Wakulima wanakosa mavuno kwa kutojua maarifa ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi

Dotto Kahindi RoadToParis with Media21project and Tabianchi blog Ukosefu wa taarifa, elimu na maarifa ya kufanya kilimo bora na kukab... thumbnail 1 summary

Dotto Kahindi
RoadToParis with Media21project and Tabianchi blog
Ukosefu wa taarifa, elimu na maarifa ya kufanya kilimo bora na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ni vyanzo vikubwa vya wakulima kutopata mavuno ya kutosha kulingana na nguvu wanayotumia kuwekeza katika kilimo chao.

Mtandao wa Tabianchi umebaini hayo baada ya kuwatembelea wakulima wa mahindi, ndizi, nyanya na mbogamboga katika Wilaya ya Moshi vijini ambao mavuno ya kutosha kwao imekuwa ni changamoto kubwa kwa sasa.
Ukosefu huo wa mavuno hasa katika zao la mahindi kwa mwaka huu 2015 unatishia kuwepo wimbi la njaa kali katika maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo hasa katika vijiji vya Kata ya Kirua Vunjo Magharibi.

“Kutokana na ufinyu wa elimu hatujafanya lolote maana kama ni migomba ni ile ile, mahindi ni yale yale sasa hatujui mabadiliko yako kwenye hali ya hewa au kwenye mazao yenyewe” anasema Methew Nguma Mkulima wa mahindi katika kijiji cha Kirua.

Anasema “Hali ni mbaya sana, migomba imenyauka na kahawa imegoma kabisa. zamani ndizi zilikuwa zinazaa sana lakini sasa sielewi nini kimetokea, hakuna taarifa za kitaalamu za kutujuza tatizo hili linasababishwa na nini”

Wilaya ya Moshi Vijijini pamoja na maeneo mengine ya mkoa wa Kilimanjaro yalisifika sana kwa kilimo cha umwagiliaji hapo zamani kutokana na kuwa na miundombinu ya kutiririsha maji kutoka milimani jambo ambalo kwa sasa halipo tena.

Hali hiyo imewaacha wananchi katika hali ya sitofahamu wakihaha huku na kule kutafuta mbinu mpya za kufanya kilimo cha kawaida ili kujipatia mavuno na mapato ya kukuza uchumi katika familia zao.

Hali ya sasa ya magonjwa ya mimea na ukame vimewaathiri wananchi wa maeneo hayo kiuchumi na hivyo kukwamisha maendeleo ya mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.

“Mimeo inazongwa na magonjwa mengi tu, kuna magonjwa ya kahawa. Zamani tulikuwa tunapata misaada ya dawa kwenye kahawa kutoka serikalini lakini sasa hivi haipo misaada hiyo, tunathirika kiuchumi na kisaikolojia” anasema Nguma

Akitoa mchanganuo wa gharama za kulima mahindi alizotumia mwaka jana, Nguma anasema alianza kwa kununua mbegu za kisasa ambazo zinauzwa TZshs10,000 kwa kilo na hivyo alinunua kilo kumi kiasi ambacho kinafaa kupandwa katika shamba la heka moja.

Mbali na gharama za mbegu pia alikodi trekta kwa shilingi Tzshs40,000, akalipa vibarua kupanda mbegu TZshs40,000, vibarua parizi TZshs50,000, mbolea TZshs50,000, vibarua wa kuweka mbolea TZShs30,000 lakini matokeo yake mahindi yalipotoa tu mbelewele yote yalikauka na hivyo kupata hasara kubwa.

Bernard Pantaleo, Afisa Kilimo Kata ya Kirua Vunjo Magharibi anakiri kuwepo hali mbaya ya mfumo wa kilimo katika kata yake inayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi na ukosefu wa elimu ya kutosha kwa wakulima wa eneo hilo.
Bernard Pantaleo, Afisa Kilimo Kata ya Kirua Vunjo Magharibi

Anasema chemichemi za asili zimekufa na kwamba zinaathiri mwenendo wa kiuchumi na kiafya. Ingawaje kuna mabwawa ambayo yangeweza kutumiwa kwa kilimo cha umwagiliaji lakini hata hivyo mabwawa hayo yanamilikiwa na watu binafsi likiwemo bwawa la Muhorohoro, Choro na Kanje ambapo vijiji havina mamlaka nayo tena.

Kwa kuzitambua changamoto zinazowakumba wakulima zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, wao kama serkali ya kata wanatoa elimu ya kupanda miti na kutoikata hovyo, kutojenga kwenye vyanzo vya maji, kufanya kilimo hifadhi na kupanda mazao yanayostahimili ukame.

“Hali ya kilimo katika miaka ya hivi karibuni ni mbaya sana hapa kwetu, hali ya ukosefu wa chakula hasa mahindi inawakabili wakazi wa kata ya Kirua vunjo Magharibi, mwaka huu kuna hatari ya kuwa na njaa” anasema Pantaleo
Bwawa la Muhorohoro

Akizungumzia mchango wa taasisi ya ICIPE kupitia mradi wake wa CHIESA katika Wilaya ya Moshi Vijijini, Pantaleo anasema mradi huo ulikuja kwa lengo la kupima hali ya hewa na kuwashirikisha wananchi katika kutambua changamoto na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na njia za kukabiliana nayo.

