TATO waiomba serikali iwasaidie

UMOJA wa Waongoza Watalii Tanzania (TATO), wameiomba serikali kushirikiana nao kikamilifu kukuza sekta ya utalii hapa nchini ili kuongeza m... thumbnail 1 summary
UMOJA wa Waongoza Watalii Tanzania (TATO), wameiomba serikali kushirikiana nao kikamilifu kukuza sekta ya utalii hapa nchini ili kuongeza mapato ya taifa.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa TATO, Wilbard Chambulo, alipokuwa akijibu hoja za wabunge mbalimbali waliohudhuria semina iliyoandaliwa na umoja huo kwa lengo la kuwaelimisha umuhimu wa sekta ya utalii.

Chambulo alisema Kenya inapiga hatua kubwa katika kutangaza utalii, kuongeza watalii, kurekebisha sheria na kukarabati miundombinu kutokana na serikali ya nchi hiyo kushirikiana na sekta binafsi zinazojishughulisha na masuala ya utalii.

Alisema kama Serikali ya Tanzania haitabadili dhana yake dhidi ya sekta binafsi inayojishughulisha kwenye utalii na kushirikiana nayo kikamilifu pato la taifa pamoja na ajira za wanaofanya shughuli hizo zitazidi kudidimia siku hadi siku.

Chimbulo alibainisha kuwa Tanzania imekuwa ikiwakaribisha wawekezaji na kusajili kampuni za utalii bila kuzifuatilia kwa ukaribu zaidi, jambo linalochangia kuongezeka kwa kampuni za mifukoni pamoja na ujangili wa tembo na uhalifu wa rasilimali za taifa.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii, Khamis Kagasheki, alikiri kuwa serikali imekuwa na mtazamo usio sahihi kwa kampuni binafsi za utalii hali iliyochangia kusuasua kwa maendeleo kwenye utalii.

“Tuna sheria nyingi zinazochangia kukwaza sekta ya utalii, mfano hapa kwetu vibali vya kufanya utalii vinaweza kuchukua hadi miezi sita wakati wenzetu wa Kenya vinapatikana ndani ya siku zisizozidi mbili, hapa ni lazima tubadilike ili tujinusuru kwenye anguko hili,” alisema.

Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Ritta Mlaki (CCM), alisema serikali imewatelekeza waongoza watalii hapa nchini, hali inayowafanya wajiongoze kama watoto yatima hatua inayochangia ufanisi na tija kutopatikana kwa kiwango kinachokidhi mahitaji ya taifa.

“Ndugu zangu wa TATO nyinyi ni watoto lakini kuanzia sasa tumeamua kushirikiana nanyi, tuleteeni mikakati ya kukuza sekta ya utalii na sisi tutaishauri na kuisimamia serikali ili tuongeze ajira na fedha zitakakuza uchumi wetu,” alisema.

Naye Katibu Mtendaji wa TATO, Mustapha Akunaay, alisema wameandaa semina hiyo kwa wabunge wa Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira pamoja na Kamati ya Bajeti ili waifahamu zaidi sekta ya utalii na waandae mazingira bora ya kuiboresha kwa lengo la kukuza ajira na uchumi wa taifa


Chanzo: Tanzania Daima