Mchina anaswa na mfupa wa tembo

RAIA wa China, Chen Weitao, dereva wa Kampuni ya ujenzi ya Chico inayotengeneza barabara ya Musoma-Mwanza, amekamatwa na askari wa Kikosi c... thumbnail 1 summary
RAIA wa China, Chen Weitao, dereva wa Kampuni ya ujenzi ya Chico inayotengeneza barabara ya Musoma-Mwanza, amekamatwa na askari wa Kikosi cha Kudhibiti Ujangili akiwa na mfupa uliokauka wa mguu wa tembo.
Weitao alikamatwa juzi, majira ya saa sita mchana, eneo la Nyasura katika mji mdogo wa Bunda.
Ofisa mmoja wa kikosi hicho Kanda ya Serengeti ambaye hakutaka kutajwa jina alisema walipata taarifa kutoka kwa raia mwema.
Alisema baada ya kupata taarifa hiyo walikwenda moja kwa moja eneo hilo na kumkuta Weitao akiwa na gari T 340 BBR na baada ya kulikagua walikuta mfupa huo ukiwa kwenye sehemu ya kutunzia spana.
Alisema walimkamata raia huyo wa China aliyekuwa na msaidizi wake aitwaye, Michael Renatus, na kuwapeleka kituo cha polisi ambako waliwaweka chini ya ulinzi na kuwahoji.
Raia huyo wa China alidhaminiwa juzi baada ya kukabidhi hati yake ya kusafiria katika Kituo cha Polisi Bunda na kupewa gari lake ingawa ataendelea kuhojiwa na kikosi hicho.
Hii ni mara ya nne sasa kwa Wachina hao kukamatwa na nyara za serikali tangu waanze kujenga barabara hiyo, ambapo mwaka jana walikamatwa na vipande vya meno ya tembo katika kambi yao iliyopo Sabasaba.
Polisi wilayani hapa wamekiri kukamatwa kwa Mchina huyo na kudai suala hilo linasimamiwa na Kikosi cha Kuzuia Ujangili Kanda ya Serengeti, ambao kwa hivi sasa wana wanasheria wao ambao wanaandaa mashitaka na kuwafikisha mahakamani watuhumiwa hao.

Chanzo: Tanzania Daima