Baada ya simu feki kuzimwa, tutupe wapi taka za mabaki yake?

Dotto Kahindi Kama wote tunavyojua kuwa serikali imekusudia kuzima simu feki nchini ifikapo Juni 17, 2016 ambapo maelfu ya si... thumbnail 1 summary
Dotto Kahindi

Kama wote tunavyojua kuwa serikali imekusudia kuzima simu feki nchini ifikapo Juni 17, 2016 ambapo maelfu ya simu yatatupwa na watu takribani milioni 1.2  wataathiriwa na hatua hiyo

Pamoja na kulalamikiwa na watu wengi hasa wananchi wenye kipato cha chini kuwa mpango huu utakuwa mateso kwa wanachi hao lakini mamlaka husika zimesisitiza kuwa  ni muhimu kuzima simu feki zote ili kupunguza tatizo la wizi kwa kutumia mitandao ya simu inayofanywa zaidi za simu za aina hiyo.

Nakubaliana na serikali kuwa faida za kuzima simu simu feki ni kubwa kuliko kuacha matumizi ya simu hizo yakiendelea lakini swali langu la msingi ambalo pengine wengi hawajaliangalia ni wapi mabaki ya simu feki zitakazozimwa tutaenda kuyatupa

Taka hizi za kielectroniki (e-waste) zina madhara makubwa kwa mwanadamu na mazingira endapo hazitahifadhiwa kiutaalamu na kuzingatia athari zake katika mazingira.

Taka hizi nyingi hubeba madini ya Mercury na kemikali nyingine hatarishi ambazo madhara yake ni makubwa mno katika maisha ya wanadamu, viumbe hai na hata mimea.

Kwa wasiofahamu merchury ya mfumo wowote ule ni sumu na huathiri mfuo wa fahamu, chakula na figo. Sumu ya mercury inaweza kupeneza na kuingia mwilini kwa njia ya mfumo wa kuvuta mvuke katika hewa yenye mercury, kula, kuchoma sindano au kufyonzwa  kwa njia ya ngozi

Kwa njia hizo za namna sumu hiyo inavyoweza kusambaa, kipi tunaweza kufanya, kuzikusanya na kuzitupa kwenye majalala? Kuzichoma? Najua kuna wengine kwakuwa walizipenda sana simu zao watataka walau waziweke kwenye kabati kama kumbukumbu, sijui nao watakuwa salama

Hatari ya taka hizi ni kubwa mno, mvua ikinyesha hubeba vipande vya mabaki ya vifaa vya kielectroniki ambavyo huwa na sumu hizo mpaka kwenye maji, ambayo maji haya baadae hutumika kwa kuoga, kufua, na kunywa wakati mwingine. Unaweza kupata picha ya madhara yake yanaweza kutufikia kirahisi kwa namna gani.

Ukisema uchome moto hizi taka, nayo ni hatari kubwa, maana moshi wake umejaa sumu kali ambayo inaweza kukupata kwa kuvuta moshi wake. Madhara ni mengi sana lakini turejee katika swali la msingi. 

Je serikali yetu kupitia wataalamu wa mazingira wamelitafakari hili kwa makini? Je kuna njia ya kitaalamu ambayo wataitumia kuhifadhi na kuziteketeza taka hizi? Je kuna utaalamu wa kutosha hapa nchini wa kubadili matumizi ya taka hizo (recycling, reuse)? 

Nategemea kuona hatua madhubuti zinachukuliwa na mamlaka husika, kwa kutueleza baada ya simu zetu kuzimwa, mabaki yake tukayatupe wapi.