Tanzania: Hatutakubali nchi nyingine kuingilia mipango yatu ya uchimbaji wa mafuta na gesi

Dotto Kahindi RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21 Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya makamu wa Rais imesema kuwa hai... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi
RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21
Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya makamu wa Rais imesema kuwa haitakuwa tayari kuona nchi zinazoendelea zikiingilia na kukwamisha mipango ya maendeleo ya uchimbaji wa gesi na mafuta kwa kigezo cha uchafuzi wa mazingira.

Msimamizi wa mchakato wa kuandaa mchango wa kila nchi katika juhudi za dunia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Intended Nationally Determined Contributions – INDCs), nchini Tanzania ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Dk Richard Muyungi anasema hategemei mataifa yaliyoendelea kuitumia INDCs kukwaza maendeleo kwa nchi zinazoendelea

“Siamini wala sitegemei wahisani wa maendeleo watatumia INDCs kama kigezo cha kutupa au kutunyima misaada katika maeneo ambayo yatakuwa hayamo kwenye mchango wetu” anasema Dk Muyungi.

Nchi zinazoendelea zimekuwa na wasiwasi kuwa, INDCs ni mtego utakaotumika kama kikwazo cha maendeleo ya kiuchumi kwa nchi hizo jambo ambalo Tanzania haitakuwa tayari kukubaliana na hoja hiyo.

Anasema kama mataifa yaliyoendelea na nchi wahisani hawatasaidia nchi katika maeneo ambayo hayakutajwa kwenye INDCS, hilo halitakuwa jambo la kiungwana kwa sabababu maeneo ya uchangiaji ni maeneo ya hiyari na sio ya lazima. 

Mapema mwezi uliopita Makamu wa Rais Benki ya Dunia (WB) na Mjumbe Maalumu wa Mabadiliko ya Tabianchi Rachel Kyte alisema benki ya dunia itatumia INDCs kama kigezo kimoja wapo wakati wa kutoa misaada ya kimaendeleo kwa nchi wanachama.

“Sisi benki ya dunia tunavutiwa na INDCs kwa sababu kwazo tunaweza kuona mahitaji ya nchi husika na hapo tunaweza kusaidia maeneo hayo, kwahiyo kupitia hizi INDCs tunahitaji kujua maeneo gani nchi imeyapa kipaumbele yenye fursa za maendeleo ya kiuchumi”

Akizungumzia uchimbaji wa gesi na mafuta kwa Tanzania kama unaweza kuwa kikwazo cha utekelezaji wa INDCs Muyungi anasema kuwa matumizi ya rasilimali hizo hayaepukiki kwakuwa ni muhimu katika maendeleo ya nchi.

“Kwasababu mafuta na gesi tumeshavipata ni lazima tuvitumie, ni lazima tuchimbe, matumizi ya nishati mbadala ni muhimu lakini kama nchi tatizo tulilonalo ni uhaba wa fedha za kuweza kuitumia njia hiyo ambayo ni ghali sana” anasema Muyungi.

Anasema Tanzania itawasilisha INDCs ambayo itachangia kupunguza uzalishaji hewa joto kwenye sekta za kilimo, mifugo, maji, bahari, misitu na uchukuzi huku ikisisitiza katika kutumia mafuta na gesi ili kupata maendeleo kiuchumi.

“Mchakato  huu ni wa kitaifa, hatukubali usimamiwe na mgeni au mtu asiyejua mahitaji halisia ya nchi, hatutaki kukurupuka, tunataka kuandaa kitu ambacho hakitaturudisha nyuma kimaendeleo”.

Afisa Miradi shirika linalojihusisha na masuala ya mabadiliko ya Tabianchi ForumCC Tanzania Fazal Issa anasema nchi zote zilizoendelea kipindi wanavumbua mafuta walitumia njia za zamani za makaa ya mawe, gesi na mafuta na wakajipatia maendeleo waliyonayo.

Lakini leo hii nchi zote zinazoendelea hazitakiwi kutumia vyanzo hivyo vya nishati na badala yake zinatakiwa kutumia nishati mbadala ambayo ina gharama kubwa na Tanzania haina uwezo wa kuwekeza katika nishati hiyo.

