapaswa kufahamu kuwa wizi kwenye mabenki ni moja ya sifa mbaya sana ya mfumo wetu wa fedha na hivyo kusababisha Benki kuweka riba kubwa sana ili kufidia ‘risk’ kama hizi za watu ‘kupiga’ amana za wateja kwenye mabenki. Kambi Rasmi ya upinzani inaitaka Wizara ya Fedha kupitia Kitengo cha Udhibiti wa Fedha haramu kudhibiti wizi kwenye Benki za hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kupata maelezo ya kina juu ya matatizo ya mtaji “Capital under pressure” yanayoikabili benki ya NBC na hatua zilizochukuliwa na Serikali kama mmoja wa wanahisa dhidi ya mwanahisa mwenye dhamana ya kuisimamia Benki hiyo (ABSA) kwa kushindwa kuisimamia kwa umakini na hivyo kuiingiza katika matatizo hayo ya mtaji. Mheshimiwa Spika, hivi sasa wanahisa (ambapo Serikali ni mmoja wao) wanapaswa kuongeza mtaji katika benki ya NBC ili kuinusuru, Benki ambayo ni moja ya Benki kubwa kabisa hapa nchini ambayo kama ingekuwa na usimamizi mzuri ingepaswa kujiendesha yenyewe na kutoa gawio kwa wanahisa.

Mheshimiwa Spika, taarifa iliyotolewa na Benki Kuu ya Uswissi na kuchapishwa na magazeti mbalimbali ya hapa nchini mwezi June, 2012 inanonyesha kuwa viongozi wa Serikali pamoja na wafanyabiashara wakubwa wametorosha fedha zao katika mabenki ya Uswissi kiasi cha shilingi bilioni 315.5. Habari zaidi zinaeleza kwamba mabilioni haya yanatokana na ‘deals’ zilizofanywa na watendaji wa Serikali na wafanyabiashara kadhaa kwenye sekta za Nishati na Madini. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imepata taarifa kuwa mmoja wa Viongozi wa juu kabisa wa Tanzania na baadhi ya Mawaziri wa Serikali za awamu zilizopita ni miongoni mwa wamiliki wa Fedha hizi. Sehemu kubwa ya Fedha zililipwa na Kampuni za utafutaji wa Mafuta na Gesi katika Pwani ya Mkoa wa Mtwara zilizopewa mikataba kati ya mwaka 2004 na 2006. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa taarifa rasmi ya hatua gani imechukua mara baada ya taarifa ile kutoka Benki ya Taifa ya Uswissi ilipotolewa. Tunaitaka Serikali kuliambia Taifa hatua itakazochukua kurejesha fedha hizi na nyingine zozote ambazo zimefichwa ughaibuni. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni italazimika kuweka wazi taarifa na majina ya watu wenye umiliki wa fedha katika Benki za nchini Uswissi iwapo Serikali haitatoa taarifa rasmi kuhusu suala hili.

Mheshimiwa Spika, Aidha, kuna taarifa nyingine zinaonyesha jinsi ambavyo taifa linaibiwa kupitia kesi mbalimbali ambazo Serikali imeshitaki au kushitakiwa kwenye Mahakama za Kimataifa. Mfano mzuri ni Kesi ya IPTL na Standard Chartered Bank ya Hong Kong ambayo imechukua muda mrefu bila kuisha na kuliingizia taifa hasara kubwa sana. Tunapenda kufahamu ni kwa nini mpango wa kumaliza kesi hii nje ya Mahakama hautekelezwi na vile vile mpango wa kugeuza Mtambo wa kufua umeme wa IPTL kuwa wa Gesi kwa nini hautekelezwi?

Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kupata majibu kuhusu mambo yafuatayo;

Kwanza, fedha zilizoko kwenye Escrow Akaunti Benki Kuu za IPTL (Tegeta escrow) zimefikia kiasi gani mpaka sasa, na usalama wa fedha hizo ukoje? Ikumbukwe kwamba kuna uamuzi wa Bunge kwamba Fedha hizi zisitumike wala kutolewa mpaka maamuzi kuhusu mtambo wa IPTL kufikiwa na hasa uamuzi wa kugeuza mtambo huu kutumia Gesi Asilia.

Pili, Suala hili la kesi ya IPTL limechukua muda mrefu sana na sasa ni wakati muafaka likamalizwa nje ya mahakama kwa Waziri wa Fedha kukutana na pande zote za mgogoro huu ili liweze kufikia mwisho.

