Mamlaka
ya Hifadhi za Taifa TANAPA imezindua tuzo za umahiri wa habari kwa Mwaka 2013
na kuwataka Wanahabari kote nchini kujitokeza katika kinyang’anyiro hicho
kinachozipambanisha kazi bora za habari zinazoyaangalia maeneo ya uhifadhi hapa
nchini na utalii wa ndani.
Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini
Arusha, Meneja Uhusiano wa TAPANA Pascal Shelutete amesema kuwa lengo la tuzo
hizo ni kuendelea kuwahamasisha Waandishi wa Habari kuona wajibu wao wa
kitaaluma katika kuibua taarifa mbalimbali zenye usahihi juu ya changamoto na
mafanikio yanayoizunguka sekta ya utalii hapa nchini.
Shelutete amesema tuzo hizo zinafanyika wakati
ambapo sekta ya Utalii hapa nchini imekuwa ikikabiliwa na vitendo vingi vya
ujangiri vinavyotia dosari harakati za uhifadhi wa maliasili huku katika suala
la Utalii wa ndani bado Watanzania hawajitokezi kwa wingi kuzitembelea Hifadhi
za Taifa.
Katika tuzo za Mwaka huu TANAPA imefanya
maboresho ya zawadi hususani katika viwango vya fedha ambapo Washindi wa kwanza
kwa kila kipengele watakabidhiwa Shilingi Milioni mbili, washindi wa pili
Shilingi milioni moja na nusu na washindi wa tatu shilingi milioni moja huku
baadhi ya washindi hao wakipata nafasi ya kujifunza uhifadhi na utalii wa ndani
katika hifadhi za Tanzania na nje ya nchi.
Mwaka 2012 katika tuzo za umahiri wa habari za
uhifadhi na utalii wa ndani Wafanyakazi wawili wa Kampuni ya Sahara Media Group
SMGL walipata tuzo kwa upande wa Televisheni na Magazeti kupitia habari na
vipindi walivyoviwasilisha katika tuzo hizo zinazoandaliwa na Mamlaka ya
Hifadhi za Taifa TANAPA.