TPDC KUMALIZA MATUMIZI YA MKAA DAR

Na Mwandishi wetu Katika jitihada za kutunza mazingira na kupunguza kasi ya ukataji miti ili kupata nishati, Shirika la Maendeleo ya Pe... thumbnail 1 summary


Na Mwandishi wetu
Katika jitihada za kutunza mazingira na kupunguza kasi ya ukataji miti ili kupata nishati, Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) linasambaza gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani badala ya kutegemea kuni na mkaa.
Mradi huo wa TPDC unaolenga kufikisha nishati hiyo majumbani ulianzia Mikocheni, Dar es Salaam na sasa unaelekea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ukitarajiwa kuwapatia huduma hiyo wakazi wanaoishi kwenye mitaa iliyopimwa kwanza.
Dar es Salaam yenye wakazi zaidi ya milioni tano watu milioni 4.9 hupikia nishati ngumu ikiwemo kuni na mkaa wakati wachache hutumia gesi, umeme na mafuta ya taa.
Mhandisi wa Petroli wa TPDC, anayeshughulia mradi huo, Modestus Lumato, aliliambia NIPASHE Jumapili, katika mahojiano ya jitihada za TPDC katika kutunza mazingira na kuendeleza matumizi ya nishati mbadala majumbuni.
Alifahamisha kuwa mradi huo unasambaza gesi asilia inayotoka Songosongo mkoani Lindi lakini pia utatumia ile ya Mtwara baada ya ujenzi wa bomba jipya la gesi la Mtwara –Dar kukalimika mwakani. Alisema ufungaji ulianzia kwenye nyumba za TPDC Mikocheni ambazo wakazi wake wameanza kuitumia.
Aliongeza kuwa sehemu zenye ramani za mitaa zote zitafikiwa na usambazaji huo unaohusisha kujenga bomba la gesi na kuwafikishia watumia watakaonunua kwa mtindo wa “LUKU’.
“Tutaanza muda wowote kusambaza nje ya TPDC baada ya pesa kupatikana toka Hazina. Ni mradi unaosimamiwa na TPDC na ni mali ya serikali kwa asilimia mia. Bajeti ya Sh bilioni 30 imetengwa kwa ajili ya kusambaza mabomba ya gesi Dar es Salaam.”
Lumato alifahamisha kuwa kazi ya kusambaza gesi asili ikikamilika jijini TPDC itaendelea mikoani kama Mtwara na Lindi ambapo nishati hiyo inapatikana kwa wingi.
Akitofautisha gesi asili na ile inayotumika majumbani sasa , Lumato alisema ile ya asili ni nishati rahisi mno duniani ikilinganishwa na ya viwandani iitwayo ‘Liquid Petroleum Gas’ (LPG) inayotokana na kusafisha mafuta ghafi , lakini ile ya asili inatokana na kuoza masalia ya viumbe hao waliokufa miaka milioni kadhaa iliyopita.
Aliongeza gesi asili ni nafuu kwani mteja aliyekuwa anatumia mitungi miwili ya LPG ya kilo 15 kwa mwezi atapunguza gharama kwa kutumia gesi asili ya Sh. 50,000 kwa miezi sita. Mtungi wa kilo 15 wa LPG huuzwa Sh. 55,000.
Tanzania imegundua tabaka la gesi lenye ujazo wa fiti za mraba trilioni 35 zilizopatika mikoani Mtwara na Lindi na ujenzi wa bomba la kuisafirisha kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam unaofanywa na mkandarasi kutoka China umeanza na utarajiwa kukamilika baada ya miezi 18.
Kadhalika iligundua fiti za mraba trilioni tatu eneo la Mnazi Bay na kiasi kingine cha fiti trilioni mbili zipo katika kisiwa cha Songo Songo ambazo hutumika kuzalisha umeme na kwenye baadhi ya viwanda.
Chanzo: Nipashe Jumapili