CCM Singida yataka wanaowavamia Wahadzabe wafukuzwe

CHAMA Cha Mapinduzi CCM mkoa wa Singida kimemuagiza mkuu wa Wilaya ya  Mkalama kuwaondoa kwa nguvu wavamizi wa hifadhi ya por... thumbnail 1 summary
CHAMA Cha Mapinduzi CCM mkoa wa Singida kimemuagiza mkuu wa Wilaya ya  Mkalama kuwaondoa kwa nguvu wavamizi wa hifadhi ya pori la Kipamba/Munguli wanamoishi na wananchi wa jamii ya  Kabila la Wahadzabe.
Wavamizi hao kutoka mikoa ya Arusha, Manyara, Shinyanga, Simiyu na Singida, wanadaiwa kufyeka  pori  hilo na kuchoma moto kwa shughuli za kilimo  na ufuagaji, hali iliyosababisha adha kubwa kwa jamii hiyo ambayo huishi kwa kutegemea mizizi, asali, matundapori na nyama  kama chakula chao kikuu.
Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa CCM  mkoa wa Singida Mgana Msindai baada ya kuitembelea jamii hiyo inayoshi kwenye pori lililopo umbali wa zaidi ya Km 120 kaskazini mashariki mwa mji wa Singida.
Amesema ingawa kumekuwepo na tishio la  baadhi ya  wananchi kukinyima kura chama chake kwenye  chaguzi mbalimbali iwapo  wavamizi hao wataondolewa, lakini CCM haiwezi kukubali uharibifu huo wa mazingira uendelee na wahadzabe kukosa vyakula vya asili kwa kuogopa kupoteza kura.
Kutokana na hali hiyo bwana Msindai amemtaka mkuu wa Wilaya ya Mkalama kutumisha sheria zilizopo kuwaondoa kwa  nguvu  haraka wavamizi kwenye hifadhi hiyo kabla hawajasabisha uharibifu zaidi.