Mraghbishi
Noorkiyengop Mbaima toka kijiji cha Enguserosambu akisimama mbele ya
mifugo iliyokutwa msituni katika eneo lililoruhusiwa la msitu wa jamii
wa Enguserosambu
Ilikuwa
ni siku ya shangwe na furaha kwa wananchi wa kata ya Enguserosambu
wilayani Ngorongoro. Hii ni baada ya serikali kukubali ombi lao la
kusimamia rasilimali ya msitu wa Loliondo namba 2 unaopakana na vijiji
vinne vinavyokadiriwa kuwa na idadi ya wakazi wapatao 20,000
wanaotegemea mahitaji yao toka katika huo msitu.
Huu
ni msitu pekee ambao wananchi kwa kushirikiana na Mkuu wao wa wilaya,
na mashirika rafiki, wamefanikiwa kuishawishi serikali kuukabidhi msitu
huo kwao. Katika mchakato huo uliochukua miaka kadhaa wanawake toka
katika vijiji vya Enguserosambu, Ng’arua, Orkiu na Naan wamekuwa mstari
wa mbele katika kufanikisha azma hiyo ya kubakiza msitu wao wa enzi
mikononi mwao. Akielezea furaha yake aliposikia msitu wa Loliondo namba 2
umekabidhiwa kwa wananchi, mraghbishi mwanamke Noorkiyengop Mbaima
alisema
“Mimi
mwenyewe nimefurahia, kwa sababu sisi akina mama tunategemea sana msitu
huu kwa mahitaji yetu. Huu msitu kama ungeondoka katika mikono ya jamii
basi tungeathirika sana sisi kina mama.” Umuhimu wa msitu huu kwa kina
mama ndio uliowapelekea wao kutunga na kuimba nyimbo za hamasa na
kutumbuiza, kushiriki kwa wingi katika vikao mbalimbali vya maamuzi
wakati wote wa mchakato huo.
Kwa
kuwa msitu huu ndio tegemeo lao katika kuendesha maisha ya kila siku.
Hakuna chochote ambacho kiliamriwa bila ya wao kuchangia na
kushirikishwa kuanzia utungaji wa sheria ndogongogo za usimamizi wa
msitu hadi kukabidhiwa rasmi msitu huo. “Nikichukulia mfano katika
mikutano yote ya vijiji. Kiukweli wanawake wamekuwa wanajitokeza kwa
wingi, kuliko makundi mengine yoyote. Hata ile siku ya uzinduzi wa msitu
walikuwa wengi zaidi,” anaelezea Jackson Nangiria
Ushiriki huu wa wanawake unatokana
na ukweli kwamba wana uhusiano wa karibu na msitu huo wa enzi wa
Enguserosambu.Si kwa ajili yao tu pamoja na watoto wao pia. Ni watoto
hawa wa kike wenye majukumu ya kujenga nyumba kwa kutumia miti inayotoka
ndani ya msitu huu, ndio wanaotembea na punda wakiwabebesha maguduria
ya maji kwa umbali mrefu wakitafuta maji ambayo chanzo chake kipo kwenye
msitu huu. Wanapopata watoto wanahitaji dawa za kuwaogeshea na dawa za
uzazi ambazo zinatoka kwenye msitu huu.
Wao
ndio wapishi katika familia zao hivyo wanahitaji kuni zinatokana na
miti iliyoanguka na kukauka ambayo inapatikana kwenye msitu huu. “Kina
mama wanafanya mitambiko ndani ya msitu huu wengine ambao hawakupata
watoto wanapatia hapo baada ya kuomba ndani ya msitu huu. Si hivyo tu
ndani ya msitu huu kuna dawa mbalimbali za asili kwa mfano mtoto
akizaliwadawa ya kumwogesha na kumnawisha hupatikana humo humo na
nyingine ni za kunywa kama maziwa na nyingine kwa ajili ya mama,”
anaeleza mwanamama mraghbishi Noorkiyengop Mbaima. Uwepo wa wanawake
hawa wa Kimasai katika kata ya Enguserosambu kiukweli unatokana na uwepo
wa msitu huu. Huu ndio msitu wa enzi ambao serikali ilipendekeza uwe
chini ya usimamizi wake kama ulivyokuwa msitnamba moja wa Loliondo.
