Usiku wa Khanga za Kale 2013 kupambwa na Mashauzi Classic

Na Andrew Chale   ONESHO  la  Usiku wa Khanga za Kale 2013, maarufu kama ‘5th Extra Vaa Khanga Party’ linatarajiwa kufanyika jijini... thumbnail 1 summary

Na Andrew Chale
 
ONESHO  la  Usiku wa Khanga za Kale 2013, maarufu kama ‘5th Extra Vaa Khanga Party’ linatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam usiku wa Novemba 8, kwenye Hoteli ya Serena na kupambwa na burudani ya nguvu kutoka kwa bendi ya Mashauzi Classic.

Mwandaaji wa onesho hilo, Asia Idarous Khamsin,  alisema jana tayari maandalizi yake yamekamilika na amewasihi wadau kujitokeza kwa wingi katika onesho hilo la aina yake kujionea mitindo mbalimbali ya khanga.

“Wadau wa mitindo nchini, watapata burudani na kufurahia mitindo ya khanga itakayooneshwa kwenye shoo hiyo, hii si ya kukosa kwa mwaka huu,” alisema Asia Idarous.

Alisema usiku huo, vazi la khanga  ndilo litakuwa maalumu  kwa wadau watakaohudhuria sambamba na kupinga matumizi ya dawa za kulevya.
Onesho la Usiku wa Khanga za Kale 2013, ambalo mwaka huu limeandaliwa kwa ushirikiano wa Asia Idarous Khamsin na Fabak Fashions, linatarajiwa kuwa na shangwe mbalimbali ikiwamo kushirikisha watu maarufu na mastaa mbalimbali.

Kuhusu kiingilio, Idarous alisema kwa viti vya kawaida ni sh 30,000 na viti maalumu itakuwa ni sh 50,000 na kuongeza kuwa tiketi zimeanza kuuzwa Fabak Fashions Mikocheni na Gift Shop Serena Hoteli.

Alisema onesho hilo linafanyika chini ya uwezeshaji wa wadhaminiwa kama bia ya Redd’s, CXC, Clouds FM, Vayle Spring, Magic FM, Eye View, Amina Design, Kabile, Voice of America, Origin Unite, Channel Ten, DTV, Times FM, Michuzi Media Group, Event Light na Miss Tz.