Inasemekana kila jina lina asili yake na maana pia.
Hata hilo jina lako ulipewa kwa sababu, na lina asili yake. Kama si la kutoka
katika Biblia ama Quran, basi ni la kimila lenye kumaanisha jambo, kama vile
siku, tukio, mahali ama hata shida au raha aliyopata mama wakati wa uzazi wako.
Jiji la Dar es salaam zamani
liliitwa Mzizima. Sultani Seyyid Majid wa Zanzibar ndiye aliyelipa jiji hili jina "Dar es
Salaam" linalotokana na lugha ya Kiarabu (Dār as-Salām) lenye
kumaanisha "nyumba ya amani." Maelezo yanayopatikana mara nyingi kuwa
maana ni "bandari ya salama" yachanganya maneno mawili yanayofanana
katika Kiarabu yaani "dar" (=nyumba) na "bandar"
(=bandari).
Dar es Salaam ilichaguliwa na wakoloni Wajerumani kuwa mji mkuu wa Afrika ya Mashariki ya Kijerumani kwa sababu ya bandari asilia yenye mdomo pana ya mto Kurasini. Kuanzia 1891 Dar es Salaam ilichukua
nafasi ya Bagamoyo kama makao makuu ya utawala. Bandari pamoja
na ujenzi wa reli ya kati kwenda Kigoma tangu 1904 ziliimarisha nafasi ya mji
ulioendelea kama mji mkuu baada ya Tanzania bara kuwa koloni ya Tanganyika chini ya Uingereza.
Bado kuna mabishano ya ni
nini hasa asili ya jina Africa. Wengine wanadai linatokana na neno la Kigiriki
la APHRIKE, lililomaanisha kusikokuwa na baridi, ama la Kilatini APRICA, lenye
kumaanisha nchi yenye jua daima.
Wengine wanasema neno "Afrika" limetokana na lugha ya Kilatini ya Waroma wa Kale. Waroma kwa jina hilo hawakumaanisha
bara lote bali eneo katika jimbo la Carthage ama Tunisia ya leo tu. Asili yake ni kabila la
"Afrig" lililoishi sehemu zile.
Wakati huo Wagiriki wa Kale walitumia zaidi jina la Libya kwa ajili ya nchi kusini ya Bahari ya Mediteraneo.
Maeneo ya ndani kuelekea kusini mara nyingi yaliitwa kwa jina la
"Ethiopia" linalomaanisha nchi ya watu weusiweusi (kwa Kigiriki "aithiops": aliyechomwa na jua).
Katika ramani za kale kutoka Ulaya maneno yote matatu ya
"Afrika", "Lybia" na "Ethiopia" yanapatikana
yakitumika kama jina la bara. Jina la "Afrika" limekuwa kawaida
kuanzia karne ya 16 BK.
Misri ya wakati huo ilikuwa
inachukuliwa kama sehemu ya bara la Asia,na alikuwa Mwanajiografia aitwaye
Ptolemy (85-165A AD) ambaye aliigawa Afrika na Asia na Ulaya kwa kuchora ramani
inayoonesha Suez na Bahari Nyekundu kuwa ndio mpaka baina ya Asia na Afrika.