Wanakijiji watumia njia za asili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi

Dotto Khaindi   RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21   Wanakijiji katika Wilaya ya Kishapu wanakumbwa na ukame... thumbnail 1 summary

Dotto Khaindi
 
RoadToParis2015 with Tabianchiblog&CFIMedias21
 
Wanakijiji katika Wilaya ya Kishapu wanakumbwa na ukame wa hali ya juu unaotokana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Lakini badala ya kukaa na kuilalamikia serikali na kuomba msaada wa chakula wanakijiji hawa wameamua kutumia maarifa yao kubuni njia mbalimbali za kukabiliana na athari hizo.

Kwa usaidizi wa karibu wa shirika la kikristu linalotoa huduma kwa wakimbizi Tanganyika (TCRS), wananchi katika vijiji mbalimbali vya Kata ya Ngofila wilayani Kishapu wamefanikiwa kubuni miradi ya upandaji miti na ufugaji nyuki kama njia ya kujipatia kipato na kutunza mazingira.

Drop Irrigation
Peter Jibungu, mkazi wa kijiji cha Busongo ni miongoni mwa wanakijiji hao ambapo yeye amepanda miti ya aina tofauti kwenye shamba la ukubwa wa hekari tatu baada ya kupata elimu ya namna ya upandaji na utunzaji wa miti kwa njia ya umwagiliaji wa matone (Drop Irrigation).

Anasema elimu hiyo ameipata kutoka TCRS ambao pia walimpatia miti na chupa za matone Baada ya kunielekeza namna ya kupanda na kuitunza miti, nilianza kutumia njia hizo kwa upandaji na umwagiliaji." Jibungu anasema.

Anasema toka apande miti hiyo pamoja na ukame wa hali ya juu katika kijiji hicho miti yake haijakumbwa na tatizo lolote lile kwakuwa amekuwa mwangalifu katika kumwagilia na kuisimamia.
Miti inakua vizuri, mwaka jana pia nimepanda miti mingine na kufikisha idadi ya miti 3660 iliyohai na hali yake ni nzuri sana, kuna michache ilikufa kutokana na ukame lakini mingi imestawi na inanipa matumaini ya kuendelea kupanda mingine. anasema Jibungu.

Kulingana na maoni yake Jibungu, upandaji miti umebadilisha maisha yake na kuwa yenye matumaini Sasa hivi maisha yangu yako vizuri niko kwenye maandhari nzuri inayozungukwa na miti Napata upepo mwanana lakini zamani nilikuwa peupe sana upepo ulitusumbua mara kwa mara, sasa hivi kwangu ni kama masika, miti ni ya kijani kabisa

Anasema kuwa pamoja na kwamba miti yake haijafikia katika umri wa kuuza lakini miaka michache ijayo ataanza kuuza na kujipatia kipato kikubwa. Jibungu anasema kwa sasa anatumia miti kupata kuni za matumizi ya nyumbani, kivuli, hewa safi na kinga dhidi ya upepo na vimbunga ambayo vilikuwa ni tishio kwake kipindi cha nyuma.

Sijaanza kuuza miti, ila nafikiria kuweka mizinga ya nyuki ili niwe napata asali. Na kwenye pori hilo nyuki wanafaa kabisa. Wananikijiji wanashangaa kuona nyumba yangu imezungukwa na pori la miti tofauti na zamani hapakuwa hata na mti wa kivuli." Jibunga anasema na kuongeza kuwa.
Wanakiji wamehamasika sana kuhusu kupanda miti, maana ni njia pekee ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi isiyokuwa na gharama kubwa, nao wameanza kupanda miti katika mashamba yao

Namna ya uandaaji wa chupa za umwagiliaji
Njia ya umwagiliaji wa matone ni njia ya kienyeji ambayo haihitaji uwekezaji mkubwa ili kuitumia kama ilivyo katika aina nyingine za kilimo cha umwagiliaji ambacho huhitaji uwekezaji wenye gharama kubwa kufanikisha.

