Umewahi kufuatilia viza kwa ajili ya
kwenda UK? Unakumbuka ilichukua siku ngapi? Nadhani habari hii itakuwa njema
kwako baada ya Serikali ya Uingereza kupitia Ubalozi wake nchini, kutangaza
huduma mpya ya haraka ya utoaji viza inayoitwa ‘huduma ya upendeleo ya utoaji
visa kwa haraka’ ili kuwawezesha Watanzania kupata viza hizo ndani
ya siku tano.
Balozi wa Uingereza nchini, Dianna Melrose, alisema huduma hiyo inalenga kuwasaidia waombaji wa visa kwa ajili ya shughuli za kibiashara, masomo kwa wanafunzi wanaokwenda kusoma nchini humo na zile za kusafiria, ili wapate haraka tofauti na nyuma kwani ilikuwa inatumia muda mrefu.
Balozi Melrose alisema huduma hiyo pia imelenga kukuza ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili na pia kusaidia kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo ya Tanzania na hivyo kuongeza ustawi na ajira kati ya pande hizo mbili.
Aliongeza kuwa huduma hiyo pia itawasaidia waombaji kusafiri kwa haraka pale wanapokuwa na shughuli zao za dharura.
Kwa mujibu wa Melrose, kuanzia sasa kupitia huduma hiyo, waombaji wanapaswa kulipia Paundi za Uingereza 100 (sawa na Sh. 250,000) ambazo zinaweza kulipwa kwa njia ya mtandao kwa kujaza fomu na pia kutembelea ofisi za Ubalozi huo kitengo cha viza.
CHANZO: NIPASHE