ForumCC: Mafuriko Dar es Salaam ni ushahidi wa athari za mabadiliko ya tabianchi

Mvua zinazoendelea kunyesha nakusababisha mafuriko na hasara kubwa jijini Dar es Salaam na maeneo mengine nchini zimetajwa kuwa ni moja... thumbnail 1 summary
Mvua zinazoendelea kunyesha nakusababisha mafuriko na hasara kubwa jijini Dar es Salaam na maeneo mengine nchini zimetajwa kuwa ni moja ya ushahidi wa udhaifu wa miundombinu ya kweza kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo ni janga kubwa duniani kwa sasa. Haya yalisemwa na FORUMCC; shirika linalijihusisha na masuala ya mabadiliko ya Tabianchi.

Watu zaidi ya 12 wameripotiwa kupoteza maisha mpaka sasa kutokana mafururiko hayo ambayo yameibua hisia na maswali mengi kutoka kwa wananchi na wadau mbalimbali wa mazingira wengi wakihoji nani wa kulaumiwa kutokana na mafuriko hayo.

Afisa Miradi, Fazal Issa kutoka shirika la ForumCC ameitaka serikali na watu binafsi kuchukua hatua thabiti katika kukabiliana na mafuriko haya ambayo yanasababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Alisema kuwa serikali na taasisi zake imekuwa na kawaida ya kuchukua hatua mara baada ya madhara kutokea badala ya kuweka mikakati ya muda mrefu ya kukabiliana na viashiria vya athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Taasisi zenye majuku ya kutoa tahadhari na kushughulikia majanga hasa ya mafuriko, mamlaka zinazohusika na ujenzi wa miundombinu katika jiji la Dar es Salaam, ukusanyaji na utoaji wa taka zinapaswa kufanyakazi kwa kushirikiana ili kutafuta suluhisho la kukomesha maafa haya kabla hayajaleta athari kwa watu” alisema Issa.

Alisema hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwani utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini unaonyesha kuwa mvua kubwa zitaendelea kunyesha hadi Mei 20 mwaka huu, hivyo kuwataka wananchi kutotupa taka hovyo na kufanyia usafi mifereji katika maeneo yao.

“Badala ya kulalamika na kuhoji nani wa kulaumiwa kutokana na mafuriko yanayojirudia jiji la Dar es Salaam, ni jambo la busara sasa kwa kila mwananchi kuwajibika katika nafasi yake katika kuzuia au kupunguza kutokea kwa mafuriko hayo” alisema Issa.  

Kwa upande wake Afisa Habari wa ForumCC, Tajiel Urioh Aliwataka Watanzania kutambua kuwa mvua na mafuriko makubwa yanayoendelea kutokea Dar es salaam na maeneo mengine yanamahusiano mkubwa na ongezeko la Joto duniani.

“Watu wanapuuza na kuchukulia mzaha mabadiliko ya tabianchi lakini wanapaswa kujifunza kutokana na mafuriko haya ambayo mbali na kusababisha vifo pia yameharibu miundombinu ya barabara, nyumba, madaraja” alisema Urioh 

Tafiti zinaonyesha kuwa joto limeongezeka kwa 0.850C duniani huku kwa Tanzania Joto likiongezeka kwa 10C tangu mwaka 1961 jambo ambalo linasababisha baadhi ya maeneo kupata mvua zinazozidi kiwango na kuwa na majanga kama vile mafuriko, vimbunga na ukame. 

Hata hivyo, repoti ya Jopo la wanasayansi duniani (IPCC 2007) inaonyesha, ili kukabiliana na uharibifu unaosababishwa na mafuriko, inategemea sana na mipango thabiti ya mipango miji, jinsi ya kutumia ardhi, ubora wa kuweza kutabiri kutokea kwa mafuriko, utoaji taarifa na jinsi ya kuchukua hatua.

Mafuriko ya namna hii yaliyoleta athari kubwa ni yale yaliyotokea mwaka 2011 katika Jiji la Dar es Salaam na kusababisha vifo vya watu  arobaini (40) huku yakiharibu vibaya miundo mbinu ya barabara, madaraja na makzi ya watu.