Pendekezo
hilo lilitolewa kupitia timu mbalimbali toka wizarani, ofisi za kanda
na halmshauri ya wilaya, ambazo zilitembelea kijijini hapo kuomba
kupatiwa muhtasari wa kikao cha kijiji kitakachopitisha ombi hilo la
serikali.
Ombi hilo linakuja kwa kijiji kwa
sababu msitu huo umekuwa chini ya usimamizi wa wananchi wa kata ya
Enguserosambu kwa miaka mingi. Ni wananchi hao ndio ambao wameutunza
msitu huo pasipo Kuombwa wala Kukabidhiwa na serikali. Na kwa kweli
wameweza kuutunza kwa muda wote huo. Miti haijakatwa, wananchi
wamejiwekea sheria ndogondogo na pia kuwakamata wale ambao wamekuwa
wakiharibu msitu huo. Hivyo wananchi hawa wamewajibika katika
kuhakikisha msitu unabaki katika hali yake ya asili pasipo kushurutishwa
na mtu yeyote.
Kwa mantiki hiyo muhtsari uliokuwa
unaombwa na serikali ya halmashauri yan wilaya ulihiitaji baraka za
wananchi, ambao hawakuwa tayari kutoa sehemu ya uhai wao unaotegemea
msitu huo. Hakuna mwanakijiji aliyekuwa tayari kukubali ombi hilo. Na
jibu lilikuwa ni wazi kabisa kwamba ombi hilo lilitishia mustakabali wa
jamii zinazozunguka msitu huo ambazo ni vijiji vya Enguserosambu,
Ng’arua, Orkiu na Naan. Hivyo wakati serikali ikipendekeza kuusimamia
msitu huo wananchi kwa upande
mwingine wakaanza kuiomba serikali iwaruhusu kuusimamia. Ni kama
kichekesho pande zote zinaombana kuusimamia msitu huo. Serikalikupitia
halmashauri ya wilaya inasema tunahitaji kuusimamia, na wananchi
wanaiomba serikali hiyo hiyo kuusimamia msitu huo. “Kwa kweli sisi kama
wananchi wa Enguserosambu tumeona kwamba huu msitu ukiondoka chini ya
usimamizi wetu tutaathirika. Kwa sababu msitu huu ni uhai wa wananchi wa
hapa. Tukikosa huu msitu, hatupati maji wala mvua, tutakosa chakula.
Kwa kifupi tutakosa kitu muhimu cha uhai wa jamii,” anaelezea mraghbishi
Noorkiyengop
Mbaima.
Ndani ya msitu huu kuna miti ambayo
wazee wanaitumia kwa ajili ya shughuli za kimila pamoja na miti ya
kiasili ambayo inatumika kwa shughuli mbalimbali. Baadhi ya miti hiyo ni
pamoja na Oroilieni ambao unatumika kwenye shughuli za jadi, ujenzi na
kiimani. Akifafanua kuhusu mti huo Robert Kamakia anaelezea, “Huwezi
kuingia jando bila kuwa na mti Oroilieni. Kwa kuwa unatumika katika
kufanya baadhi ya shughuli za kimila. Mti mwingine ni Orikienyi ambao
unatumika kama dawa ya kutibia magonjwa ya aina mbalimbali kama homa,
kifua, malaria na kadhalika. Mti mwingine ni Ostiani ambao hutumika kwa
ajili ya kivuli na kutunza maji.”
Hivyo
msitu huu una maana kubwa sana kwa makundi mbalimbali yakiwemo ya
wazee, wanawake na vijana. K wa upande wa vijana kwa mfano, mila na
desturi za kimasai zinawataka kujitenga hasa pale wanapoingia ngazi ya
Morani. Ambapo hutakiwa kuweka kambi kwa ajili ya kuchinja ng’ombe na
kula nyama. Tukio hili huchukua mpaka mwezi mmoja wakati vijana hao,
wanapoazimisha sherehe hizo.