2.6 Kampuni ya Oxford University Press Tanzania Kufungiwa Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 03 Julai 2012 Benki ya Dunia ilitangaza kuifungia kampuni ya uchapishaji ya Oxford University Press Tanzania Ltd (OUPTL) kutokana na vitendo vya rushwa ambavyo kampuni hiyo ilikiri kuhusika kwake kwenye miradi mbalimbali ya elimu iliyokuwa inafadhiliwa na Benki hiyo katika ukanda wa Afrika Mashariki. Mheshimiwa Spika, kampuni hiyo ilikiri kuhusika katika kuwahonga maafisa mbalimbali wa Serikali katika mkataba wake wa kusambaza vitabu na kampuni hiyo ilikubali kuilipa Benki ya Dunia kiasi cha dola 500,000 kama sehemu ya makubaliano yake kutokana na kashfa hiyo.


Mheshimiwa Spika, mamlaka ya manunuzi ya umma ilitangaza kuifungia kampuni hiyo hapa nchini kwa kipindi cha miaka saba, wakati ambao tayari tulishawapa zabuni ya kusambaza vitabu vilivyotokana na chenji ya rushwa ya Rada ambazo ziliamuliwa kuwa zitaenda kununua vitabu. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuinyang’anya kampuni hii zabuni ya kuchapisha na kusambaza vitabu hivyo na badala yake kazi hiyo yapewe makampuni ya ndani ya nchi. Tabia ya Serikali kufanya kazi na Kampuni ambazo tayari zina dosari ama za kifisadi au kukiuka sheria na maagizo ya Serikali inatoa picha mbaya kwenye uchumi. Hali kadhalika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuwachukulia hatua maafisa wote wa Wizara waliohusika katika “rushwa ya Oxford”.
3.0 Mishahara hewa nchini

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu makadirio ya mapato na matumizi katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mwaka wa fedha 2012/2013, tulitaja kiasi cha shilingi bilioni 91 ambazo zililipwa kama mishahara kwa watumishi hewa kama ilivyoripotiwa na magazeti ya ‘The Daily News’ na ‘The Guardian’ ya Machi 23, 2011.


Mheshimiwa Spika, ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya tarehe 31 Machi, 2012 inaonesha kwamba kwa mwaka wa fedha 2010/2011 jumla ya shilingi 142,715,827.992 zililipwa kama mishahara kwa wastaafu, watumishi walioacha au kufukuzwa kazi na watumishi wengine ambao hawakustahili. Aidha, ripoti hiyo imeonesha kiasi cha shilingi 1,842,607,565.29 zilizolipwa kama mishahara hewa kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Fedha kwa kamati ya kudumu ya Bunge ya fedha na uchumi ya tarehe 7 Agosti, 2012 ni kwamba uhakiki wa watumishi uliofanyika mwezi Januari, 2012 kwenye Halimashauri 133 na kwenye taasisi na wakala za Serikali 154 ulibaini majina 9,949 ya watumishi wasiostahili kuwemo kwenye orodha ya mishahara. Idadi hii ya watumishi hewa ni sawasawa na takribani idadi ya watumishi walioajiriwa katika sekta nzima ya madini kwenye migodi ya dhahabu hapa nchini. Watumishi hewa wanaokaribia 10,000 ni wengi mno na inaonyesha dhahiri namna Serikali isivyo makini katika suala hili ambalo linasababisha upotevu mkubwa wa Fedha za Umma.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Fedha alikiri mbele ya Kamati ya Fedha na Uchumi kwamba mwezi Februari Serikali ililipa shilingi bilioni 5.1 kama mishahara hewa. Hii maana yake ni kwamba Serikali


2 Tazama Ripoti ya CAG toleo la Kiingereza uk.37.hutumia zaidi ya shilingi bilioni 70 kila mwaka kwa watumishi hewa wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, tunataka fedha hizi wanazolipwa watumishi hewa zitumike kuwalipa walimu na madaktari madai yao kwani ni nyingi na zinatosha sana. Siku zote sababu za Serikali kutotimiza matakwa ya wafanyakazi kwenye sekta ya Afya na Elimu ni kwamba Serikali haina Fedha. Lakini hapa tunashuhudia Shilingi bilioni 70 kila mwaka zikiteketea kulipa watumishi hewa ambao hawapo, hawafanyi kazi na hivyo kufaidisha mtandao wa kifisadi ambao kwa vyovyote vile unaanzia Wizara ya Fedha na Wizara ya Utumishi. Serikali inakosa vipi fedha za kulipa madai ya Walimu na inapata za kulipa watumishi hewa? Serikali inakosa vipi fedha za kulipa Madaktari na Manesi lakini inapata shilingi bilioni 70 kila mwaka kulipa watumishi hewa?


Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka mradi huu wa watumishi hewa wenye mauzo (turnover) ya shilingi 70 bilioni kwa mwaka uvunjwevunjwe ili kupata fedha za kulipa Walimu na Madaktari. Waziri wa Fedha asambaratishe mtandao huu mwovu ambao sasa umeota mizizi kwenye Taasisi za Serikali. Vile vile Waziri agawe kwa Wabunge taarifa ya uhakiki wa wafanyakazi wa Serikali na pia hatua ambazo Serikali imechukua dhidi ya vinara wa mtandao wa watumishi hewa Serikalini.

4.0 Benki Kuu ya Tanzania-(BOT)

Mheshimiwa Spika, taasisi hii ndiyo yenye dhamana ya kutayarisha na kusimamia sera za fedha na utendaji mzima wa taasisi za fedha kwa ujumla. Katika kutekeleza hilo Benki Kuu ndicho chombo kinachoweka miongozo kwa taasisi za fedha, taasisi za bima na taasisi za hifadhi za jamii ili kuhakikisha fedha za wanachama katika taasisi hizo zinalindwa.

Mheshimiwa Spika, taasisi za fedha zimegawanyika katika sehemu kuu mbili, ambazo ni tasnia ya benki (Banking industry) na tasnia ndogo ya fedha (Microfinance industry). Tasnia zote hizi zinahudumia wateja tofauti kwa kulingana na wanachojishughulisha nacho katika kuinua kipato cha familia inayomtegemea, mteja yuko kwenye sekta binafsi au sekta rasmi ya ajira.

Mheshimiwa Spika, Benki Kuu katika kutimiza wajibu wake inailazimu kutoa vigezo vitakavyozingatiwa katika utoaji wa mikopo ili kukabiliana na wakopaji ambao wanaweza kuwa na lengo la kuchukua fedha wakati hawana nia ya dhati ya kurejesha mikopo yao.

4.1 RIBA KATIKA TAASISI ZA FEDHA

Mheshimiwa Spika, tofauti kati ya viwango vya riba vinavyotozwa kwenye mikopo na vile vinavyotolewa kwenye amana kama faida vimeendelea kuwa juu, licha ya kuongezeka kwa ushindani katika sekta ya kibenki. Hii imechangiwa kwa kiasi kikubwa na kukosekana kwa taarifa sahihi za wakopaji (credit reference data bank) na kutokuwepo kwa taasisi ya utoaji wa taarifa sahihi za waombaji mikopo (Credit Rerefence Bureau) nchini. Aidha, gharama kubwa za kufanya biashara kutokana na miundombinu hafifu, nazo zimechangia kuongeza viwango vya riba vinavyotozwa kwenye mikopo. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaomba taarifa ya kuanzishwa kwa Credit Reference Bureaux kwa mujibu wa Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006.

4.2 Usimamizi Wa Tasnia Ndogo ya Fedha (Microfinance Industry-MFI)

Mheshimiwa Spika, tasnia hii ndiyo inayoshughulika moja kwa moja na kundi kubwa la Watanzania ambao hawako kwenye mfumo rasmi wa ajira kwa kuwapa mikopo midogo midogo kwa shughuli rasmi au zisizo rasmi, ili kuhakikisha kuwa kipato cha familia kinapanda na hivyo uchumi wa mwananchi mmoja mmoja unakua.

Mheshimiwa Spika, tasnia hii inalenga kuboresha maisha ya wananchi wa vijijini na maeneo mbalimbali ya mijini. Tasnia hii inalenga kuboresha maisha kwa wananchi mmoja mmoja au makundi (Saccoss) na benki jamii (vicoba) ambazo zimekuwa na wanachama wengi wanaoendelea kujiunga ili kujikwamua kiuchumi.


