Prof. Muhongo ataka kuharakishwa kwa uzalishaji wa nishati ya jotoardhi kwenye Ziwa Ngozi, Mbeya

Na Asteria Muhozya WAZIRI wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo ameiaigiza  Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi  Tanzania (TGDC... thumbnail 1 summary
Na Asteria Muhozya
WAZIRI wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo ameiaigiza  Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi  Tanzania (TGDC Ltd) kuwa ifikapo June 2016, iwe imeanza kuchoronga mashimo 3 katika eneo la Ziwa Ngozi ikiwa ni hatua ya mwisho inayohitajika kabla ya kuanza kujenga mitambo ya kuzalisha jotoardhi.

"Utafiti muhimu umekamilika. Joto la maji ni kubwa, 230-250C linalokidhi uzalishaji wa umeme. Hiki kitakuwa ni chanzo kipya muhimu cha umeme jadidifu" ,alisema Prof. Muhongo.

Ameongeza kuwa, jambo hilo haliwezi kuendelea kusubiri kutokana na mahitaji ya nishati hiyo nchini ikizingatiwa kuwa, Tanzania inapitiwa na  Bonde la Ufa kwa kiasi kikubwa.

"Tayari wenzetu Kenya na Ethiopia wamepiga hatua kubwa katika nishati hii lakni kwa upande wetu hatuna megawati hata moja kwa hili lazima tuchukue hatua tutoke hapa tulipo. Hakuna kusubiri anzeni na Ziwa Ngozi" amesema Muhongo.

Prof. Muhongo aliitaka Kampuni hiyo kuongeza nguvu katika eneo lenye viashiria vya jotoardhi la  Ziwa Ngozi kutokana na kuwepo maendeleo makubwa ya kitafiti ikilinganishwa na maeneo mengine yenye viashiria kama hivyo ikiwemo eneo la Mbaka lililopo Wilaya ya Rungwe.

"TGDC tunataka umeme wa jotoardhi, wananchi wanataka umeme, hawatakuwa kusikia maneno, ifikapo Mwezi juni na  mimi nitakwenda Ngozi kuangalia mmefikia wapi na kama hakuna maendeleo tutabadilisha timu ya wataalamu", alisisitiza Prof. Muhongo.

Akizungumzia kuhusu fedha za miradi, Prof. Muhongo alieleza kuwa, nchi nyingi duniani hazitegemei fedha za Serikali kutekeleza  miradi mikubwa ya nishati na ndiyo sababu hata Tanzania inatafuta fedha katika taasisi mbalimbali ikiwemo kukaribisha wawekezaji  ili kutekeleza miradi hiyo.

"Serikali kwa upande wake itasaidia kuwezesha upatikanaji wa fedha za kutekeleza miradi na ninyi kazi yenu ni kuhakikisha umeme wa jotoardhi unaanza kutumika Tanzania kwa kuanza na Ziwa Ngozi".

Naye Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro alisema kuwa amefarijika na maelekezo aliyoyatoa Prof. Muhongo na kuahidi kuweka nguvu kubwa katika kufuatilia suala hilo. " Ujio wako umetupa ari mpya katika kusimamia miradi hii kwa sababu rasilimali zipo lakini zimekaa tu nakuahidi kasi ya ufuatiliaji itaongezwa",alisema Kandoro

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Rugwe ,Mwalimu Zainabu Mbusi alieleza kuwa maagizo ya Prof. Muhongo yamekuwa faraja na kuongeza kuwa, kukamilika kwa mradi huo itaongeza kasi ya ukuaji uchumi na kuifanya Tanzania kufikia lengo lake la kuwa miongoni mwa nchi za uchumi wa Kati ifikapo 2025.

Kwa pande wake  Mbunge wa Jimbo la Busokelo, Fred Atupele alieleza kuwa, kukamilika kwa mradi huo kutachochea kasi ya uendelezaji wa viwanda vikubwa na vidogo na kueleza kuwa, kwa nafasi yake  watachukua jukumu la kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa vyanzo hivyo.

Awali akieleza akieleza Mikakati ya Taasisi hiyo, Mkurugenzi wa TGDC , Mhandisi Boniface Njombe alisema eneo la Mbaka ni miongoni mwa maeneo ya maji moto yenye viashiria vya nishati ya jotoardhi.

Vilevile, alieleza hivi sasa wataalam kadhaa wamesambaa wakifanya tafiti za mwisho katika  eneo la Mbaka ili kuanisha mipasuko na maeneo ya kuchimba nishati hiyo na kuongeza kuwa, TGDC imelenga kwa  kuanza kuzalisha umeme wa jotoradhi  wa kiasi cha  megawati 200 huku lengo ikiwa ni kufikia megawati 5000.

Aidha, alieleza kuwa, mbali na kuzalisha umeme , maji moto yanaweza kutumika viwandani na majumbani katika kukausha mazao ikiwemo kuwa kivutio cha utalii kuoga kwa kuwa inaelezwa kuwa maji hayo yanatajwa kuwa tiba ya magonjwa ya ngozi.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazopitiwa na Bonde la Ufa eneo ambalo linatajwa kuwa na viashiria vya nishati ya jotoardhi.