Mzee Jibungu anasema ili kufanikisha kilimo cha miti kwa umwagiliaji wa aina hii mkulima anapaswa kuwa na eneo la kupanda hiyo miti, kuandaa shamba, kupata miche ya miti, kuandaa chupa za maji zilizokwishatumika (chupa za maji ya Uhai, Kilimanjaro, Dasani na kadhalika) kisha zoezi la kupanda miti.

Anasema makopo hayo hutobolewa tundu dogo kwenye mfuniko wa chupa kwa kutumia spoku ya baiskeli na kisha hujazwa maji na kuegeshwa kwa kuinamishwa kwenye kila mche uliopandwa ambapo chupa moja yenye ujazo wa lita moja ya maji hukaa kwa muda wa siku nne.
Anasema njia hii imemsaidia sana kukuza miti yake kwakuwa hutumia maji kiasi kidogo sana na hivyo kuepukana na adhari ya ukame. Mwaka huu (2015) hakukuwa na mvua kabisa huku Kishapu lakini utaratibu huu umenisaidia kukuza miti anasema Jibungu

Jibungu amepanda miti mchanganyiko katika shamba lake ambapo kuna miti ya asili na ile ya kisasa, mingi ikiwa ni kwaajili ya mbao na nguzo ambayo anatarajia kuanza kuiuza baaada ya miaka mitano hadi kumi kuanzia sasa.


Miti hii inachukua kama miaka kumi kukomaa kufikia kukata mbao, kwa hiyo baada ya miaka mitano mpaka kumi ijayo nitaweza kuvuna miti kwa mbaoanasema Jibungu.
Wakati huu ambao kilimo chake cha miti kikiendelea kustawi na akisubiri kufikia wakati wa kuuza mwanakijiji huyo anafanya kilimo cha mazao ya vyakula kama vile mtama, mahindi, uwele, alizeti na kunde, ambavyo humsaidia kwa chakula na kuuza na pia kwa mahitaji ya familia.

Ufugaji nyuki
Andrew Shigela mbaye ni mwanakijiji wa Inolelo, Kata Ngofila, Kishapu, Shinyanga ni mmoja kati ya viongozi wa kundi la Mshikamano linalojihusisha na ufugaji wa nyuki kwa muda wa miaka miwili sasa.
Kundi la Mshikamano linaamini kuwa ufugaji nyuki ni njia muhimu katika kukabiliana na athari za ukame zinazosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, kwakuwa njia hii inawapatia kipato na kuwawezesha kuendesha familia zao.

Mwaka jana (2014) tulianza na mizinga 7 lakini kufikia muda huu tuna mizinga 48. Tumeshaanza kuvuna asali tayari, tunavuna kila baada ya miezi mitatu, tulivuna mwezi wa sita, tukavuna tena wa tisa na tunategemea kuvuna tena mwezi wa 12 anasema Shigela.
Kulingana na Shigela zamani walikuwa wakivuna asali kwa njia za kienyeji lakini sasa wamenunua vifaa maalumu vya kuvuna asali japo uvunaji bado uko chini ikilinganishwa na idadi ya mizinga waliyonayo.

Mavuno ya asali kwa awamu mmoja ni kati ya lita 60 hadi 100 kiasi ambacho ni kidogo sana na huchangiwa na uchelewaji wa kuanza zoezi la uvunaji asali Hawa nyuki wa kienyeji wajanja sana, mkichelewa kidogo tu mnakuta wameshakula asali yote, hii ni changamoto kwetu lakini tutaikabili kwakuwa iko ndani ya uwezo wetu anasema Shigela.

Kikundi hicho cha wafugaji asali kina wanachama.25, wanaonufaika na asali na fedha wanazopata kutokana na ufugaji huo. Pesa hizo za asali huhifadhiwa kwenye akaunti ya benki ya kikundi kwaajili ya kuendeleza mradi wao huku kiasi kidogo cha pesa wakigawana kwaajili ya mahitaji muhimu ikiwamo kusomesha watoto, kusaidia watoto yatima na wasiojiweza.

