Hadi kufikia Agosti mwaka huu 2013 Tanzania ina jumla ya marubani 539, takribani asilimia 40 ya marubani hao ni watanzania yaani marubani 208
Kuwepo kwa idadi ndogo ya marubani kunachangiwa na gharama kubwa za ada katika vyuo vya urubani pia uchache wa vyuo vinavyoweza kutosheleza mahitaji ya wanafunzi kwa gharama ndogo hapa nchini.
Afisa Habari wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Nchini (TCAA) Bestina Magutu ameuambia mtandao wa tabianchi kuwa kwa sasa mafunzo ya urubani yanayotolewa na vyuo vya Tanzania ni yale ya ngazi/ leseni Private Pilot Licence(PPL) .
“Mafunzo ya kuanzia ngazi ya Commercial Pilot Lisence(CPL) na yanatolewa nje ya nchi ikiwa ni pamoja na nchi za Afrika, mfano Afrika Kusini, Ethiopia” anasema Magutu.
TCAA inamiliki chuo kinachotoa mafunzo ya usafiri wa anga yaani Tanzania Civil Aviation Center-CATC na miongoni mwa mafunzo yanayotolewa na chuo hicho ni pamoja na ya uongozaji Ndege (Air Traffic Management), Taarifa Za Usafiri Wa Anga (Aeronautical Information Services ) na Usalama ( Aviation security).
Aidha Mamlaka inatumia maonyesho mbali mbali, mfano maonyesho ya Nane Nane kutoa elimu kuhusu namna mtu anavyoweza kujiunga na mafunzo ya usafiri wa anga, sifa anazopaswa kuwa nazo.
TCAA pia inaratibu mfuko wa mafunzo ya marubani na wahandisi (usafiri wa anga) ambao katika awamu ya kwanza umetoa udhamini wa mafunzo kwa marubani 5 watakaofanya mafunzo yao nchini Afrika Kusini.
Tayari kundi hilo la kwanza la wanufaika limeanza masomo( kuanzia Septemba, 2013) Lengo ni kuongeza idadi ya watalaam wazalendo katika sekta ya usafiri wa anga nchini.