Na
Mohammed Mhina wa Jeshi la Polisi-Zanzibar
ZANZIBAR
NOVEMBA 15, 2013. Jeshi la Polisi Zanzibar limewakamata watuhumiwa
wemgine watatu wakiwemo Maafisa wawili wa Mamlaka ya Mapato nchini
TRA kituo cha Bandari Zanzibar kwa kuhusika na kashfa ya kupatikana
kwa meno ya tembo yenye thamani ya Mabilioni ya shilingi.
Kamishna
wa Polisi Zanzibar CP Mussa Ali Mussa, amewataja Maafisa hao wa TRA
waliokamatwa kuwa ni Omari Hamad Ali(50) na Mohammed Hija(48) ambao
wote wanafanyia kazi katika Bandari ya Zanzibar. Mtuhumiwa mwingine
ni kibarua wa Mamlaka ya bandari Zanzibar Haidar Ahmad Abdallah(54).
Kukamatwa
kwa watuhumiwa hao kunaifanya idadi ya watuhumiwa waliokamatwa hadi
sasa kwa kuhusika na sakata hilo kufikia watano.
Kamishna
Mussa amesema Watuhumiwa wengine wawili ambao ni wafanyakazi wa
Kampuni ya Uwakala wa Mizigo ya Island Sea Food Limited, Mohammed
Suleiman Mussa(45) na Juma Ali Makame(34) wao walikamatwa siku ya
tukio la kukamatwa kwa meno hayo ya tembo kwenye Bandari ya Zanzibar.
Tayari
watuhumiwa hao wamesafirishwa kwenda Makao Makuu ya Polisi Dar es
Salaam kwa ajili ya mahojiano zaidi.Pamoja na mambo mengine,
kusafirishwa kwa watuhumiwa hao kwenda Jijini Dar es Salaam,
kunatokana na Zanzibar kutokuwa na Sheria maalumu inayohusu
wanyamapori.
Maafisa
wa Idara ya Wanyamapori nchini, leo wamekamilisha kazi ya kuhesabu
na kulinganisha vipande 1,023 vya meno ya tembo vilivyokamatwa jana
kwenye Bandari ya Zanzibar na kubaini idadi ya tembo waliouawa kuwa
ni 305.
Meno
hao yenye uzito wa kilo 2,915 yenye thamani ya Dolla
4,775,000 sawa na shilingi 7,480,125,000 za Tanzania (Bil.7.4),
yalikamatwa juzi yakiwa yamehifadhiwa katika magunia 98 na kuwekwa
kwenye konteina moja la futi 40 lenye namba PCIU 857619/0 lillilokuwa
tayari kupakiwa kwenye meli ya MV Kota Henning kupelekwa nchini
Ufilipino kwa magendo.
Hadi
sasa bado Makachero wa Polisi wa Kimataifa Interpol hapa nchini kwa
kushirikiana na Makachero wa Polisi Zanzibar, idara ya wanyamapori
makao makuu wanaendelea na upelelezi wa kuwabaini wale wote
waliohusika na kashfa hiyo.
Jana
Kamishna wa Polisi Zanzibar CP Mussa Ali Mussa, alisema kuwa kazi
kubwa iliyobaki ni kuhakikisha kuwa upelelezi wa kina unafanyika ili
kuwakamata wale wote wanaohusika na mtandao huo.
Alisema
hadi sasa Jeshi la Polisi bado linamsaka tajiri aliyewezesha mipango
ya kukusanywa na kusafirisha shehena hiyo kutoka Tanzania Bara hadi
Zanzibar ili kusafirishwa nje ya nchi.