MWENYEKITI wa Kamati ya Maliasili na Mazingira, James Lembeli,
amesema kamati hiyo itaanza kazi ya kuchunguza tuhuma mbalimbali
zilizotolewa na wabunge kuhusu mwenendo mzima wa Operesheni Tokomeza
Majangili iliyositishwa hivi karibuni Novemba 18 mwaka huu.
Akizungumza na Tanzania Daima jana alisema kamati yake itaanza kazi
ya kuchunguza mikoa mbalimbali iliyolalamikiwa kuwa operesheni hiyo
imesababisha mauaji ya mifugo na binadamu.
Alisema maeneo watakayoenda ni Kigoma, Rufiji, Maswa, Meatu, Simiyu,
Bukombe, Kahama na Biharamulo huku akiahidi yeye na kamati yake kufanya
kazi hiyo kwa ufanisi, maadili na kutoa ripoti iliyo sahihi.
Hata hivyo, Lembeli ambaye pia ni Mbunge wa Kahama alimpongeza Waziri
wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, kwa kuendelea
kuwanasa majangili wanaoendelea kuua tembo.
Alisema watu wengi na hasa wanasiasa wanafanya jambo hilo kuwa la
kisiasa na wakidhani kuwa ni jambo la kitoto bila kujua ukubwa wa
tatizo lenyewe na kuwataka badala ya kuweka siasa wawape moyo wale wote
walio katika mapambano hayo.
Chanzo: Tanzania Daima