Serikali yapiga marufuku matumizi ya plastiki na viroba

Hakuna kitu kinachowaharibu vijana wa Tanzania kama madawa ya kulevya na viroba. Lakini wakati vita dhidi ya biashara ya madawa... thumbnail 1 summary
Hakuna kitu kinachowaharibu vijana wa Tanzania kama madawa ya kulevya na viroba.
Lakini wakati vita dhidi ya biashara ya madawa ya kulevya ikionekana kuendelea kuwa ngumu, serikali inakaribia kupata ushindi kwenye vita dhidi ya viroba. Serikali imetangaza kupiga marufuku utengenezaji, usambazaji na uingizaji wa plastiki nchini hadi kufikia mwaka 2017.

Hiyo inamaanisha kuwa viroba vitakuwa vimechimbiwa kaburi lake moja kwa moja. Uamuzi huo umetangazwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) January Makamba wakati akizungumza na waandishi wa habari Jumapili. 

Alidai kuwa mifuko hiyo ambayo mingi hutolewa bure imekuwa mstari wa mbele katika uchafuzi wa mazingira nchini. Alisema uamuzi huo utaanza kutekelezwa ili kuwapa muda wafanyabiashara wanaoingiza mkate wa kila siku kupitia biashara hiyo kutafuta nyingine mapema kabla mambo hayajawa magumu kwao. 

Pamoja na kuharibu nguvu kazi ya taifa, viroba ambavyo hutumiwa na vijana wengi katika muda ambao walipaswa wafanye kazi, mifuko yake imekuwa ikichafua mazingira ikiwa ni pamoja na kuziba mifereji mbalimbali ya kupitisha maji.

Hata hivyo kuzuiwa kwa mifuko ya plastiki kutawafanya watengenezaji wa vilevi vya bei chee kufikiria njia mbadala ya kufungasha zaidi ya chupa zilizoeleka.

Chanzo: Bongo5