Mheshimiwa Spika, kukosekana kwa mdhibiti anayeelewa jinsi tasnia hii inavyofanya kazi zake na aina ya wateja inaowahudumia ni udhaifu mkubwa unaosababisha tasnia hii kushindwa kukua. Kukosekana kwa udhibiti wa sekta ndogo ya Fedha kunasababisha wananchi masikini kuumia sana. Mfano tumeshuhudia namna Kampuni za kukopesha zinavyowafanya Walimu vijijini kuwa masikini zaidi kwa kuweka riba kubwa sana. Hata hivyo Serikali imekaa kimya bila kusaidia wanyonge hawa kwa kuchukua hatua madhubuti za kudhibiti na kusimamia sekta hii. Mfano mzuri wa Serikali kushindwa kusaidia wanyonge ni pale ambapo wannachi wengi sana kujikuta wamepoteza fedha zao kupitia ‘schemes’ kama vile DECI ambapo wananchi walikusanya zaidi ya shilingi bilioni 16 ambazo mpaka sasa hata riba yake hatujui inakwenda wapi? 

Kungekuwa na Mamlaka ya kusimamia sekta ya fedha kwa ajili ya wanyonge tusingeshuhudia unyonyaji huu.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuunda Mamlaka ya Usimamizi wa sekta ndogo ya Fedha (Tanzania Microfinace Regulatory Authority) hapa nchini badala ya Benki Kuu ya Tanzania ambayo ndiyo msimamizi wa tasnia ya benki. Lengo ni kuhakikisha kuwa wananchi wa vijijini wanaopata mikopo kutoka kwenye taasisi za Benki wanalindwa na dola. Mamlaka italinda Haki za wanyonge dhidi ya ‘loan sharks’ na Wajibu wa wanyonge wenye kuchukua mikopo.

Mheshimiwa Spika, kuundwa kwa chombo chenye mamlaka ya kusimamia taasisi ndogo ya fedha ni lazima kutokana na ukweli kwamba kuna utofauti wa muundo baina ya mabenki na taasisi ndogondogo za fedha; inakuwa ni vigumu kudhibiti riba na utoaji wa vigezo vya kifedha katika kuhudumia wananchi na kutoa mikopo kwa wateja wa tasnia hizo mbili zilizo tofauti kimuundo.


Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa chombo chenye mamlaka pia itasaidia kuwa na Credit Reference Bureau itakalokuwa na taarifa za wakopaji kutoka taasisi ndogondogo za fedha tofauti na itakayosimamia wadaiwa wa mabenki na taarifa hizi zitasaidia udhibiti wa wateja wa taasisi hizi kuchukua zaidi ya mkopo mmoja kwenye taasisi tofauti tofauti ambapo hali hii husababishwa na ucheleweshaji wa mikopo inayotolewa na taasisi hizi pamoja na uhafifu wa mikopo katika kumsaidia mlengwa.

4.3 Mifuko ya Hifadhi za Jamii

Mheshimiwa Spika, Mifuko ya Hifadhi za Jamii ni mojawapo ya sekta ambayo ina uwezo mkubwa wa kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana wetu, kama uwekezaji unaofanywa kwa kutumia mifuko hiyo utasimamiwa vizuri.

Meshimiwa Spika, inaonesha kwamba mifuko hii imekuwa ikikusanya michango ya wanachama na kulipa wastaafu wanachama wa Mifuko hii vizuri. Kutokana na maelekezo ya sheria mpya iliyoleta mjadala baina ya wafanyakazi na serikali juu ya mabadiliko ya sheria na utoaji wa mafao kwa wafanyakazi, pamoja na Bunge

21

kutaka mabadiliko ya sheria hiyo bado kuna haja ya kutazama namna mifuko ifanyavyo kazi.

Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kuweka wazi utendaji wa Mifuko hii katika maeneo nyeti yafuatayo, kwanza Ukwasi wake (Liquidity of the Social Security funds), pili Uwekezaji (Investments) pia Risk Management reports. Taarifa katika maeneo haya hupelekwa na mifuko kwenye Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma na kutokana na utaratibu wa Kazi wa Kamati hii ya POAC ni vigumu wananchi wote kuona taarifa hizi ambazo ni muhimu kuwa wazi kwa umma. Taarifa kama hizi zitaliwezesha Bunge kuelewa kiwango cha usalama wa Mifuko hii na uwezo ziada (excess financial capacity) kuendelea kutoa huduma zinazohitajika. Kama ilivyo kwa Mabenki, tunashauri kuwa taarifa za robo mwaka za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ziwe zinatangazwa kwenye magazeti yanayosomwa zaidi nchini ili wananchi na hasa wanachama wa mifuko waone namna mifuko yao inavyofanya kazi.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa kuwa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa kipindi chote imekuwa ikitoa ushauri katika sekta hii, hatuna budi kurudia ushauri tulioutoa mwaka jana kama ifuatavyo:

“Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapendekeza kwa Mifuko ya PSPF na PPF kuangalia namna ya kuwekeza katika maeneo yanayochochea ukuaji wa uchumi na hivyo kuzalisha ajira na kupata wanachama zaidi. Maeneo kama uwekezaji kwenye Bandari na Reli yanapaswa kuangaliwa kwani kutokana na Jiografia ya nchi yetu ni maeneo yanayoweza kuzalisha faida kubwa sana. Tunaitaka Serikali ilieleze Bunge kuna mipango gani katika Mashirika haya (PSPF na PPF) kuangalia maeneo mapya ya uwekezaji katika miundombinu na hasa Bandari.

Mheshimiwa Spika, Mifuko ya hifadhi ya jamii imewekeza katika miradi ya ujenzi wa nyumba nafuu kwa ajili ya wanachama wao na pia wanachi kwa ujumla. Tunasisitiza Miradi hii isiwe Dar es salaam na Mwanza tu bali ienee nchi nzima kama ambavyo mfuko wa PSPF umeanza.


Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani pia inashauri kwamba fao la Elimu ambalo Mfuko wa PPF unatoa kwanza litolewe na Mifuko mingine pia lakini pia lipanuliwe hadi kufikia elimu ya Chuo Kikuu. Fao hili la Elimu ambalo ni muhimu sana na twapongeza mfuko wa PPF kwa kulianzisha ni fao ambalo litasaidia sana kuhakikisha kuwa yatima ambao wazazi wao wanakuwa wamefariki wanapata uhakika wa kuendelea na masomo. Fao hili liwe fao la lazima kwa mifuko yote nchini.


Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani Bungeni bado inasisitiza ushauri wake kuwa Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii ihamishiwe Wizara ya Kazi na Ajira kama Wizara inayohusika na ‘social security’. Hoja hii inatiliwa nguvu na uhalisia kwamba Mdhibiti wa Mifuko

23

(SSRA) yupo chini ya Wizara ya Kazi. Vile vile Wizara ya Fedha kama mlipaji mkuu wa Pensheni asiwe na Taasisi hata moja ya Pensheni chini yake ili kuweka ‘checks’.

Mheshimiwa Spika, Hali kadhalika hakuna sababu ya kuwa na utitiri wa mifuko mingi kama ilivyo sasa. Ipunguzwe na kubakia na mifuko miwili tu, mmoja wa wafanyakazi walio katika sekta binafsi na sekta isiyo rasmi na mwingine kwa wafanyakazi wa sekta ya umma. Tunarejea pendekezo letu kwamba mifuko ya NSSF na PPF iunganishwe kuwa mfuko mmoja kwa ajili ya sekta binafsi na sekta isiyo rasmi na mifuko ya PSPF, LAPF na GEPF iunganishwe kuwa mfuko mmoja kwa ajili ya kushughulika na wafanyakazi wa Sekta ya Umma”.

Mheshimiwa Spika, mojawapo ya vipaumbele vya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa mwaka 2012/2013 ni kupunguza misamaha ya kodi ya kutozidi asilimia moja ya GDP, kutokana na Mapato mengi ya Serikali kupotea kwa sababu ya kutoa misamaha ya kodi kwa wadau mbalimbali wanaotakiwa kulipa kodi, na ikizingatiwa moja ya michango ya waziri akiwa mbunge tarehe 25/8/2011 alisema “kupunguza misamaha ya kodi ya kutozidi asilimia moja ya GDP”. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini waziri alikuwa na nia ya dhati na kukubaliana na Kambi Rasmi ya Upinzani uwezekano wa jambo hili. Hivyo basi, ili kuonesha kuwepo kwa dhamira ya kweli Kambi Rasmi ya Upinzani inataka waziri alijulishe bunge juu ya utekelezaji wa azimio hili.

6.0 MSAJILI WA HAZINA NA BODI ZA MASHIRIKA YA UMMA

Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa mnamo mwaka 2010 Sheria namba 2 (the written laws (miscellaneous amendments) No 2. ACT 2010 ilipitishwa na katika eneo la kumi (part X) ilifanyia marekebisho sheria ya mashirika ya umma (the public Corporations Act, CAP 257). Sheria hii ilisainiwa na Rais mnamo tarehe 20 Mei 2010.

