Serikali: Migogoro ya Tanapa, wananchi imalizwe

KAMATI  ya  Kudumu ya Bunge ya Maliasili na Mazingira, imeitaka serikali kuhakikisha inashughulikia migogoro yote ya ardhi inayohusu Tanapa... thumbnail 1 summary
KAMATI  ya  Kudumu ya Bunge ya Maliasili na Mazingira, imeitaka serikali kuhakikisha inashughulikia migogoro yote ya ardhi inayohusu Tanapa na wananchi.
Akizungumza hivi karibuni na waandishi wa habari kamati hiyo ilipofanya ziara jijini Mbeya, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, James Lembeli, alisema kuna migogoro  ya mipaka inayozikabili baadhi ya hifadhi za taifa nchini.
Akitolea mfano, Lembeli alisema hifadhi ya taifa ya Ruaha yenye eneo oevu la  Ihefu iliyoko mkoani hapa ilikumbwa na mgogoro huo baada ya Kkikao cha Maendeleo cha Mkoa (RCC), kushindwa kusimamia suala hilo kikamilifu.
Alisema  baada ya kujitokeza mgogoro huo serikali iliunda kamati mbalimbali kwa ajili ya kuchunguza na tayari umeshafanyiwa kazi.
Alisema kilichosababisha kuchelewa kutolewa kwa maamuzi ya kamati ni kesi zilizofunguliwa  mahakamani zinazohusu  mgogoro huo wa mipaka katika hifadhi hiyo.
Aidha alienda mbali na kusema kuwa serikali inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha  wananchi wake hawapati mateso au  usumbufu usio wa lazima katika maeneo  yao kwa  kwani ndiyo wenye rasilimali hizo.
Pia alibainisha kuwa maeneo mengi  yanayotumiwa na wananchi, yamekuwa na migogoro mingi inayohusu mipaka ya ardhi hasa wakati wa shughuli za upanuzi wa hifadhi za taifa au uwezekezaji  mkubwa unapotakiwa kufanyika jirani na makazi ya wananchi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Maimuna Kibenga, alisema mipango ya wizara yake iko katika hatua nzuri ikilenga kuondoa au kumaliza migogoro yote ambayo imekuwa ikijitokeza katika maeneo mengi ya hifadhi za taifa nchini.
Maimuna alisema kuwa wizara yake kupitia bodi ya hifadhi za taifa imekuwa ikifanya kazi kwa kufuata taratibu kanuni na sheria zinazoiongoza wizara hiyo hivyo hatarajii kuona mambo yanaenda kinyume kwa kuwa kila mtumishi wa wizara hiyo anatakiwa kufanya kazi kwa kuheshimu na kuzingatia sheria.
Pia Dk. Martin Loibooki ambaye ni Mkurugenzi  wa Hifadhi za Taifa (Tanapa), alisema kuwa kazi na majukumu ya Wizara  ya Maliasili na Utalii ni uhifadhi si vinginevyo.
Hata hivyo alitahadharisha kuwa huenda shirika hilo  likafungwa  katika siku zijazo kutokana na mifumo mipya iliyopo ambayo lengo lake halilengi kuendeleza shirika bali kusababisha  mwingiliano wa kiutendaji na kudhoofisha uwajibikaji kwa kuwa mfumo uliopo, hauko  kwa ajili ya maslahi ya shirika hilo.

Chanzo: Tanzania Daima