Niliyojifunza kutoka Mkutano wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi COP21

Dotto Kahindi, Le Bourget, Paris, Ufaransa Kupitia mradi wa CFIMedia21 nimekuwa miongoni mwa waandishi wa habari, Bloggers na Watang... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi, Le Bourget, Paris, Ufaransa

Kupitia mradi wa CFIMedia21 nimekuwa miongoni mwa waandishi wa habari, Bloggers na Watangazaji kutoka nchi za Afrika na Asia waliohudhuria Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi COP21, uliofanyika Mjini Paris, Ufaransa Disemba 2015.

Makala hii fupi inalenga kutoa ‘mtazamo wangu’ juu ya mambo kadhaa yaliyojitokeza kwenye mkutano huu.
Wanufaika wa mradi wa CFIMedias21 kutoka Afrika na Asia katika picha ya pamoja
Maandalizi
Maandalizi ya mkutano huu ambayo yamefanywa na wenyeji Serikali ya Ufaransa kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi (UNFCCC) yamekuwa ni ya hali ya juu kufanikisha jambo hili.

Ufaransa ilijipanga sawasawa kuhakikisha mkutano huu unafanyika katika mazingira mazuri yatakayotoa mwanya kwa nchi wanachama wa mkutano, wanaharakati, waandishi wa habari na wadau wengine wa mabadiliko ya tabianchi kufanya kazi zao katika mazingira mazuri.

Mkutano huu umefanyika Le Bourget, Paris, Ufaransa, eneo ambalo hutumika kama uwanja mdogo wa ndege lakini likabadilishwa kwa muda ili kutosheleza mahitaji ya mkutano wenyewe.

Usafiri
Utaratibu wa alama za usafiri na namna ya kufika eneo la mkutano ulikuwa mzuri na rahisi jambo ambalo liliwezesha kila mtu kufika Le Bourget kila alipotaka kufanya hivyo.

Kwa wale waliotumia treni kuna alama za uelekeo wa treni ya kuelekea kwenye mkutano, kwa kuwa kuna treni nyingi na zinakwenda sehemu tofauti hii ilikuwa na msaada mkubwa kwa wenzangu na mimi ambao kujua ni mpaka kuona.

Kulikuwa na mabasi ambayo yaliwachukua washiriki kutoka kwenye kituo cha treni kwenda kwenye eneo la mkutano, ambayo yalikuwa yakiondoka kila baada ya dakika 5.

Ukarimu (Hospitality)
Inawezekana kulikuwa na mafunzo mazuri kwa wasaidizi katika mkutano huo ambao muda wote hata pale walipokuwa na njaa walitabasamu na kukaribisha washiriki kwa upendo.

Hii si tu kwa wahudumu katika mkutano huo ambao walikuwa kila kona kuanzia kwenye vituo vya treni, kwenye mabasi, na katika mkutano wenyewe bali hata kwenye maeneo ya hoteli tulipoishi mambo yalikuwa murua.

Ulinzi na Usalama
Kulikuwa na ulinzi wa hali ya juu katika mkutano huu pengine ni kutokana na shambulio la kigaidi lililotokea mapema mwezi Novemba 2015, hivyo walihakikisha washiriki katika mkutano huu wanashiriki salama  bila kuwa na shaka ya shambulio.

Ukaguzi wa mali za washiriki walizoingia nazo kwenye mkutano ulikuwa mkali sana, kila ukiingia ‘wali-scan’ mizigo yako yote na kuchunguza kibali chako cha kuhudhuria mkutano huo, jambo ambalo liliondoa hofu ya watu wengi ya kuwa huenda kukawa na shambulio kwenye mkutano huo.

Chakula
Kwakweli kwenye chakula mambo ndo yalikuwa magumu, yaani ni full mikate, miti (mboga za majani), burger, sandwhich nk, yaani kwa wale tunaotoka Musoma na Kakamega kwetu ilikuwa kama mboga tu, kwa kifupi muda wote tukiwa Paris tulikuwa tunakula mboga.

COP ijayo nitabeba unga wa muhogo na mahindi halafu nitajipikia mwenyewe, haipendezi kabisa kukomba mboga kwa masiku yote hayo.

