Serikali yakiri uharibifu wa vyanzo vya maji, misitu, kingo za bahari na mito ni wakutisha nchini

Dotto Kahindi Pamoja na kuwepo kwa Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 ambayo inaweka makatazo mahsusi kwa nia ya kuepusha uharibifu wa m... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi
Pamoja na kuwepo kwa Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 ambayo inaweka makatazo mahsusi kwa nia ya kuepusha uharibifu wa mazingira lakini Taarifa ya Hali ya Mazingira Nchini inaonyesha uharibifu wa mazingira ni wa kutisha. 

Mito mingi nchini inakauka, Vyanzo vingi vya maji vinakufa, Miti na misitu ya asili inapungua kwa kasi kubwa kila mwaka na taifa linapoteza zaidi ya ekari milioni moja za misitu.
 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Mazingira January Makamba (MB) anasema Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha kwamba Sheria hii inatekelezwa kwa ukamilifu wake ili kupunguza kama sio kumaliza kabisa vitendo vya uharibifu wa mazingira.

Anasema mwanzoni mwa mwaka ujao (2016) Serikali italeta mpango kabambe wa kupambana na uharibifu wa mazingira, ambao utatoa wajibu kwa kila mwananchi na kila taasisi ya umma na binafsi.

Makamba anakiri kuwa uharibifu wa mazingira unaathiri sekta zote muhimu ikiwamo kilimo, mifugo, uvuvi, utalii, uzalishaji umeme, makazi, miundombinu na hivyo kupunguza uwezo wa nchi kupata maendeleo endelevu. 

“Tukiendelea na mwenendo wa sasa wa uchafuzi wa mazingira, ndani ya kipindi kifupi, mifugo na wanyamapori watakosa malisho, tumeshaanza kuona viboko wanakufa kwenye Mto Ruaha kutokana na kukauka kwa mto, watu watakosa maji ya kutumia, kilimo kitashindikana” anasema Makamba

Tayari Serikali ya awamu ya Tano imeanza kutekeleza mipango yake ya kuyalinda mazingira kwa kuanzisha operesheni ya kuwaondoa watu wanaoishi na kufanya shughuli kwenye maeneo ya kingo za mito na maziwa, fukwe za bahari, maeneo oevu (swampy) na maeneo ya wazi (Open spaces).

Kwa Dar es Salaam, zoezi la kuwaondoa wananchi waliojenga au kufanya shughuli kwenye maeneo haya kinyume cha sheria na taratibu lilianza rasmi tarehe 17/12/2015 likiratibiwa na kusimamiwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwa kushirikiana na mamlaka za Serikali za Mitaa.

Makamba anasema kuwa ongezeko la watu jijini Dar es Salaam na maeneo mengine ya miji, uvamizi wa maeneo ya kingo za mito, mikondo ya bahari, maeneo oevu umeongezeka kwa watu kufanya ujenzi wa nyumba, kilimo, ufugaji, utupiaji taka na uchimbaji mchanga.

“Shughuli hizi katika maeneo hayo husababisha uharibifu na madhara makubwa ya mazingira hasa kipindi cha mvua ambapo maji hukosa uelekeo kutokana na njia zake za asili kuzibwa na hivyo kutawanyika hovyo na kusababisha mafuriko, uharibifu mkubwa wa miundombinu hasa madaraja ambayo huvunjika, kukatika kwa barabara na vifo” anasema Makamba.

Anataja athari nyingine za kuvamia maeneo hayo kuwa ni kusambaa kwa magonjwa ya mlipuko yasiyoisha hasa kipindupindu kutokana na maeneo hayo ya mikondo ya mito kutokua na mfumo wa utoaji wa maji taka.