WAJUE VYURA WA KIHANSI

Chura wa Kihansi kama zilivyo raslimali nyingine ni maliasili muhimu ya watanzania.Chura wa kihansi aligundulika mwaka 1996 katika mapromo... thumbnail 1 summary
Chura wa Kihansi kama zilivyo raslimali nyingine ni maliasili muhimu ya watanzania.Chura wa kihansi aligundulika mwaka 1996 katika mapromoko ya maji yaitwayo Mhalala yaliyoko ndani ya Milima ya Udzungwa katika Wilaya ya Kilombero,Mkoa Morogoro.Chura huyu anaishi kwenye mazingira ya maji yanayotiririka na kutoa mvuke mwingi sana kutokana na nguvu ya maji.Chura huyu ambae kitalaamu anaitwa Nectophrynoides asperginis hapatikani sehemu nyingine yeyote duniani isipokuwa katika bonde la Kihansi nchini Tanzania tu.

Chura wa kihansi ni chura pekee katika jamii ya vyura waliopo duniani kwa sababu vyura hawa hutaga mayai na kukaa nayo kwenye kifuko kilichopo ndani ya chura mwenyewe hadi muda wa kuanguliwa unapofika na ndipo hutoa vitoto hai.Kwa lugha rahisi ni kwamba Chura hawa huzaa kwa sababu hatagi mayai yakaonekana bali hukaa ndani ya Chura mwenyewe.

Chura huyu anatofautiana na vyura wengine kwa sababu vyura wa jamii nyingine hutaga mayai na kuyaacha majini ambako huanguliwa wakati mama yao hayo,wakati Chura wa kihansi huangulia tumboni na kuwazaa watoto wakiwa hai,tabia hii ya kuzaa ndio inayomfanya chura huyu kuwa wa kipekee duniani

Chura huyu amewekwa kwenye kundi la viumbe wanaolindwa kutokana na kutoweka kwake na kuwekwa kwenye kifungu cha kwanza cha Mkataba wa Biashara ya Wanyamapori na Mimea iliyo hatarinikutoweka.Mkataba huu kwa Kiingereza unaitwa "Convention on International Trade in Endangered Species" (CITES) na kisheria chura huyu hawezi kufanyiwa biashara ya aina yeyote hapa duniani.

Maporomoko ya korongo la Mto Kihansi ambayo ndiyo makazi ya asili ya Chura hawa yana ukubwa wa eneo la urefu wa Kilometa nne na upana wa nusu Kilometa.Bonde la Mto Kihansi linapatikana katika mto Kihansi unaoanzia katika Wilaya za Mufindi na Kilolo Mkoa wa Iringa na kupeleka maji yake katika Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro.

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii na taasisi zake zimekuwa zikiandaa mradi wa utunzaji wa mazingira katika bonde la Mto Kihansi "LKEMP" Mradi huu unasimamiwa na Baraza la Taifa la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira "NEMC "

Katika kurudisha mazingira asilia ya vyura hawa,mradi wa "LKEMP"wameweka mabomba yanayotoa maji yenye uvuke unaofanana na ule wa asilia kwa ajili ya kurudisha uoto uliokuwapo.Kazi hii imekua ikifanyika kwa kushirikiana na idara ya Wanyamapori kupitia taasisi yake ya utafiti wa wanyamapori "TAWIRI" Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira " NEMC" ,Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Sokoine.


Chanzo: Maliasili Zetu