Vyumba vya habari (Newsrooms)
Kama ni kujali waandishi wa habari basi mkutano huu ulijali sana waandishi pamoja na kuwa na idadi kubwa ya waandishi lakini kulikuwa na vifaa vya kutosha vya kutendea kazi hasa kompyuta na makabati ya kutunzia vifaa vingine.

Kulikuwa pia na eneo la kupumzika (Kulala) maalumu kwa waandishi wa habari ili kupunguza uchovu wa mihangaiko ya kutafuta habari ndani ya mkutano huo ambazo zilikuwa na changamoto kubwa pia. Pia kulikuwa na intaneti nzuri

Afrika
Ni mataifa machache tu ya Afrika yaliyoweza kuweka mabanda yake au vituo vya taarifa kwenye banda kubwa la Afrika (African Pavillion), kwa bahati mbaya katika nchi hizo chache Tanzania pamoja na kupeleka ujumbe wake kwenye mkutano huo haimo.

Kwa Tanzania pengine ni kutokana na kutokuwa na waziri kwa wakati huu, au pengine ni kutokana na kubana matumzi yasiyo ya lazima kama alivyoagiza Rais Magufuli lakini nilidhani ingekuwa muhimu kutumia fursa hizi kutangaza mambo muhimu ikiwemo fursa za biashara na uwekezaji pamoja na utalii.

Mataifa mengine yalikwenda na ushawishi wa miradi, biashara na uwekezaji ili kuutumia mkutano huo kupata washirika watakaosaidia kutumia changamoto za mabadiliko ya tabianchi kama fursa za kiuchumi.

Kama kuwa na banda la Tanzania pekee ni gharama basi kungekuwa hata na banda la Afrika Mashariki lakini haikuwa hivyo, ushirikiano wa Afrika Mashariki unahitajika pia katika mambo muhimu kama ya mabadiliko ya tabiachi. Si Kenya, Tanzania, Rwanda, Burundi ama Uganda waliokuwa na banda.

Mashirika ya Binafsi na Wanaharakati
Afisa Miradi Forumcc, Fazal Issa akihamasisha katika moja ya maandamano waliyoyafanya wakati wa COP21
Mashirika binafsi na wanaharakati walikuwa na nafasi kubwa sana ya kufanya ushawishi katika majadiliano hayo kwa manufaa ya nchi wanazotoka ambapo Tanzania tulipata nguvu kutoka ForumCC ambao walishirikiana na PACJA.

ForumCC kwa kushirikiana na PACJA wameleta mchango mkubwa katika kuwezesha kupatikana kwa andiko la mkabata wa mabadiliko ya tabianchi.

Ni taasisi hii ambayo ilikuwa mstari wa mbele kusema, kukosoa na kutoa mapendekezo mbadala ambayo yangefaa kuwamo kwenye mkataba mpya wa mabadiliko ya tabianchi na mchango wao umeifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana

Niliwatumia pia katika kupata ufafanuzi wa kina wa vipengele vya mkataba huo ili kuuelewa vizuri kabla ya kuupasha umma wa watanzania na wapeni wa mtandao wangu kwa ujumla

Place-to-B
Miongoni mwa shughuli za ubunifu zenye lengo la kuwaunganisha watu wa mataifa mbalimbali katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi bila kujali wanatoka katika fani gani, Place-to-B ilionekana sehemu muhimu sana.

Mpango huu ambao unaendeshwa na Anne-Sophie Novel kwa lengo la kupata mawazo ya kibunifu kutoka pande tofauti za dunia.

Kwa kutambua kuwa mpango huu ungewakutanisha watu wengi, Place-to-B iliamuliwa ifanyike kwenye hoteli ya St. Christophers Inn iliyopo Gare du Nord, ambayo ina uwezo wa kuchukua zaidi ya watu 600 kwa usiku mmoja.

Kulikuwa na shughuli mbalimbali zilizoendelea katika Place-to-B na moja wapo ilikuwa ni majadiliano, uandaaji wa vipindi vya radio, televisheni na kulikuwa na kipindi cha televisheni ambacho kilirushwa moja kwa moja kutokea hapo.

