TEMBO WAUA WATU WAWILI

na Joseph Malembeka, Morogoro KUNDI kubwa la tembo limeibuka katika vijiji vya Kata ya Bwakila Chini, wilayani Morogoro na kuua... thumbnail 1 summary
na Joseph Malembeka, Morogoro

KUNDI kubwa la tembo limeibuka katika vijiji vya Kata ya Bwakila Chini, wilayani Morogoro na kuua watu wawili na kujeruhi watatu wakiwamo wawili waliojeruhiwa vibaya na kulazwa katika kituo cha afya Duthumi.
Diwani wa kata hiyo, Pesa Pesa, aliwataja waliouawa kuwa ni mwalimu mstaafu, Thobias Alfani (74) na Milembe Pawa (38).
Alisema waliojeruhiwa ambao sasa wamehamishiwa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ni Dogomisi Makinga (18) na Holo sagala (3) na wengine walitibiwa na kuruhusiwa.
Alisema kundi hilo la tembo liliibuka alfajiri ya kuamkia juzi kijijini hapo na kuanza vurumai hiyo kabla hawajadhibitiwa na askari wa wanyama pori kutoka Hifadhi ya Selous.
Alisema Alfani alikutwa na zahama hiyo akiwa porini kutafuta kuni ambazo hufanya biashara kijijini hapo huku Pawa alikutwa na zahama hiyo akiwa njiani na mwanae.
Aliongeza kuwa baada ya watu kupata taarifa ya tukio hilo waliingia mitaani kuwasaka tembo hao.
Akizungumzia hali za majeruhi, Daktari wa Kituo cha Afya Dhutumi, Japhet Gande, mbali na kukiri kupokea majeruhi hao, alisema wamehamishiwa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu zaidi
Chanzo: Tanzania Daima