Tukio
hili linashirikisha matumizi ya miti mbalimbali kwa mujibu wa taratibu
zao. Supu wanazokunywa huchanganywa na baadhi ya majani ya miti hiyo. Ni
dhahiri ulaji wa nyama kwa mwezi mzima unahitaji pia matumizi ya dawa
za asili. Na ndio maana wamasai hawasumbuliwi sana na magonjwa
yanayotokana na ulaji mwingi wa nyamba. Si hivyo tu porini hamna vitanda
hivyo baadhi ya majani hutumika kwa ajili ya zoezi hilo.
“Kiukweli
bila msitu vijana hawawezi kufanya chochote. Kwa kuwa kila kitu
kinatoka katika huo msitu,” anafafanua Julius Long’oli. Lakini si hivyo
tu, wakati wanaingizwa jando pia kuna miti inayotumika. Vivyo hivyo na
katika sherehe za kumaliza jando. Hivyo msitu ni sehemu ya mila na
utamaduni wa jamii hizi zinaouzunguka. Ni imani yao pia, ambayo kimsingi
ni lazima iheshimiwe. Huu ni msitu wao wa enzi na enzi. “Huu ni msitu
wa jamii kwa Kimasai unaitwa Elieteti yaani ndani ya jamii kwa maana ya
jina hilo ni msitu unaosaidia jamii ya sasa na ya kizazi kijacho. Kwamba
huu msitu unategemewa na kizazi cha sasa na kijacho,” anafafanua Yohana
Tuluni mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya kusimamia msitu. Mtizamo huu
wa wananchi wa kata hii, kwamba wao ndio wausimamie msitu huu, unatokana
hali halisi ya msitu namba moja wa Loliondo unaosimamiwa na serikali
kupitia halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro kuwa katika hali ya
kutoridhisha. Miti mingi imekatwa kwa ajili ya matumizi ya ujenzi na
hivyo kutishia uhai wa msitu huo. Kitu ambacho wana Enguserosambu
hawakupenda kitokee kwa msitu namba mbili wa Loliondo ambao wanautegemea
kwa mustakabali wa maisha yao. Msitu huu umekuwa ukitegemewa na jamii
ya hapa kwa miaka mingi. Ni wao ndio ambao wamekuwa wakiutunza na kwa
kweli wamefanikiwa kwa njia moja ama nyingine kuufanya uwe mzuri zaidi
kuliko hata ule wa Liliondo moja unasimamiwa na serikali.
“Wazo la kutaka kumiliki msitu
lilikuwa kama ndoto, ukiangalia na hali halisi ilivyokuwa. Ni maono ya
mtu mmoja aliyewashirikisha wenzake. Mwishowe wazo likatolewa Kwa
wanakijiji ambao waliungamkono wazo hilo. Na mwishowe tukamwandikia Mkuu
wa Wilaya na kwa kweli alituunga mkono sana,” anafafanua mraghbishi na
mjumbe wa Bodi ya Wadhamini Jackso Nangiria Mchakato wa kuomba hadi
kukabidhiwa usimamizi wa msitu umewezesha wananchi wa Enguserosambu
kuongeza ufahamu wa mambo mbalimbali juu ya usimamizi wa misitu lakini
pia mahusiano baina ya wananchi na viongozi yameboreka zaidi.
Umoja
ni nguvu utengano ni udhaifu, hivi ndivyo unavyoweza kusema
Wanaenguserosambu wamekuwa wamoja zaidi. Mashirika rafiki yamesaidia
sana katika kutoa elimu kwa wananchi na viongozi wao ambao maarifa hayo
yamewezesha kujiwekea mikakati na hatimaye kufanikisha jamii kumiliki
msitu wake wa enzi kwenye mikono yake. Wakati mchakato unaanza palikuwa
na kijiji kimoja tu cha Enguserosambu kilichokuwa kinaundwa na vitongoji
vinne vya Enguserosambu, Ng’arua, Orkiu na Naan ambavyo sasa vimepata
hadhi ya kuwa vijiji. Kwa sasa sauti yao ni kubwa zaidi kuliko pale
Mwanzo.
Watendaji wa PALISEP wakiwa pamoja
na wanajamii wakishikana mikono kuonesha ushirikiano baina yao. Kuanzia
kushoto ni Sarah Saningo, Robert Kamakia, Jackson Nangiria, Norkiyengop
Mbaima, Sunde Tutayo na Fredy Samberu
Hivyo Bodi ya Wadhamini ilichaguliwa
na mkutano mkuu wa kijiji, ambacho sasa kina hadhi ya kata. Kwa hiyo
usimamizi wa msitu huu kwa sasa umekabidhiwa kwa Kata ya Enguserosambu.
