KINAMAMA WAHAHA KUTAFUTA MAJI MPWAPWA

na Danson Kaijage, Mpwapwa WANAWAKE wa Kijiji cha Iyoma, wilayani Mpwapwa wanalazimika kutembea saa mbili hadi tatu kwa ajili ya kut... thumbnail 1 summary

na Danson Kaijage, Mpwapwa
WANAWAKE wa Kijiji cha Iyoma, wilayani Mpwapwa wanalazimika kutembea saa mbili hadi tatu kwa ajili ya kutafuta maji kwa matumizi ya kawaida.
Hayo yalielezwa na wanakijiji wa kijiji hicho kwenye mkutano wa hadhara na Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Christopher Kangoye.
Mkuu huyo alilazimika kukutana na wananchi kwa lengo la kutoa elimu, juu ya uzalishaji wa kipato na utunzaji wa mazingira wilayani hapo.
Wanakijiji hao walisema pamoja na serikali kuwahimiza kuwa na maendeleo, lakini wanasahau kuwa bado wanakosa maji ya uhakika ambayo ni huduma muhimu katika maisha ya kiumbe hai.
Mmoja wa wananchi ambaye alijitambulisha kwa jina la Jackson Noah, alisema kuwa kitendo cha kukosa maji katika maeneo yao, kinasababisha wake zao kuyafuata umbali mrefu.
Noah alisema kitendo cha kinamama kuamka saa kumi alfajiri kufuata maji kwa umbali mrefu, ni sababu kubwa ya kukosekana kwa maendeleo kwani nguvu kazi inapotelea katika kufuata maji.
Naye Zaina Bakari alisema kijiji hicho kwa miaka kumi sasa wananchi wanatumia maji ya kwenye madimbwi wanayogombania kati yao na wanyama.
Zaina alisema kutokana na tatizo hilo, uzalishaji umepungua kijijini hapo kutokana na akinamama wengi kujikita kwenye utafutaji maji badala ya kwenda kwenye shughuli za uzalishaji.
Chanzo: Tanzania Daima