Mheshimiwa Spika, katika mabadiliko hayo ya sheria ibara ya 20 na 21 ilibainisha bayana majukumu ya msajili wa hazina na ndipo iliweka majukumu yake ya kazi kuwa ni kusimamia mashirika yote ya umma. Aidha, mabadiliko hayo yalibainisha wazi kuwa msajili wa hazina hatakuwa mjumbe wa Bodi za mashirika haya na wala hapaswi kushiriki kwenye vikao vya bodi vya mashirika haya kwani yeye ni msimamizi mkuu wa mashirika hayo na anapaswa kusimamia utendaji kazi wake.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mabadiliko hayo ya sheria bado msajili wa hazina amekuwa akihudhuria vikao mbalimbali vya bodi za Mashirika ya Umma kama mjumbe jambo ambalo ni kinyume na sheria, na amekuwa akishiriki moja kwa moja kwenye maamuzi ya bodi hizo jambo ambalo linamfanya kushindwa kutimiza wajibu wake wa kuwa msimamizi kama ambavyo sheria inaelekeza

25

Kambi ya Upinzani inataka kupata maelezo ya kina ni kwa nini hali hii imeendelea kuachwa iwe ilivyo kwa msajili wa hazina kuendelea kuwa mjumbe wa vikao vya Bodi za mashirika ya umma kinyume na sheria. Aidha tunataka kauli ya serikali kuhusiana na suala hili.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kupata maelezo ya Serikali kuhusu masuala yafuatayo.

Moja, Sakata la uuzwaji wa hisa za Shirika la UDA umefikia wapi?

Pili, Serikali imefikia wapi katika utungaji wa Sheria mpya ya Ofisi ya Msajili wa Hazina ili kuimarisha usimamizi wa Mashirika ya Umma.

Tatu, Serikali imefikia wapi katika pendekezo la kuifanyia marekebisho Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma (CHC) ili liweze kumiliki, kusimamia na kuziendesha hisa za serikali katika Kampuni binafsi ambapo umiliki wa Serikali ni chini ya asilimia 50. Pendekezo hili lilikuwa ni uamuzi wa Bunge na hivi sasa mwaka mzima umepita bila Bunge kupatiwa taarifa yeyote kinyume na maelekezo yake.


Nne, Serikali imefikia wapi katika utekelezaji wa Waraka namba moja wa mwaka 2012 kuhusu usimamizi na uendeshaji wa Mashirika ya Umma na hasa mahusiano kati ya Mashirika ya Umma na Wizara mama. Waziri wa Fedha kama msimamizi mkuu wa Mashirika ya Umma amechukua hatua gani kuhakikisha falsafa ya ‘eyes on, hands off’ katika kusimamia Mashirika ya Umma inatekelezwa

26

kikamilifu na kuhakikisha Mashirika ya Umma yanaendeshwa kwa faida na bila kuingiliwa ingiliwa na Wanasiasa?

7.0 Ofisi ya Takwimu ya Taifa

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Taifa ya Takwimu (National Bureau of Statistics – NBS) ilizinduliwa rasmi tarehe 26 Machi, 1999 kama Wakala wa Serikali (Executive Agency) kwa mujibu wa Sheria ya Wakala wa Serikali Na. 30 ya mwaka 1997, (The Executive Agencies Act 1997) (Act No. 30 of 1997), na ndio chombo rasmi kinachojihusisha na kutafuta, kuandaa na kusambaza takwimu hapa Tanzania.


Mheshimiwa Spika, katika kupanga mipango ya maendeleo na kuandaa sera mbalimbali za nchi husika, upatikanaji wa takwimu rasmi zinazotokana na Kanuni na Mbinu za Kitaalamu iliyowekwa na Ofisi ya Takwimu ya Umoja wa Mataifa (United Nations Statistical Division) ni muhimu. Takwimu zote zilizo rasmi duniani hutolewa na Ofisi za Takwimu za nchi husika kupitia Sheria za Takwimu za nchi mbali mbali.


Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imekua ikitoa Mapendekezo ya kuboresha utendaji wa Ofisi ya Takwimu katika Nyanja mbalimbali na serikali kutothubutu kuchukua mapendekezo hayo na kuyafanyia kazi.

