Walimu walala madarasani Katavi

na Walter Mguluchuma, Mpanda   SHULE za  msingi  za Mnyamasi  na Moto  zilizopo  wilayani  Mlele Mkoa wa Katavi, zinakabiliwa  na  ch... thumbnail 1 summary

na Walter Mguluchuma, Mpanda
 
SHULE za  msingi  za Mnyamasi  na Moto  zilizopo  wilayani  Mlele Mkoa wa Katavi, zinakabiliwa  na  changamoto  kadhaa  zikiwamo   walimu  kuishi   katika  vyumba   vya  madarasa  huku  wanafunzi  wakisomea  chini  ya  miti.

Haya yalibainika wakati wakati wa  ziara ya Mkuu  wa Wilaya  hiyo, Kanali Ngemela Lubinga, katika  kata za Nsimbo  na  Mamba kwaajili ya kujitambulisha, kukagua miradi ya  maedeleo na kusikiliza kero za wananchi.

Mwalimu  Mkuu  wa  Shule  ya  Msingi  Majimoto, Delamu Binde  alimfahamisha mkuu  huyo kuwa kutokana  na uhaba  wa vyumba za  walimu katika Shule ya Msingi Mnyamasi, walimu  wanne  wamelazimika  kuishi  katika  vyumba vya  madarasa shuleni hapo.

Akisoma  taarifa   kwa  niaba ya Mkuu  wa  Shule  ya  Msingi  Namasi, mkuu  huyo wa shule, alisema kuwa shule hiyo yenye walimu  sita wa kiume, wanne  kati yao  wamelazimika  kuishi katika vyumba vya madarasa.

Binde aliongeza kuwa wanafunzi wa shule hizo  za  Majimoto na Mnyamasi, wanasomea chini ya miti kufuatia  uhaba mkubwa wa  vyumba vya madarasa na madawati unaozikabili.

“Shule ya Msingi Majimoto  ina wanafunzi 1,661 na kati yao 420 tu ndio wanakalia madawati  huku wengine 1,241 wakilazimika kukaa  chini,” alisema.

Akizungumza kwa niaba  ya Ofisa  Elimu  wa wilaya hiyo, Marius Nazi,  alisema  kuwa  tayari ofisi  hiyo imeshatengeneza  madawati  zaidi  ya 7,000  ambayo  yatagawiwa  katika mbalimbali hivi  karibuni  ili kukabiliana na kadhia hiyo ya upungufu.

Ili  kuondokana na adha ya walimu  kuishi  katika  vyumba  vya madarasa, alisema tayari ofisi  yake  imetengewa  zaidi  ya sh  milioni 30 kwa ajili  ya ujenzi  wa  nyumba  za  walimu  shuleni hapo.

Chanzo: Tanzania Daima