Rais Kikwete kuzindua rasmi Jiji la Arusha

Na Eliya Mbonea, Arusha. RAIS Jakaya Kikwete, kesho atazindua hadhi ya Jiji la Arusha, baada ya kukabidhiwa hati rasmi ya kutambulika kuto... thumbnail 1 summary
Na Eliya Mbonea, Arusha.
RAIS Jakaya Kikwete, kesho atazindua hadhi ya Jiji la Arusha, baada ya kukabidhiwa hati rasmi ya kutambulika kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Hati hiyo ilitolewa Agosti 15, 2012, ambapo uzinduzi rasmi sasa unatarajiwa kufanywa katika Mnara wa Mwenge jijini hapa.


Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo.

Alisema mbali na kuzindua Jiji la Arusha, Rais Jakaya Kikwete, atakuwa na ziara ya kikazi ya siku tatu.

“Rais atazindua Hospitali ya Oltrumet kule Arumeru Magharibi, ataweka jiwe la msingi ujenzi wa Barabara ya Arusha–Minjingu.

“Shughuli nyingine atakayoifanya akiwa mkoani kwetu, ni kuzungumza na wananchi katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid hiyo Novemba Mosi,” alisema Mulongo.

Alisema Novemba 2, 2012, Rais Kikwete atazindua Chuo Kikuu cha Mandela cha Sayansi na Teknolojia na kisha kutembelea kiwanda cha A to Z.

Alisema ziara hiyo itakwenda hadi Novemba 3, mwaka huu ambapo atakwenda kuzindua Shule ya Msingi ya Sokoine, iliyojengwa katika eneo la JWTZ Monduli.

“Baada ya shughuli hiyo, atakwenda kuweka jiwe la msingi katika eneo la Nanja Barabara ya Arusha hadi Minjingu,” alisema Mulongo.

Kwa upande wake, Meya wa Arusha, Gaudence Lyimo, alisema kupatikana kwa cheti hicho, kunaipa mamlaka iliyokuwa Halmashauri ya Manispaa ya Arusha kutumia rasmi hadhi ya jiji.

“Hii inatufanya kubadilisha kuanzia nyaraka zote za vitendea kazi, pamoja na Nembo ya Manispaa ambapo sasa tutatumia nembo mpya.

Alisema Halmashauri hiyo ilianza tangu mwaka 1948, ikiwa ni Halmashauri ya Mji baada ya kukua kwa mji, ambapo ilipandishwa hadhi na kuwa manispaa mwaka 1980.

Kutokana na kupanuka kwa shughuli katika eneo la kilomita za mraba 93, Serikali iliamua kupandisha hadhi ya eneo hilo hadi kufikia kilomita za mraba 2,008.

“Hii ni kwa mujibu wa tangazo la Serikali namba 341 la Oktoba 14, mwaka 2011,” alisema Meya Lyimo.

Chanzo: Mtanzania