UDSM: Mabadiliko tabianchi ni tishio

Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kimesema, Bara la Afrika lisipochukua hatua za makusudi za kupambana na Mabadiliko ya Tabianchi, linaweza kuan... thumbnail 1 summary
Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kimesema, Bara la Afrika lisipochukua hatua za makusudi za kupambana na Mabadiliko ya Tabianchi, linaweza kuangamia kwa ugumu wa maisha.
Pia, chuo hicho kimeitahadharisha Serikali ya Tanzania, kupambana na mabadiliko hayo hususan kutenga maeneo ya wakulima na wafugaji kuepuka migogoro inayoweza kusababisha vurugu na kugharimu maisha ya watu.
Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi wa Kituo cha Mabadiliko ya Tabianchi wa chuo hicho, Profesa Pius Yanda wakati akielezea kuhusu mkutano wa kimataifa wa kujadili tatizo hilo utakaofanyika Oktoba 15, mwaka huu jijini Arusha.
Profesa Yanda alisema, tatizo la mabadiliko ya tabianchi barani Afrika linatokana na kutokuwapo kwa jitihada za makusudi za kupambana na janga hilo.
Alisema katika mkutano huo utakaoandaliwa na chuo hicho, utashirikisha wanasayansi na watunga sera kutoka Barani Afrika, America na Asia ambapo Tanzania ni mwenyeji wa mkutano huo.
“Bara la Afrika limekuwa likifanya tafiti kidogo katika mambo ya Tabianchi lakini hata hivyo, bado hazifanyiwi kazi hivyo kupitia mkutano huo tutakuwa na wataalamu kutoka nje ya bara hili ambao watatupa ujuzi wa kupambana na mabadiliko hayo,” alisema Profesa Yanda na kuongeza:
“Ili kuelewa kwa kina jinsi ya kupambana na mabadiliko haya, ni lazima kufanya tafiti nyingi zitakazobainisha ni maeneo gani kunahitajika kufanyiwa kazi.”
Profesa huyo alisema, migogoro ya wafugaji na wakulima inatakiwa kutengewa maeneo mapema kwa ajili ya shughuli zao ili kuepuka pindi eneo fulani linapoathiriwa na mabadiliko hayo kuhamia katika eneo jingine na kusababisha kutokea vurugu.

Chanzo: Mwananchi