Bagamoyo wapinga kizuizi cha TANAPA

na Julieth Mkireri, Bagamoyo MWENYEKITI wa baraza la mji mdogo wa Bagamoyo, Abdullzahoro Sharifu, ameuagiza uongozi wa Mamlaka ya Hifad... thumbnail 1 summary
na Julieth Mkireri, Bagamoyo
MWENYEKITI wa baraza la mji mdogo wa Bagamoyo, Abdullzahoro Sharifu, ameuagiza uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa nchini (TANAPA) kuondoa kizuizi kilichopo katika Kijiji cha Gama, Kata ya Magomeni wilayani humo kwani kimekuwa kero kwa wananchi.
Sharifu alitoa agizo hilo jana baada ya kutembelea na kuzungumza na wakazi wa Kitongoji cha Gama akisema pamoja na lengo zuri la TANAPA, lakini kizuizi hicho kimegeuka kuwa kero kwa wakazi hao.
Alisema kwamba kero hiyo si kwa wakazi wa Kitongoji cha Gama pekee bali na vitongoji jirani na Kijiji cha Matipwili, kwani wakazi hao wamewekewa muda wa kupita katika kizuizi hicho bila ya kujali shughuli za wakazi hao wanazofanya.
Akizungumzia suala hilo, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo, Shukuru Mbato, amekiri kuwapo kwa kero hiyo ambayo imekuwa ikiwakwamisha wakazi wa vijiji hivyo kufanya shughuli zao za maendeleo kwa muda wanaotaka.
Mbato alisema kutokana na hali hiyo anatarajia kumuomba Mkuu wa Wilaya hiyo, Ahmed Kipozi, kuongozana na wajumbe wa baraza la madiwani na wale wa mji mdogo kwenda kuzungumza na uongozi wa TANAPA na wakazi wa vitongoji hivyo ili suala hilo liweze kupatiwa ufumbuzi na kuondoa kero iliyopo kwa wananchi.

Una taarifa, picha za usafiri wa anga, mazingira, maliasili na utalii? tutumie kupitia kingkahindi@gmail.com