TANAPA WAZINDUA TUZO ZA UMAHIRI WA HABARI 2013

Mamlaka ya Hifadhi za Taifa TANAPA imezindua tuzo za umahiri wa habari kwa Mwaka 2013 na kuwataka Wanahabari kote nchini kujitokeza katika ... thumbnail 1 summary
Mamlaka ya Hifadhi za Taifa TANAPA imezindua tuzo za umahiri wa habari kwa Mwaka 2013 na kuwataka Wanahabari kote nchini kujitokeza katika kinyang’anyiro hicho kinachozipambanisha kazi bora za habari zinazoyaangalia maeneo ya uhifadhi hapa nchini na utalii wa ndani.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Arusha, Meneja Uhusiano wa TAPANA Pascal Shelutete amesema kuwa lengo la tuzo hizo ni kuendelea kuwahamasisha Waandishi wa Habari kuona wajibu wao wa kitaaluma katika kuibua taarifa mbalimbali zenye usahihi juu ya changamoto na mafanikio yanayoizunguka sekta ya utalii hapa nchini.
Shelutete amesema tuzo hizo zinafanyika wakati ambapo sekta ya Utalii hapa nchini imekuwa ikikabiliwa na vitendo vingi vya ujangiri vinavyotia dosari harakati za uhifadhi wa maliasili huku katika suala la Utalii wa ndani bado Watanzania hawajitokezi kwa wingi kuzitembelea Hifadhi za Taifa.
Katika tuzo za Mwaka huu TANAPA imefanya maboresho ya zawadi hususani katika viwango vya fedha ambapo Washindi wa kwanza kwa kila kipengele watakabidhiwa Shilingi Milioni mbili, washindi wa pili Shilingi milioni moja na nusu na washindi wa tatu shilingi milioni moja huku baadhi ya washindi hao wakipata nafasi ya kujifunza uhifadhi na utalii wa ndani katika hifadhi za Tanzania na nje ya nchi.

Mwaka 2012 katika tuzo za umahiri wa habari za uhifadhi na utalii wa ndani Wafanyakazi wawili wa Kampuni ya Sahara Media Group SMGL walipata tuzo kwa upande wa Televisheni na Magazeti kupitia habari na vipindi walivyoviwasilisha katika tuzo hizo zinazoandaliwa na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa TANAPA.