Tabora.
VIJIJI vitatu katika Kata ya Ndevelwa, Manispaa ya
Tabora viko hatarini kukumbwa na njaa, hali ambayo imetishia wakazi
zaidi ya 6790 waishio kwenye vijiji hivyo.
Wakazi wa vijiji vya kata ya Ndevelwa tayari
imebainika kuwa wamekuwa wakila mlo mmoja kwa siku na wengine hata
kupitisha siku nzima bila kula.
Akizungumza na gazeti hili,Diwani wa kata ya
Ndevelwa Seleman Maganga, amekiri kuwepo kwa hali hiyo huku akiitaka
serikali kuchukua juhudi za makusudi kukabiliana na janga hilo.
Maganga alisema tatizo hilo ni matokeo ya hali ya
ukame iliyovikumba vijiji hivyo tangu mwishoni mwa mwaka jana,na tayari
amekwishalifikisha kwenye vikao vya baraza la madiwani na kujadiliwa.
Alifafanua kuwa kwa upande mwingine hali hiyo
imechangiwa na idadi kubwa ya vijana waishio vijiji vya Inala,Ituru na
Ndevelwa kutoshiriki shughuli za kilimo hata cha bustani na kuwaachia
wazee peke yao ambao huzalisha kidogo kulingana na uwezo wao.
Aidha alisema idadi kubwa ya vijana wamekuwa
wakikimbilia mjini na wale wanaobaki vijijini hujihusisha na vitendo vya
kihalifu ili mradi kujihakikishia kipato kisicho cha halali.
Hata hivyo baadhi ya wakazi wa vjijiji hivyo
waliolima zao la muhogo wanalazimika kuuza madebe mawili kwa Sh16,000
ili wakanunue debe moja la mahindi, ambalo wanadai kuwa ndio
linatosheleza kwa mlo wa siku saba katika familia moja.
Mwaka 2010 serikali ilitoa chakula cha msaada
baada ya vijiji hivyo vya kata ya Ndevelwa kukumbwa na mvua kubwa
iliyoharibu mazao ya chakula na biashara kama tumbaku na mahindi.
Chanzo: Mwananchi
Chanzo: Mwananchi