Ni eneo hili ambalo nilipata nafasi ya kukutana na viongozi, wanaharakati, wanahabari kutoka mataifa mbalimbali na kubadilishana mawazo.

Uwakilishi wa Tanzania
Pamoja na Tanzania kutokuwa na Waziri wa Mazingira katika majadiliano ya mkutano huu wa Paris, kazi kubwa iliyofanywa na balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Begum Taj ambaye kwa kushirkiana kwa ukaribu na mwakilishi wa Tanzania kwenye mkutano huo Dr. Richard Muyungi wamecheza karata yao vizuri.

Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe Begum Taj akiwa na Dr. Richard Muyungi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Tanzania
Ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huu ulikuwa na jumla ya watu 12, idadi ambayo  ilimjumuisha balozi huyo na walikuwa na kazi kubwa ya kusimamia maslahi ya nchi katika kufikia makubaliano ya mkataba huo mpya wa mabadiliko ya tabianchi.

Ujumbe huu ulieleza kuwa Tanzania inahitaji kiasi cha dola za Kimarekani 65 bilioni sawa na bilioni 140 kwa mwaka kwa ajili ya kutekeleza mchango wake wa kila nchi katika juhudi za dunia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Intended Nationally Determined Contributions – INDCs).

Magufuli
Jambo ambalo sikutegemea kulipata Paris ni namna watu wanavyomkubali Rais mpya wa Tanzania, Dr. John Pombe Magufuli, kutokana na utendaji aliouonyesha kwa kipindi kifupi cha uongozi wake.

Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr. John Pombe Magufuli

Pengine kutokana na kupenda kwangu kuvaa skafu yenye rangi ya bendera ya Tanzania ilikuwa rahisi kwa watu wengi kutambua utaifa wangu na jambo la kwanza walilouliza baada ya salamu ilikuwa ni Magufuli.

Wanaamini chini ya uongozi wa Magufuli mikataba ya kibwenyenye haitapata nafasi na hivyo utekelezaji wa mambo yote yatakayoamuliwa kwenye mkataba mpya wa mabadiliko ya tabianchi utasimamiwa mguu kwa mguu kama sio jicho kwa jicho.

Sifa hii pia inaongeza matumaini kwa nchi wahisani kuwa na imani ya kuendelea kuisaidia Tanzania katika miradi ya maendeleo na madailiko ya tabianchi kwakuwa usimamizi na uwajibikaji utakuwa umeongezeka ndani na nje ya serikali ya Tanzania

Mkataba wa mabadiliko ya tabianchi
Baada ya majadiliano makali baina ya nchi wanachama wa mkutano huo mnamo siku ya Jumamosi, Disemba 12, 2015 makubaliano ya mkataba mpya wa mabadiliko ya tabianchi yakafikiwa.

Pamoja na mkataba wenyewe kuwa na mapungufu kadhaa lakini nchi ziliufurahia ikiwa kama ni hatua ya kwanza kuelekea kwenye makubaliano mapana yenye manufaa kwa wote.

Miongoni mwa mambo yaliyomo kwenye mkataba huo ni pamoja na Kiwango cha nyuzi joto, Upunguzaji wa gesi Joto, Kukabiliana na mabadiliko ya tabainchi, Uharibifu na upotevu, Fedha za mabadiliko ya tabianchi na Mfumo wa taasisi.

Hatua inayofuata baada ya majadiliano ya Paris kumalizika, ni Katibu Mkuu wa COP kuwaalika wanachama wote Aprili 22, 2016 ili kutia sahihi mkataba huu na utakuwa wazi kuridhia mpaka 2017.

Idadi ya nchi wanachama wanaotakiwa kuasini ili kuupa nguvu ya kuanza kutumika mkabata huo ni 55, idadi ambayo ni karibu na theluthi moja ya nchi wanachama wa mkutano huo ambayo ni 196.

Makala ifuatayo itaeleza na kuchambua kwa kina vipengele vyote vya mkataba mpya wa mabadiliko ya tabianchi, endelea kutembelea mtandao huu