na Datus Boniface
KAMPUNi ya ndege ya Fly 540 inayofanya safari zake hapa nchini, imeahidi kuboresha huduma zake ili tatizo la hitilafu lililojitokeza hivi karibuni lisijirudie.
Akizungumza na Tanzania Daima kwenye viwanja vya Maonyesho ya Sabasaba, Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Brown Francis, aliahidi kuwa watahakikisha hali kama ile haitokei tena.
"Tunawaomba radhi wateja na kuwataka wasamehe na kusahau kwani uongozi na wafanyakazi wa kampuni hii wanawahakikishia kutotokea kwa tatizo kama hilo tena,” alisema.
Alisema kwa kutambua umuhimu na unyeti wa tatizo hilo kibiashara, wateja wao na Watanzania kwa ujumla, Fly 540 wanafanyakazi kwa lengo la kuboresha huduma ambapo ndege moja ya kampuni ipo katika matengenezo ya kubadilishwa injini na baada ya kukamilika watatangaza ruti mpya.
Akifafanua kuhusiana na hitilafu iliyojitokeza na abiria wake kushindwa kusafiri, Francis alisema ilitokea kwenye injini mara tu baada ya kutua Mwanza, ambapo mafundi waliirekebisha lakini katika hali ya kusikitisha jitihada hizo hazikufanikiwa.
Alisema hali hiyo ni kutokana kuharibika kwa kifaa ambacho hakikuweza kupatikana mara moja na badala yake ilibidi kikanunuliwe jijini Nairobi, Kenya.
Chanzo: Tanzania Daima