Nchi za bara la Afrika zatakiwa kuungana kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

By Sadiq Kisimikwe Nchi za kiafrika zimeaswa kuungana katika mapambano ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa sababu wao ni wahang... thumbnail 1 summary
By Sadiq Kisimikwe

Nchi za kiafrika zimeaswa kuungana katika mapambano ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa sababu wao ni wahanga na waathirika wa kwanza wa mabadiliko ya tabianchi duniani .

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira Dkt. Benelith Mahenge wakati akifungua mkutano wa vyama vya kiraia vinavyopambana na mabadiliko ya tabia nchi ukanda wa Afrika Mashariki(East Africa Civil Society Conference on Climate Change Adaptation) ulioitishwa na wenyeji Forum CC kwa kushirikiana na PACJA kutoka Kenya na AFCN  Kunduchi  jijini  Dar es salaam .

Akiongea katika mkutano huo Dtk.  Mahenge amesema hatua za haraka za makabiliano ya tabianchi lazima zichukuliwe  kutoka ngazi ya chini ya nchi hadi kimataifa ili kuzuia na kulinda usalama wa dunia kwa vizazi vijavyo.

“ni kweli  nchi za Afrika Mashariki tayari tumechukua hatua nzuri ya kuwa na mipango ya mabadiliko ya tabianchi lakini haitoshi kuwa na mipiango bila utekelezaji”amesema Mahenge

Kuna changamoto nyingi zinazotukabili kama Afrika juu ya mabadiliko ya tabianchi kama ukosefu wa fedha katika kukabiliana huko. Nchi wachafuzi wa Ulaya ambao asilimia 97 ndio waharibifu  kutokana na kuwa na viwanda vikubwa vinavyotoa hali joto duniani. Bado hazijakubali kufadhili na kutoa pesa kwa nchi zilizoathirika hasa Afrika na nchi za bara la Asia.

“Bado hatujafanya tafiti za kutosha kubaini ukubwa wa tatizo la mabadiliko ya tabia nchi hasa kwetu ukanda huu wa Afrika Mashariki, hi yote inatokana na kutokuwa na bajeti ya kutosha katika nchi zetu za Afrika. ”Anasema Mahenge

Mwisho Waziri huyo wa mazingira amesema elimu ni muhimu katika mabadiliko ya tabianchi  bado nchi za Afrika Mashariki hazijatoa elimu ya kutosha kwa wananchi wake.  Watu wetu wanaendelea kukata miti hovyo, wanalima hadi katika vyanzo vya maji, ukame umeongezeka , hamna chakula cha kutosha, tunabakisha majangwa bila kuwa na juhudi za upandaji miti.

Amewaomba washiriki wa kongamano hili kuzichukulia changamoto za mabadiliko ya tabianchi kama njia  ama chanzo cha kupigana dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kuwa na suluhisho mbadala bila kusubiri wafadhili na wahisani wa nchi za Ulaya.

Mkutano huo uliodumu kwa siku mbili ulishuhudia vyama kutoka ukanda wa Afrika Mashariki vikizindua umoja wao wa kushirikiana katika mapambano ya mabadiliko ya tabianchi ikishirikisha washiriki kutoka Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi ,na wenyeji Tanzania.