Serikali za Vijiji zatakiwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabianchi wakati wa kupanga mipango yao ya maendeleo

Washiriki kutoka kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani  Arumeru mkoani Arusha, wakiwa katika picha ya pamoja na Mratibu mradi ... thumbnail 1 summary
PICHA NO. 4
Washiriki kutoka kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani  Arumeru mkoani Arusha, wakiwa katika picha ya pamoja na Mratibu mradi kitaifa wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini, Alfei Daniel (wa kwanza kushoto) mara baada ya kufunga mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo, tarehe 13 Juni, 2015

Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu Maafa kupitia mradi wa kuimarisha mifumo ya habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari nchini imezitaka serikali za mitaa na vijiji nchini kuhusisha maafa yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi na mipango yao ya maendeleo, ili kuhakikisha jamii inakuwa na uchumi bora na uwezo wa kupunguza athari za Maafa hayo.

Akizungumza  wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati ya Maafa wa Kata ya Makiba Wilayani Arumeru, mkoani Arusha, uliofanyika hivi karibuni, Mratibu Mradi huo Kitaifa, Alfei Daniel alieleza kuwa, serikali za vijiji zitumie taarifa za athari za mabadiliko ya tabianchi za vijiji vyao ambazo zitakuwa zinaainishwa kupitia mradi huo kama sehemu ya kuandaa mipango mikakati ya maendeleo vijijini.

“Kupitia mradi huu tutakuwa tunatoa taarifa za hali ya hewa kwa eneo husika na kwa wakati, Ufahamu juu ya Hali ya hewa, mabadiliko ya tabianchi, maji na mazingira ni muhimu sana na ni kiungo kikubwa katika kuandaa mikakati na mipango ya maendeleo vijijini, hii itasaidia kuimarisha uwezo wa serikali za vijiji kuwalinda wananchi kwa athari zinazoweza kusababishwa na mabadiliko ya tabianchi” alisisitiza Daniel.

 Aliongeza kuwa uwepo wa miundombinu hafifu vijijini, upungufu wa wataalamu wa masuala ya hali ya hewa pamoja na taarifa za hali ya hewa kutowafikia wanavijiji kwa wakati, kumekuwepo na matumizi madogo ya taarifa za hali ya hewa kitendo ambacho huziweka jamii za vijijini katika mazingira magumu hasa kwenye shughuli za kiuchumi pindi yanapotokea maafa ya mabadiliko ya tabianchi kama ukame na mafuriko.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata Makiba, Mwanaidi Kim alifafanua kuwa ni muhimu vijiji kuhusisha maafa yatokanayo na maafa ya mabadiliko ya tabianchi katika mipango ya maendeleo kwani athari zake zinapotokea shughuli za maendeleo hukwama.

“Katika kata yangu kuna vijiji sita ambavyo ni; Makiba, Patanumbe, Valesika, Engatani na Kaloleni, lakini katika vijiji hivi vyote kuna ishara ya upungufu wa chakula, Hivyo kama mtu hana chakula ni vigumu kufanya shughuli za maendeleo lakini kupitia mradi huu athari hizi hazitatupata tena kwani tutakuwa tunapata taarifa za hali ya hewa kwa wakati na sisi tunapanga vizuri mipango yetu ya kimaendeleo” alisema Mradi huo ambao utatekelezwa nchi nzima, kwa sasa unatekelezwa kwa majaribio tangu mwaka 2014 hadi 2018 katika Halmashauri ya wilaya ya Meru, Mkoani Arusha na Halmashauri ya wilaya ya Liwale, mkoani Lindi.
PICHA NO. 2
Mratibu mradi kitaifa wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini, Alfei Daniel akifafanua jambo wakati wa mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo kwa wajumbe wa  kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani Arumeru mkoani Arusha, wengine ni wawezeshaji wa mafunzo hayo.
PICHA NO. 1
Mshiriki wa Mafunzo  ya  utekelezaji mradi wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini akichangia wakati wa mafunzo hayo kwa wajumbe wa kamati za maafa za kata ya Makiba, wilayani Arumeru mkoani Arusha, mafunzo hayo yameratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia mradi huo , hivi karibuni.
PICHA NO. 3
Washiriki wakiwa katika warsha hiyo..