RoadToParis2015
with Tabianchiblog&CFIMedias21
Dotto
Kahindi
Nimekuandalia
mbinu 20 za namna bora ya kuandika habari za mabadiliko ya tabianchi. Mbinu
hizi zimetokana na maoni yangu binafsi ambayo yamepitiwa na Mhariri wa jarida la
Mtandaoni la Indian Ocean na Mchambuzi wa mambo ya mazingira katika ukanda wa
bahari nchini Kenya, Wanjohi Kabukuru, naamini yatakuwa yenye msaada mkubwa
kwako.
1.Ijue hadhira yako, unapoketi
kuandika habari yako kuna mtu mmoja tu unayetakiwa kumfikiria, mtu huyu siyo
wewe wala mhariri wako, bali ni msomaji ama msikilizaji wa habari yako. Ni
muhimu sana kujua hadhira yako ni nani na pengine aina ya uelewa wao juu ya
jambo unaloliandika, usitumie maneno ya kisayansi wakati unayemwandikia ni mtu
wa darasa la saba.
2.Ielewe mada, kama
utakaa kuandika mada ya mazingira ambayo huna uelewa nayo, usitegemee msomaji
wako ataielewa. Fanya utafiti wa kutosha kuweza kujipatia ufahamu wa kutosha wa
mada yako, iwe kwa kusoma majarida au kuzungumza na wadau wenye uzoefu wa eneo
hilo. Lakini bila hivyo ni sawa na kupaka rangi upepo, utakuwa unaandika madudu
ambayo yatakufanya uonekana hauna maana mbele za watu. Ni sawasawa na kupika
chakula, usipike chakula kibaya ambacho hata wewe mwenyewe huwezi kukila.
3.Jiielimishe, soma
majarida mbalimbali ya sayansi na mazingira, ili kujijengea uwanda mpana na
uelewa kwa manufaa yako. Kuandika habari za mabadiliko ya tabianchi ni muhumu
kuelewa masuala ya kijamii, kisiasa na kisayansi, usibaki kuandika habari za
mabadiliko ya tabianchi ni hatari, hakuna mtu anapenda kutishwa bila kuonyeshwa
ukweli wa mambo. Jichanganye na watu mbalimbali, kama wanasayansi, wanasiasa na
jamii ili kujua mambo mengi zaidi nje ya hapo. Waandishi wengi wa habari za
mazingira wanadhani kujitenga na jamii na wanasiasa ni jambo jema, la hasha ni
lazima kujua hakuna mabadiliko ya tabianchi bila siasa wala jamii.
4.Chagua mada, pamoja na
kwamba hali ya uandishi wa habari kwenye nchi nyingi bado hairuhusu mtu
kuchagua mchepua Fulani tu wa habari, lakini bado unanafasi ya kuamua kufanya
mada Fulani au aina Fulani ya habari. Lakini uamuzi huu usukumwe na motisha
yako, elimu yako na hata mazingira unayofanyia kazi, usilazimishe kufanya
habari ambazo huna mapenzi nazo
5.Simama kwenye lengo, baadhi ya
waandishi hupenda kuonekana wanajua mambo mengi sana hivyo kuandika habari
ambazo zimejaa maelezo mengiiii wakidhani huo ndio uhodari. Hapana, hata waswahili
husema miluzi mingi humpoteza mbwa, jaribu kuchukua mada moja na ieleze kwa
unagaubaga kiasi kwamba msomaji anaweza kuielewa vyema, usichanganye mada,
nisawa na kuchanganya mlenda na pilau, unaweza kutengeneza sumu
6.Misamiati, hakikisha
unatoa ufafanuzi wa kila msamiati au neno gumu, ikiwezekana achana nayo kabisa
maana yataweza kumchanganya msomaji. Maneno kama REDD, INDCs, UNFCCC, COP ni
vyema ukayawekea ufafanuzi wake ili msomaji aweze kuelewa. Utaratibu huu uanzie
kwa mtu unayemfanyia mahojiano yaani chanzo cha habari yako, hakikisha unakuwa
na ufafanuzi wa kila neno gumu ili uwe na uwanda mpana wa kujimwaga kuandika
habari yako
7.Kwa ufupi, waluguru
wanasema Keep it Short and Simple, yaani usiandike lihabari lireeeeefu mpaka
msomaji anaanza kutokwa na jasho, tumia maneno mafupi, mepesi na yanayoeleweka,
nakwambia hakuna mtu atakuja kulalamika eti kwamba habari zako zinaeleweka sana
kwa watu.
