Polisi wafukuzwa kazi, ni baada ya kukutwa na jino la tembo

WATU watatu wakiwemo waliokuwa maaskari wa Jeshi la Polisi wilayani Serengeti katika mkoa wa Mara jana walifikishwa katika mahaka... thumbnail 1 summary
WATU watatu wakiwemo waliokuwa maaskari wa Jeshi la Polisi wilayani Serengeti katika mkoa wa Mara jana walifikishwa katika mahakama ya wilaya ya Bunda kujibu mashtaka ya kukutwa na jino moja la tembo, lenye thamani ya sh milioni 3, kinyume cha sheria.
Waliofikishwa katika mahakama hiyo iliyokuwa chini ya Hakimu Mkazi Mfawidhi  wa wilaya hiyo, Safina Semfukwe, ni John Sigita Masese (25) ambaye ni mkulima na mkazi wa eneo la Bomani mjini Mugumu, Sixberth Amos (35) na Isaac John Ackley (43) ambao wote walikuwa ni maaskari wa jeshi la polisi.
Awali ilidaiwa na mwanasheria wa hifadhi za taifa Serengeti (SENAPA), Emmanuel Zomba, kuwa Oktoba 25 mwaka huu, huko katika eneo la maktaba mjini Mugumu washtakiwa wote kwa pamoja  walikamatwa na askari wa idara ya wanyamapori wakiwa na jino moja la tembo lenye thamani tajwa na walikuwa wakilitafutia mteja.
Mwanasheria huyo aliiambia mahakama kuwa baada ya kukamatwa washtakiwa kwa pamoja walifikishwa katika kituo kikuu cha polisi cha mjini Mugumu ambapo maofisa hao wa polisi walishtakiwa kijeshi na kukutwa na hatia iliyosababisha wafukuzwe kazi mwishoni mwa wiki iliyopita na hivyo kushtakiwa katika mahakama za kiserikali.
Mbali na shtaka hilo, pia mshtakiwa Isaac John Ackley alikutwa na risasi moja ya bunduki ya SMG na nyingine tano zinazotumika kuwindia wanyama pamoja na nyama ya aina ya nyumbu, yenye thamani ya sh 1,040,000.
Washtakiwa kwa pamoja wamekana mashtaka na wako nje kwa dhamana hadi Novemba 18 mwaka huu kesi yao itakapotajwa tena mahakamani hapo.
 
Chano: Tanzania Daima