“Ni bora tutumie hizi njia rahisi za makaa ya mawe, gesi na mafuta tukiwa na lengo la kuwekeza kwenye nishati mbadala hapo baadae, lakini tukisema tuingie moja kwa moja tuhamie kwenye gesi asilia itakuwa ni uongo, hatutaweza kwa sababu uwekezaji wake ni mkubwa mno” anasema Fazal

Anasema nchi zinazoendelea zingeweza tu kuhamia moja kwa moja kwenye uwekezaji wa nishati mbadala endapo nchi zilizoendelea zingeweka fedha za kusaidia uwekezaji huo jambo ambalo halifanyiki kwa sasa.

Historia ya gesi nchini
Shughuli za utafutaji mafuta na gesi asilia nchini Tanzania zilianza miaka ya 1950 kupitia Kampuni ya Agip kutoka Italia na ugunduzi wa kwanza katika Kisiwa cha Songo Songo (Lindi) mwaka 1974 ambao ulifuatiwa na ugunduzi mwingine katika eneo la Mnazi Bay (Mtwara) mwaka 1982.

Hata hivyo, gesi asilia hiyo haikuendelezwa kwa kuwa ilionekana haina manufaa ya kiuchumi (uneconomical) kwa wakati huo. Baada ya ugunduzi huo, TPDC iliendelea kufanya utafiti ikiwa ni pamoja na kuchimba Visima mbalimbali kwa ajili ya kuthibitisha kiasi cha gesi asilia kilichopo katika maeneo ambako gesi asilia iliyogunduliwa.

Utafiti wa mwisho ulikamilika mwaka 1991 ambapo mradi wa ujenzi wa mitambo ya kusafisha gesi asilia Kisiwani Songo Songo pamoja na Bomba la kusafirisha gesi asilia hiyo mpaka Dar es Salaam ulibuniwa na hadi Novemba, 2014 kiasi cha gesi asilia kilichogunduliwa nchini ni futi za ujazo trilioni 53.28 (53.28TCF)

Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli wa Wizara ya Nishati na Madini Injinia Hoseah Mbise mwaka 2013 alisema Serikali inakusudia kujenga kiwanda cha gesi kwa ajili ya mauzo ya nje (LNG=liquefied natural gas), ambapo kitaliwezesha taifa kuvuna mapato ya dola za Marekani milioni 200 (sh. bilioni 320) kwa mwaka.

Pamoja na kuwepo kwa fununua za nchi nyingi za jirani kutaka kununua gesi asilia ya Tanzania ni nchi ya Zambia ndio pekee iliyoomba kuuziwa gesi hiyo kwa madhumuni ya kuzalisha umeme na kupanua wigo wa uzalishaji wa viwandani.

Ombi hilo lilitolewa Jumatano, Februari 25, 2015 na Rais wa Zambia Edgar Chagwa Lungu kwa Rais wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete wakati wa mazungumzo rasmi kati ya nchi hizo mbili.

Msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini, Badra Masoud January 2015 akaweka bayana kuwa mradi mkubwa wa umeme wa gesi kupitia bomba kubwa kutoka Mtwara na Lindi hadi Kinyerezi jijini Dar es Salaam umekamilika na kwamba wananchi wameanza kunufaika.

 “Mradi huu utasaidia kuokoa sh.1.6 trilioni, zinazotumika kununulia mafuta ya kuzalishia umeme kwa sasa,” amesema.

Kwa mujibu wa Badra, umeme wa gesi una faida kubwa kwa wananchi wa hali ya chini kwa vile unapatikana kwa bei nafuu na hautegemei maji wala mabadiliko ya hali ya hewa kama umeme wa kawaida.

 “Kukamilika kwa mradi huu pia kutachochea matumizi ya gesi asilia majumbani, na katika shughuri za usafirishaji, hivyo kupunguza uchafuzi wa mazingira, matumizi ya mkaa na kuni nchini” anasema


Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Gesi Asilia ni Muhimu sana kwa Utekelezaji wa Dira yetu ya Maendeleo ya Mwaka 2025. Tanzania imeingia kwenye Uchumi wa Gesi Asilia na Miundombinu ya aina hii ya Uchumi lazima ijengwe.