Tanzania kuwasilisha INDCs mwezi Septemba

Dotto Kahindi RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21 Tanzania imesema itawasilisha mchango wake wa kila nchi katika juhudi z... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi
RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21
Tanzania imesema itawasilisha mchango wake wa kila nchi katika juhudi za dunia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Intended Nationally Determined Contributions – INDCs) katika wiki ya pili ya mwezi Septemba mwaka huu.

Msimamizi wa mchakato huo nchini Tanzania ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Dk Richard Muyungi amesema mchakato huo ambao ulianza tangu mwezi Januari mwaka huu uko katika hatua nzuri.

Moja ya mabasi ya mwendo kasi ambayo yanatajwa kuchangia kupunguza 
uzalishaji wa hewa ukaa
Ili kufanikisha mchakato huo Tanzania kama ilivyo kwa nchi nyingine zinazoendelea imepata msaada wa wataalamu wa kufanya uchambuzi yakinifu kutoka Serikali ya Ufaransa, na fedha kutoka GEF na UNDP kwa ajili ya kuwezesha shughuli nzima ikiwemo mijadala na wananchi na wadau mbalimbali wa mabadiliko ya tabianchi kutoka katika sekta tofauti.

Muyungi anasema “mchakato wa kuandaa INDCs ni lazima uwe wa kitaifa ili kupata maoni ya jamii hasa wale wanaohusika, kwa hiyo ni muhimu ukafanywa  kwa uangalifu pasipo kukurupuka na kujikuta tukiwasilisha mchango ambao utaturudisha nyuma kimaendeleo”

Anasema pamoja na kwamba INDCs kuwa ni jambo la hiari kwa nchi lakini maeneo ambayo yatatajwa kama muhimu itawalazimu kuyafanyia kazi, hivyo anaona ni muhimu kujua kama watakayoyawasilisha watakuwa na uwezo wa kuyasimamia na kuyatekeleza.

Maeneo muhimu kwa Tanzania
Muyingi anasema maeneo ambayo yanaweza kusaidia kukabiliana na kusaidia dunia katika kuhimili mabadiliko ya tabianchi ni pamoja na sekta ya kilimo, mifugo, maji, afya, nishati, uchukuzi, misitu na sekta ya masuala ya bahari.

“Tukipunguza athari za mabadiliko ya tabianchi kwenye sekta hizo, tunaamini tutakuwa tumechangia kuisadia dunia kuhimili mabadiliko ya tabianchi na wananchi watakuwa na maisha bora”

Muyungi anaamini kuwa INDCs zitachangia kupunguza matatizo ya migogoro ya ardhi ya wakulima na wafugaji inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na uhaba wa mvua na ufugaji usiokuwa na tija.


Anasema kupitia miradi ya gesi asilia, uchimbaji wa visima, uanzishwaji wa usafiri wa mabasi ya mwendo kasi na upatikanaji wa umeme vijini utapunguza matumizi ya kuni na mkaa na matumizi ya magari binafsi jijini Dar na hivyo kupunguza uazalishaji wa hewa ukaa.

“Mradi wa gesi asilia umeshakamilika, na mradi wa umeme vijini nao unakwenda vizuri hii itapunguza matumizi ya mkaa na kuni, lakini hata mradi wa mabasi ya mwendo kasi utapunguza msongamano wa magari barabarani, hiyo ni mipango ya kimaendeleo isiyo na madhara kimazingira” anasema Muyungi

Ushirikishwaji wadau
Pamoja na kwamba mchakato wa kuandaa INDCs umeshaanza lakini zoezi la kupata maoni kutoka kwa bado halijafanyika jambo ambalo linatia shaka kama kweli Tanzania itakuwa tayari kuwasilisha mchango wake ndani ya wakati.

“Sisi hatuna taarifa yeyote ya kuanza kwa mchakato wa kuandaa INDCs kwa Tanzania, kwa kifupi habari hii ndio kwanza nalisikia kutoka kwako na hatujashirikishwa hata kidogo” anasema Mwenyekiti wa Umoja wa Azaki za Kiraia za Mabadiliko ya Tabianchi Zanzibar (ZACCA) Ally Juma

Katika kutetea hoja hii Muyungi anakiri kuwa zoezi la kuwashirikisha wadau limechelewa kutokana na kuchelewa kwa pesa kutoka kwa wahisani na kwamba wadau wote wa Zanzibar na Tanzania bara watashirikishwa ili kupata maoni yao.

“Ukimuuliza Mkurugenzi wa mazingira Zanzibar anajua maana tumeshampatia taarifa na ni huyo ndiye anayetakiwa kuainisha wadau tutakaofanya nao kazi tutakapofikia hatua hiyo. Sasa hivi tunasubiri UNDP watupatie pesa ili tuanze na hatua ya kupata maoni ya wadau wote nchi nzima, ikiwemo Zanzibar” anasema Muyungi.