Lita moja ya asali jijini Dar es Salaam, huuzwa kati ya 80,000TZS mpaka 10,000TZS wakati kwenye maeneo ya mikoani ikiwemo Shinyanga huuzwa kati ya 40,000TZS na 80,000TZS.

Mkulima mwingine Joseph Kadala, kutoka kijiji cha Ngofila, kata ya Ngofila Wilaya ya Kishapu, Shinyanga analia na hali ya ukame jinsi inavyokwamisha na kurudisha nyuma mipango na maendeleo ya wakulima Kishapu.

Anasema kwa sasa hawategemei kilimo cha mvua hasa katika kijiji cha Ngofila zaidi ya kutumia kilimo cha umwagiliaji wakitegemea zaidi maji kutoka kwenye mto mdogo wa Manonga ambao hauko mbali na kijiji chao.

Mto wenyewe hauna maji mengi, kwahiyo tunachofanya ni kuanza kulima mwezi wa nne na kufikia mwezi wa saba tunakuwa tumeshavuna. Changamoto ya kilimo cha umwagiliaji huwezi kutumia shamba kubwa hivyo tunalima heka moja kwa mazao ya chakula na tunapata hata gunia tano (gunia moja lina kilo 100) anasema Kadala.

Kijiji cha Ngofila kina kaya 430, ambazo zina wakaazi 3466 hata hivyo hali ya ukame imesababisha umaskini kuongezeka ambapo hakuna uwezekano wa familia kupata milo mitatu kwa siku. 

Wakati kijiji cha Inolelo, kina mwamko wa hali ya juu katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwani kuna shamba lenye msitu wa kupandwa ekari 15 za miti ya milonge na miarobaini na ndani ya msitu huo kuna mradi wa ufugaji nyuki. 

 Faida za kilimo cha miti
Kilimo cha miti kimepata umaarufu wa ghafla miaka ya hivi karibuni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ongezeko la mahitaji ya mazao ya miti na changamoto ya mazingira ambapo kwa hapa Tanzania mkoa wa Iringa ni moja ya mikoa maarufu inayoongoza kwa misitu mikubwa ya kupandwa.

Miti inatumika kwa mbao, nguzo za umeme, nguzo za kujengea pamoja na utengenezeji wa karatasi lakini ukiacha mahitaji haya hivi sasa kumeibuka fursa nyingine mpya ambapo mashirika ya kimazingira kutoka Magharibi yananunua hewa ukaa (carbon dioxide). 

Kwa maana hiyo mkulima anaweza kupanda shamba la miti halafu akawa anakusanya dola kwa kuuza hewa ukaa wakati akisubiri miti ikomae avune mbao, nguzo ama miti ghafi ya kutengenezea karatasi.

Mwezeshaji wa TCRS, Genes Tarimo, anasema kazi yao ilikuwa ni kuwawezesha wakulima hao ujuzi na maarifa ya kupanda miti na ufugaji wa nyuki na kuwapatia nyenzo za kuanzia kama mbegu (miche) za miti na mizinga ya nyuki.

Tarimo asema miti waliyotoa kwa wakulima ilipatikana kwa ushirikiano mkubwa na ofisi ya misitu ya Kishapu ambapo miti zaidi ya 20,000 imepandwa katika Wilaya ya Kishapu katika kipindi cha mwaka 2012 hadi 2015.

 Nashauri uoteshaji wa miti ufanyike katika maeneo ya vijijini ili wananchi waweze kupata miti kwa urahisi na kwa gharama nafuu. Kutoa miti mbali kwanza ni changamoto kwakuwa wakati mwingine haiendani na eneo hilo na inatumia gharama kubwa pia anasema Tarimo. 

Habari hii imefadhiliwa na CFIMedia21 Project