na Hellen Ngoromera, Mtwara
MFUMKO mkubwa
wa dhahabu umegundulika kuwepo katika kijiji cha Lukwika, wilaya ya Nanyumbu,
mkoani Mtwara.
Hatua hiyo
ilitangazwa mwishoni mwa wiki mjini hapa na Kaimu Kamishna wa Madini Kanda ya
Kusini, Aloyce Tesha, alipozungumza na waandishi wa habari walioko kwenye ziara
kutembelea miradi ya Wizara ya Nishati na Madini mkoani hapa.
Alisema dhahabu
hiyo iligundulika wiki mbili zilizopita na tayari ofisi yake kwa kushirikiana
na Wakala wa Ukaguzi wa Madini Nchini (TMAA) imetuma timu ya wataalamu katika
eneo hilo, ili kudhibiti madini hayo ili serikali iweze kupata kodi na ushuru
unaostahili kutoka kwa wachimbaji.
“Tayari
wachimbaji pamoja na watoa huduma zaidi ya 7,000 wako katika eneo hilo na
kwamba tushatuma wataalamu,” alisema Tesha.
Pamoja na mambo
mengine, alisema mkoa wa Mtwara una aina mbalimbali za madini yakiwemo ya
chumvi ambayo huzalishwa kandokando ya bahari na jasi kwenye viwanda na
mengineyo.
Alisema kwa
sasa kuna maandalizi makubwa ya uzalishaji wa saruji mkoani hapa.
Tesha alisema
tayari kampuni ya kufanya shughuli hiyo imeshapatikana na hivi sasa iko kwenye
hatua za mwisho kuanza kazi hiyo.
Msemaji wa
Wizara ya Nishati na Madini, Fadhil Kilewo, alisema lengo la ziara hiyo ni
kuwawezesha waandishi wa habari kujifunza masuala mbalimbali ya wizara hiyo na
kuihabarisha jamii kwa ufasaha.
Chanzo: Tanzania Daima