27

Mheshimiwa Spika, katika taarifa ya miaka hamsini ya wizara,taarifa inaonesha wizara kuwa na nia ya kuboresha ofisi ya takwimu ya taifa kwa kuboresha miundombinu ya utoaji takwimu nchini ,kuimarisha mfumo wa takwimu nchini (NBS), kutoa takwimu sahihi na kwa wakati, kutokana na nia hii ya serikali Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kuzingatia Ofisi ya Takwimu Kuwa na uhisiano wa moja kwa moja wa Ofisi ya Takwimu ya Taifa na ngazi za Mikoa, Halmashauri za Wilaya, Kata na Vijiji kurahisisha upatikanaji wa takwimu ili zisaidie katika kupanga mipango ya maendeleo.

8.0 Mamlaka Ya Mapato-TRA

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inapendekeza kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania ijenge uwezo wa kukagua mahesabu ya kikodi kwenye Kampuni za Utafutaji wa Mafuta na Gesi, Kampuni za Madini na Kampuni za Simu ambazo uzoefu unaonyesha kuwa katika maeneo haya kuna mbinu nyingi sana za kukwepa kodi.

Mheshimiwa Spika, kwa msisitizo mkubwa sana Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka mamlaka ya Mapato Tanzania kushirikiana kwa karibu na Mamlaka ya Mawasiliano nchini kukagua mapato ya Kampuni za simu na hasa kampuni ambazo zinatoa huduma kwenye kampuni za Simu.

28

Mheshimiwa Spika, Katika mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Mawasiliano kulikuwa na mjadala kuhusu namna ambavyo wasanii wa Tanzania wanavyonyonywa mapato na Kampuni zinazotoa huduma ya miito kwenye kampuni za simu. Bunge lako lilielezwa kwamba Biashara ya miito kwenye simu ina thamani ya shilingi bilioni 43 kwa mwaka lakini msanii anayetengeneza kazi zinazouzwa anapata asilimia 7 tu ya mapato hayo.

Mheshimiwa Spika, taarifa zaidi za ziada zinaonyesha kuwa kampuni ya On Mobile yenye mkataba na Kampuni za Simu za Vodacom na Airtel kama ‘aggrigator’ wa miito ya simu yenye miziki ya wasanii hapa nchini hailipi kodi kutokana na mapato yake. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa taarifa za kikodi za kampuni hii na washirika wake na hatua ambazo Serikali imechukua dhidi yao. Kambi ya upinzani inashauri pia kwamba Mapato yanayotokana na miradi kama hii kwenye Kampuni za simu yawe ‘ring fenced’ na kutozwa kodi stahiki au kodi maalumu.

9.0 Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani-Internal Auditor General

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Mkuguzi Mkuu wa Ndani (Internal Auditor General) iliyoanzishwa na mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2010 inakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikileta migongano katika maeneo ya kiutendaji na uwajibikaji, sheria haipo wazi juu ya upatikanaji wa mtaalam huyo kama

29

inavyotakiwa na sheria na 8 ya utumishi wa umma, kwa mfano kutangazwa kwa nafasi hizo na waombaji kufanyiwa usaili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utata wa uteuzi wa mkaguzi wa ndani kama sheria ya utumishi wa umma inavyoelekeza mkaguzi wa ndani anasimamiwa na Katibu Mkuu Hazina (Paymaster General) ambaye naye ni mkaguliwa- kwa hiyo kunakuwa na mgongano wa kimaslahi uhuru wa ofisi ya mkaguzi wa ndani inaweza kukosa uhuru Kambi Rasmi ya Upinzani inaishauri serikali katika ofisi ya Mkaguzi wa Ndani (Internal Auditor General office) ingepaswa iwe na bodi ambako maalumu wangekuwa wanaripoti ili kuweka uhuru unaofaa.

Mheshimiwa Spika, wakaguzi wa ndani ni waajiriwa wa serikali na hufanya kazi zao za ukaguzi kwa kipindi chote ambacho shughuli za serikali zikifanyika, mfano; katika halmashauri wakaguzi hutakiwa kuwajibika kuanzia upokeaji wa fedha kutoka hazina, hadi kutumika kwake, Kambi Rasmi ya Upinzani inahoji serikali nini nafasi ya wakaguzi wa ndani kama ubadhirifu wa fedha za umma umeendelea kuwepo kama ripoti za mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali zinavyothibisha?


Mheshimiwa Spika, katika ushughulikiaji wa matumizi mabovu ya rasilimali za umma serikali imekuwa legelege hasa pale taarifa

30

zinapotolewa na wakaguzi wa ndani ambao hutoa taarifa mara kwa mara na seriakali kukaa kimya, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kutambua umuhimu wa taarifa hizi za wakaguzi wa ndani na kuhakiki inachukua hatua stahiki pasipo kusubiri taarifa za mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali ambazo ukaguzi wake hufanyika kwa kuchelewa zaidi.