8.Ungana na wenzako, siku zote
kidole kimoja hakivunji chawa. Jitahidi kuungana na vyama vya waandishi wa
habari za mazingira, kwa Tanzania kuna Chama cha Waandishi wa Habari za
Mazingira (JET), pia kuna Mtandao wa Bloggers wa Mabadiliko ya Tabianchi (BNCC)
ambao umeanzishwa hivi karibuni, ungana nao. Huko utapata taarifa, uzoefu na
utaweza kushiriki pia katika warsha mbalimbali zitakazokuongezea uelewa wa
mambo.
Jiunge na
mitandao ya kimataifa pia, kuna tovuti nyingi tu za mabadiliko ya tabianchi,
tumia mitandao kama google kutafuta na ujiunge nao ili uweze kupokea taarifa
mbalimbali kwa email zinazoweza kukusaidia kuwa na ufahamu ya mambo mengi
9.Nenda kibiashara, moja ya
sababu kubwa ya waandishi wengi kukwepa kuandika habari za mabadiliko ya
tabianchi ni kipato. Kumbuka ili wazo lako la habari likubalike kwa mhariri
lazima liwe na mwelekeo wa utofauti ambao utasaidia gazeti kuuza. Tumie mada
kama za uchumi, kilimo, biashara nk kama sehemu moja ya wazo lako la habari,
usiishie tu kusema nakwenda kutafuta habari ya mabadiliko ya tabianchi, hapana,
ila italeta maana kama utasema natafuta habari ya mabadiliko ya tabianchi
yanavyochangia kupanda kwa bei ya samaki. Hii italeta uzito kidogo
10.Vaa miwani ya mabadiliko ya
tabianchi, kila tukio linapotokea, liangalie kwa kutumia miwani hiyo, iwe
ni uchaguzi, elimu, njaa, mafuriko, harusi nk fikiria ni kwa namna gani mambo
hayo yanaweza kuathiri au kuathiriwa na mabadiliko ya tabianchi. Hata hivyo
usiangalie mambo hasi tu, angalia pia na mambo chanya
Kumbuka neno
mabadiliko ya tabianchi sio lazima yawe kwenye stori yako, Habari ya mabadiliko
ya tabianchi itajulikana tu hata kama hutataja neno mabadiliko ya tabianchi
kwenye habari yako, kwa mfano ukiandika habari kama hii, ‘Ng’ombe 20 wamekufa
kutokana na ukame’, inafahamika ukame unasababishwa na nini na ni rahisi watu
kuelewa uhuasiano wa tukio kama hilo na mabadiliko ya tabianchi
11.Tumia lugha ya picha, habari
nyingi za mabadiliko ya tabianchi ni ngumu kuzielezea, ukikutana na hali hii,
inashauriwa kutumia picha kama njia moja wapo ya kuonyesha hali halisi na
kumfanya mtu aelewe zaidi. Wanasema picha husema maneno zaidi ya elfu moja
12.Weka utu na ubinadamu mbele, watu wengi
hujali zaidi mambo yanayogusa maisha yao, familia zao, afya zao na mali zao.
Mabadiliko ya tabianchi yanagusa maeneo hayo yote pia kwahiyo wakati unaandika
habari yako jaribu kufikiria watu na vitu wanavyovijali. Gusa imani zao, maisha
yao, tamaduni zao na hata mazingira yao na utaweza kukubalika katika jamii hiyo
13. Jiandae vyema kwa mahojiano, Kadri
unavyojua mengi kuhusu mada na mtu unayekwenda kufanya nae mahojiano ndivyo
utakavyokuwa na nafasi nzuri ya kupata maelezo stahiki. Usifike kwenye
mahojiano halafu unaanza kumangamanga hata hujui wapi pa kuanzia, kuna watu
wanakwenda kufanya mahojiano hawajua hata majina ya wanaokwenda kuwahoji, hili
liepuke na ujiandae mapema kwa mahojiano yenye mafanikio. Pia eleza mahojiano
hayo unakwenda kuyatumia wapi, nani ni hadhira yako, hii itampa nafasi
unayemhoji kutoa maelezo ambayo yanaeleweka pia kwa aina ya hadhira yako.