Hivyo wananchi kutoka katika kila kijiji walichagua wawakilishi wao
waliounda Bodi ya Wadhamini. Wawakilishi hawa jukumu lao kubwa ni
kuratibu mchakato wote wa uombaji usimamizi wa msitu wa Loliondo 2.
Baada
ya kuchaguliwa wajumbe walipatiwa mafunzo na shirika la PALISEP ambao
pia walisaidia uandikishwaji wa bodi tarehe 12/09/2012. Bodi hiyo
imeundwa na wajumbe 10 kati ya hao wanawake ni 4. Bodi hii ilipata
mafunzo ya sheria mbalimbali za misitu, usimamizi wa misitu na bodi
yenyewe pia kupitia video ya hali ya msitu wa Loliondo 1. Walipata pia
ziara za mafunzo kwa kutembelea misitu inayosimamiwa na jamii kwa mfano
msitu wa Suledo uliopo Manyara wilaya ya Kiteto. Bila jamii kujitoa kwa
hali na mali isingewezekana kufanikiwa kwenye hili. Kwani bodi ya
wadhamini imefanya kazi kubwa. Jamii imeshiriki katika kuandika katiba
ya bodi na sheria ndogondogo ambazo zimepitishwa katika mikutano ya
vijiji.
“Baada ya kuchaguliwa jukumu letu
ilikuwa ni kutembelea msitu ili kujua hali yake. Lakini pia tuliweza
kutoa elimu kwa wale waliokuwa wanaishi na kufanya shughuli za kilimo
ndani ya msitu. Ili waweze kuondoka. Si kazi rahisi,” mjumbe wa Kamati
ya Bodi ya Wadhamini Sunde Tutayo.
Kwa sasa mpango ni kuboresha na
kutunza vyanzo vya maji. Kupitia bodi hiyo, wananchi wamejiwekea malengo
ya kuuongeza zaidi kwa kupanda miti zaidi. Hili linafanywa kwa
uangalifu mkubwa kwa kuwa kuna baadhi ya miti si rafiki mzuri kwa vyanzo
vya maji inayakausha. Lakini si hivyo tu Bodi ya Wadhamini inaangalia
njia sahii ya kuhakikisha kwamba zinapatika fedha za kununulia miti
mipya. Wazo lililopo ni kuwakilisha mtizamo huu kwa wanajamii ili waweze
kutaarifiwa na kusikilizwa nini yatakuwa maamuzi yao kwenye
uchangishaji huo wa fedha. Changamoto nyingine ni uboreshwaji wa sheria
ndogondogo kwa kuwa hakuna mipaka ya majukumu baina ya Bodi ya Wadhamini
na Halmashauri ya serikali za vijiji. Kuna umuhimu wa suala hili
kuwekewa utaratibu mzuri wa kiuwajibikaji kwa sababu muda mwingine
vyombo hivi vinaweza kugongana kimawazo na kiutendaji na nani
anawajibika kwa nani.
“Hapo
nje kuna mikaratusi tumeikamata sisi kama Bodi ya Wadhamini. Mtu
ameangusha mti mbichi ambao haujakauka. Na ameiyangusha bila idhini.
Tumefanya hivi kwa kushirikiana na Mheshimiwa Diwani. Tunachosubili
tukae na serikali ya kijiji ili tujue tunafanya nini,” anafafanua
mraghbishi na Kaimu Katibu wa Bodi ya Wadhamini Jackson Nangiria. Kwenye
kukabidhiwa msitu mgeni rasmi alikuwa ni Mkuu wa Wilaya na Diwani wa
Kata ya Enguserosambu walikuwepo wakati wa kukabidhiwa kwa msitu huo
pamoja na wenyeviti wa vijiji vyote vinavyounda kata ya Enguserosambu.
Kwa hakika wenzetu wa Enguserosambu wameweza kujipanga na kuhakikisha
kwamba msitu wao wa enzi unabaki mikononi mwao.