Anasema mradi huo uliweka vifaa vya kupima hali ya hewa ili kutoa taarifa hizo katika vituo vya redio na televisheni ili kuwasaidia wananchi kupata taarifa hizo.

“Mwanzoni walipokuja walitoa mafunzo kwa wananchi wote wa vijiji vya kata hii, lakini baada ya hapo sijaona tena wakifanya kitu zaidi ya kupita tu hapa wakielekea kwenye vituo hivyo vya kupima hali ya hewa.” anasema Pantaleo na kuongeza kuwa.

“Taarifa za hali ya hewa pia zilipangwa kubandikwa kwenye mbao za matangazo kwenye kata ili wananchi waweze kuwa na maandalizi stahiki ya kufanya kilimo lakini hawajawahi kufanya hivyo”

Chemichemi ya Miwaleni
Kwa mujibu wa Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Kisangesangeni, Alphonce Mgalla chemichemi ya Miwaleni ni muhimu sana kwa mahitaji ya maji ya kunywa, kilimo na ufugaji na inategemewa na watu wengi wa vijini vinavyoizunguka. 
Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Kisangesangeni, Alphonce Mgalla
 
Chemichemi hiyo imezungukwa na vijiji vya Kisangesangeni, Miwaleni, Uchira, Koresa, Mwangalea, Ngasimu A na B, Moria, Mawala, Kiwanda cha sukari TPC, kiwanda cha Ngano na maeneo mengi ya Kata nzima ya Kahe.

Hata hivyo chemichemi hii inakabiliwa na changamoto za shughuli za binadamu zikiwemo kulima kwenye vyanzo vya maji, kukata miti na kufanya ujenzi wa makazi ndani ya chemichemi hiyo.
Mfereji wa maji unaotokana na chemichemi ya Miwaleni
Kwa kuona umuhimu wa chemichemi hiyo kwa wananchi sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, CHIESA kwa kushirkiana na Mamlaka ya Bonde la Mto Pangani na wananchi wa vijiji vya Sangesangeni na Miwaleni wameanzisha vuguvugu la utunzaji wa chemichemi hiyo.

“Kuna timu imeundwa ambayo inalenga kuhamasisha kuhifadhi chemichemi hii ambayo imeshirikisha watu wenye ushawishi vijijini na wadau mbalimbali ngazi ya kijiji na wilaya.” anasema Mgalla

Mradi wa CHIESA kwa kipindi cha miaka mitatu umekuwa ukifanya utafiti wa athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kuweka kituo cha hali ya hewa katika kijiji cha Kisangesangeni na kuwashirikisha wananchi ili kupata maoni yao juu ya njia gani zitumike kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

“CHIESA walikuwa wanashirikisha wananchi kutafuta dawa, nafikiri watakuja na dawa baada ya utafiti wao kukamilika” anasema Mgalla

Mradi wa CHIESA
Akizungumza kwa niaba ya Msimamizi wa mradi wa CHIESA Kilimanjaro, Prof. Shadrack Mwakalila, Mtaalam wa Mambo ya maji kutoka Bonde la Mto Pangani, Philipo Patrick anasema kuwa Mradi wa CHIESA unasimamia matumizi ya rasilimali ya maji, kuangalia uharibifu wa vyanzo vya maji na kuangalia hali ya hewa kwa kuweka vifaa maalumu vya kupima hali ya hewa, katika meneo ya Moshi vijijini.
Kituo cha kupima hali ya hewa kwenye kijiji cha Kisangesangeni
Anasema mradi huo umewashirikisha wananchi katika vijiji mbalimbali vya Wilaya ya Moshi Vijijini katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto za mabadiliko ya tabianchi jambo ambalo limefanyika kwa kipindi cha miaka mitatu ya awamu ya kwanza ya mradi huo.

Vile vile anaashiria kwamba baada ya kukamilika kwa awamu ya kwanza, wanajiandaa kufanya utekelezaji wa awamu ya pili itakayohusisha usambazaji wa taarifa zilizopatikana kwenye awamu ya kwanza ya mradi jambo ambalo litawawezesha wananchi kuchukua hatua stahiki za kuboresha kilimo chao na kupata maendeleo.

Utafiti huu pia ulilenga kupata taarifa zaidi za namna gani Bonde la mto Pangani na vyuo washiriki ambao ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine wataweza kutekeleza miradi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kushirikiana na Halimashauri za Wilaya. 

“Katika kushirikiana na wananchi kuibua njia za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, tumeona ni muhimu kuwepo kwa mashamba darasa mengi ili wakulima wengi washiriki kujifunza na kulinda chemichemi kama njia moja wapo ya kuboresha kilimo cha umwagiliaji” anasema Philipo

Makala hii imekujia kwa ufadhili wa CFI.