Washiriki
kutoka kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani Arumeru mkoani
Arusha, wakiwa katika picha ya pamoja na Mratibu mradi kitaifa wa
Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya
mapema nchini, Alfei Daniel (wa kwanza kushoto) mara baada ya kufunga
mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo, tarehe 13 Juni, 2015
Ofisi
ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu Maafa kupitia mradi wa kuimarisha
mifumo ya habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari nchini imezitaka
serikali za mitaa na vijiji nchini kuhusisha maafa yatokanayo na
mabadiliko ya tabianchi na mipango yao ya maendeleo, ili kuhakikisha
jamii inakuwa na uchumi bora na uwezo wa kupunguza athari za Maafa hayo.
Akizungumza
wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati ya Maafa wa
Kata ya Makiba Wilayani Arumeru, mkoani Arusha, uliofanyika hivi
karibuni, Mratibu Mradi huo Kitaifa, Alfei Daniel alieleza kuwa,
serikali za vijiji zitumie taarifa za athari za mabadiliko ya tabianchi
za vijiji vyao ambazo zitakuwa zinaainishwa kupitia mradi huo kama
sehemu ya kuandaa mipango mikakati ya maendeleo vijijini.
“Kupitia
mradi huu tutakuwa tunatoa taarifa za hali ya hewa kwa eneo husika na
kwa wakati, Ufahamu juu ya Hali ya hewa, mabadiliko ya tabianchi, maji
na mazingira ni muhimu sana na ni kiungo kikubwa katika kuandaa mikakati
na mipango ya maendeleo vijijini, hii itasaidia kuimarisha uwezo wa
serikali za vijiji kuwalinda wananchi kwa athari zinazoweza kusababishwa
na mabadiliko ya tabianchi” alisisitiza Daniel.
Aliongeza
kuwa uwepo wa miundombinu hafifu vijijini, upungufu wa wataalamu wa
masuala ya hali ya hewa pamoja na taarifa za hali ya hewa kutowafikia
wanavijiji kwa wakati, kumekuwepo na matumizi madogo ya taarifa za hali
ya hewa kitendo ambacho huziweka jamii za vijijini katika mazingira
magumu hasa kwenye shughuli za kiuchumi pindi yanapotokea maafa ya
mabadiliko ya tabianchi kama ukame na mafuriko.
Kwa
upande wake, Diwani wa Kata Makiba, Mwanaidi Kim alifafanua kuwa ni
muhimu vijiji kuhusisha maafa yatokanayo na maafa ya mabadiliko ya
tabianchi katika mipango ya maendeleo kwani athari zake zinapotokea
shughuli za maendeleo hukwama.
“Katika
kata yangu kuna vijiji sita ambavyo ni; Makiba, Patanumbe, Valesika,
Engatani na Kaloleni, lakini katika vijiji hivi vyote kuna ishara ya
upungufu wa chakula, Hivyo kama mtu hana chakula ni vigumu kufanya
shughuli za maendeleo lakini kupitia mradi huu athari hizi hazitatupata
tena kwani tutakuwa tunapata taarifa za hali ya hewa kwa wakati na sisi
tunapanga vizuri mipango yetu ya kimaendeleo” alisema Mradi huo ambao
utatekelezwa nchi nzima, kwa sasa unatekelezwa kwa majaribio tangu mwaka
2014 hadi 2018 katika Halmashauri ya wilaya ya Meru, Mkoani Arusha na
Halmashauri ya wilaya ya Liwale, mkoani Lindi.
Mratibu
mradi kitaifa wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya
tahadhari ya mapema nchini, Alfei Daniel akifafanua jambo wakati wa
mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo kwa wajumbe wa kamati za maafa za
kata ya Makiba, Wilayani Arumeru mkoani Arusha, wengine ni wawezeshaji
wa mafunzo hayo.
Mshiriki wa
Mafunzo ya utekelezaji mradi wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya
hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini akichangia wakati wa
mafunzo hayo kwa wajumbe wa kamati za maafa za kata ya Makiba, wilayani
Arumeru mkoani Arusha, mafunzo hayo yameratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu
kupitia mradi huo , hivi karibuni.
Washiriki wakiwa katika warsha hiyo..