14.Tafuta mbadala, wakati
mwingine tunapofanya mahojiano na vyanzo vetu vya habari tunaweza kujikuta
katika hali ya njia panda, unaweza kupata taarifa ambayo sio sahihi na kwakuwa
umepewa au imetolewa na mtu mwenye nafasi au mwanasayansi basi ukadhani iko
sahihi na ukaiandika kama ilivyo. Hapana, hii sio njia sahihi, jitahidi
kuzungumza na mtu mwingine mwenye hadhi kama hiyo ili kupata picha nyingine.
Mtu wa kwanza anaweza kuwa amekupatia taarifa yenye upendeleo ama isiyokuwa na
ukweli, basi zungumza na watu wengine zaidi kwa uhakika na weledi.
15.Ukweli, baada ya
kusema hapo juu haimaanishi sasa kila unapofanya mahojiano unachoambiwa ni
uongo, la hasha, bali sikiliza maneno ya chanzo chako na ili kuhakikisha
kinachosemwa ni kweli basi omba uthibitisho, kama anazungumzia takwimu, mwambie
akupatie, kama anazungumzia idadi mwambie akupatia, na kama anazungumzie eneo
mwambie akupatia uthibitisho huo. Kwa kufanya hivyo utaweza kubaini na
kujiridhisha juu ya anachokizungumza. Siku zote njia ya mwongo ni fupi kama
atakuwa anapika takwimu itakuwa rahisi sana kumbamba.
16.Nukuu, katika
kufanya ripoti yako jitahidi kuweka nukuu za kila aina, washirikishe watu wa
jinsia zote, marika yote ili kunena na kuongeza nguvu ya taarifa yako, lakini
ni vyema kuzingatia nani ni muhimu kusema kitu ambacho kitaongeza uzito kwenye
habari yako, kuna makundi muhimu ambayo ni vizuri kuyaangalia, hii ni pamoja na
watoto, wanawake, walemavu, wazee na hata vijana. Hawa ukizungumza nao watakupa
majibu yatakayokuongezea nyama kwenye habari yako, zungumza na watu wengi kadri
uwezavyo kuweza kujipatia uelewa wa kutosha
17.Ukaribu na uhalisia, habari
nyingi kutoka kwenye mikutano ya kimataifa, ya wanasayansi inaongelea zaidi
mambo ya mabadiliko ya tabianchi kimataifa zaidi, tumia taarifa hizo kwa
kuzihusisha na matukio ya nyumbani, kwa kutumia mifano iliyopo nyumbani ili
kuweka uhalisia na ukaribu wa tukio lenyewe. Angalia ni jambo gani linahusiasa
na mada Fulani iliyowasilishwa ambalo watu wa nyumbani wakilisikia wanaweza
kuguswa na habari yako
18.Usilemazwe na taarifa za
habari (press release), mara nyingi waandishi wa habari wanapenda
ku-copy na ku-paste taarifa za habari na kuweka majina yao tu kisha kuwasilisha
stori zao wakijiona ni wajanja kwelikweli, sawa utalipwa kwa habari yako
kutoka, lakini itakuwa ni habari yenye ukakasi isiyovutia msomaji. Ukweli ni
kwamba press release sio habari, ni mfupa tu ambao unahitaji ubunifu wa
mwandishi kuuongezea nyama. Kwahiyo unatakiwa kuifanyia kazi zaidi ili kuwagusa
wasomaji wako.
19.Kuwa mfuatiliaji na mdadisi, fuatilia
kazi za waandishi wengine ili kujifunza wanavyoandika, unaweza kubaini mazuri
na hata mabaya kutoka kwenye kazi zao, unaweza kupata habari nyingi za namna
hiyo kwenye magazeti, blogs hasa kwenye blog hii ya tabianchi. Huwezi kujua
kuandika vizuri kama hauna tabia ya kusoma kazi za wengine.
20.Fuata pesa zilipo, Kama
hukujua, mabadiliko ya tabianchi ni stori zenye mamilioni ya pesa, kuna pesa
nyingi kwenye eneo hili, pesa za kuzuia na kupambana na mabadiliko ya tabianchi
zipo kwa wingi, lakini ni lazima ujue zilipo, nani anazipokea nani anazitumia,
nani anahakikisha zinatumika ipasavyo, nani anatoa ufadhili kwa NGOs na hata
wanasiasa. Fuatilia mambo haya utakuta umepata habari nzuri na nyingi
zitakazokulipa hata wewe pia. Ukifuata nyuki utapata asali.
Ni hayo
machache nimefanikiwa kukuletea, kama kuna mbinu nyingine sijaziweka,
unakaribishwa kuchangia ili kuboresha zaidi kilichopo.