Picha na maelezo: Mtalii aliyeuawa na tembo Tarangire alikuwa ni afisa mkubwa Marekani

Dr Thomas McAfee  MTALII mmoja raia wa Marekani, Thomas Macfee (58), alieuawa na kundi la tembo wakati akiwa kwenye kambi ya Kakoi Ta... thumbnail 1 summary
Dr Thomas McAfee 

MTALII mmoja raia wa Marekani, Thomas Macfee (58), alieuawa na kundi la tembo wakati akiwa kwenye kambi ya Kakoi Tarangire eneo linalodaiwa kuwa ni mapito ya asili ya wanyama hao alikuwa ni mfanyakazi wa chuo cha Califonia kampasi ya San Diego. Alikuja Tanzania kwenye mapumziko ili akirejea aingie kwenye nafasi yake mpya aliyopewa ya kuwa Mtendaji Mkuu wa Keck Medicine of University of Southern California (USC) Medical Foundation.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Manyara, Musa Marambo, alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 30 mwaka huu, saa 2:30 asubuhi baada ya mtalii huyo akiwa na wenzake watano ambao majina yao hayakupatikana kujaribu kupiga picha za kundi kubwa la tembo lililokuwa likipita karibu na eneo walilokuwa.

Alisema kuwa wakiwa kwenye harakati za kupiga picha, ghafla tembo hao walibadili uelekeo na kuanza kuwafuata ndipo wakaanza kukimbia ambapo kwa bahati mbaya Macfee alinasa kwenye dimbwi la matope.
“Baada ya kunasa kwenye matope alishindwa kutoka ndipo tembo wale wakaanza kumpitia juu na baada ya hapo wenzake walienda kumchukua na kumuwahisha kwenye zahanati ya hifadhi ya taifa ya Tarangire ndipo akafariki,” alisema Manyara.

Alisema kuwa baada ya kufariki alipelekwa kuhifadhiwa kwenye hospitali ya Selian jijini Arusha ambapo ubalozi wa Marekani ulimchukua kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Meneja uhusiano wa Tanapa, Paschal Shelutete, alitoa taarifa kwa vyombo mbalimbali vya habari akifafanua kuwa eneo alilokuwa mgeni huyo ni nje ya hifadhi yao.

“Tukio la mgeni husika lilitokea nje ya hifadhi ya Tarangire katika kijiji cha Kakoi kambi ya Tarangire River Camp, wakiwa wanafanya utalii wa kutembea kwa miguu.”

“Baada ya kuvamiwa na kuumizwa, mgeni huyu alifikishwa katika zahanati ya Tarangire na watumishi wa kambi aliyofikia ambayo iko nje ya hifadhi kwa ajili ya matibabu ya huduma ya kwanza ambapo alifariki,” alisema.