10.0 Utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2011/2012 Pamoja na Mpango wa Maendeleo kwa Mwaka 2012/2013


Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Wizara ya Fedha mwaka 2011/2012 fungu Namba 50 wizara ilitenga shilingi bilioni 659 kwa ajili ya miradi ya maendeleo na fedha zilizotumika hadi kufikia Juni 2012 ni shilingi bilino 402.7 ambapo fedha za ndani zikiwa shilingi bilioni 78.65 sawa na asilimia 11.9 ya bajeti ya maendeleo hivyo kutegemea fedha za nje katika kutekeleza miradi ya maendeleo kwa asilimia 88.1. Kambi Rasmi ya Upinzani, pamoja na Seriliali kutokubali kutumia mapato ya ndani zaidi katika kugharimia miradi ya maendeleo, I azidi kushauri serikali kuwa na Makati wa dhati wa muda mrefu wa kuachana na utaratibu wa kutegemea misaada ya nje. Mkakati huo ulenge kuiongezea mapato kwa kutumia mbinu mbalimbali za kodi.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya 2012/2013 serikali imetenga shilingi bilioni 546.51 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo

31

ambayo ni pungufu kwa asilimia 18 ya bajeti ya mwaka 2011/2012 ambapo serikali ilitenga shilingi bilioni 659. Katika bajeti ya 2012/2013 ni asilimia 19.3 tu ya fedha za ndani ndizo zimeelekezwa kwenye miradi ya maendeleo na asilimia 80.7 ya makadirio ni fedha za nje ikiwa ni mikopo ya kibiashara na misaada. Kambi Rasmi ya Upinzani inahoji: ni maendeleo yapi ambayo serikali inadhamiria kwa kutenga fedha ya maendeleo ambayo ni pungufu kwa asilimia 18 ya bajeti ya mwaka jana?

Hitimisho

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani Bungeni inasisitiza umuhimu wa kuisimamia vema Wizara ya Fedha katika kusimamia uchumi wa nchi. Tuna imani kwamba Waziri wa Fedha ndugu William Mgimwa na Manaibu wake Mhe. Janeth Mbene na Mhe. Saada Mkuya Salum wataweza kukabili changamoto tulizoainisha katika hotuba yetu na kufanyia kazi mapendekezo ambayo tumeyatoa. Tumeona dalili za Wizara hii na hasa Waziri na Manaibu wake kusikiliza katika masuala ya Kikodi hivyo, tuna imani kwamba wataendelea kusikiliza.

Kambi Rasmi ya Upinzani haitasita kutoa ushirikiano kwa lengo la kuleta maendeleo katika nchi yetu. Hata hivyo, tutakosoa kwa nguvu zetu zote na kuchukua hatua za kiuwajibikaji dhidi ya njama zozote za kudhoofisha maendeleo ya Taifa na watu wake. Siku zote tutasimama upande wa wanyonge na kuwasemea wasio na sauti,

32

Watanzania milioni 30 wanaoishi vijijini na kwenye dimbwi la Umasikini (The Bottom 30M).

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani naomba kuwasilisha.

……………………………………

Kabwe Zuberi Zitto (Mb)
Waziri Kivuli-Wizara ya Fedha
12.08.2012

KIAMBATANISHO A.

Sheria mbalimbali kuhusiana na fedha haramu

i. the establishment of the Permanent Commission of Inquiry, or Ombudsman, 1966;

ii. the Foreign Exchange Control Act 1966;

iv. the establishment of an anti-corruption squad in 1975;

v. the Economic Sabotage Act 1983;

vi. the Economic and Organised Crime Act 1984;

vii. the Proceeds of Crime Act 1991;

viii. the Leadership Code (Declaration of Assets) Act 1995;

ix. the appointment of the Presidential Commission of Inquiry into Corruption, 1996;

x. the BOT Circular to Banking and Non-banking Financial Institutions, No. 8 of 2000, on Money Laundering.


xi. the Drugs and Illicit Traffic of Drugs Act 1995;

xii. the Arms and Ammunition Act 1991;

xiii. the Mutual Assistance in Criminal Matters Act 1991; and

xiv. the Tanzania Intelligence and Security Act 1998.

xv. The anti-money laundering Act, 2007

xvi. the anti-money laundering (amendment) act, 2012
 
Chanzo: Dodoma Yetu